Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano

Hon. Edward Franz Mwalongo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Njombe Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano

MHE. EDWARD F. MWALONGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa nianze kwa kumpongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli kwa kazi nzuri ya kutuongoza Watanzania. Pili, nampongeza sana Mheshimiwa Waziri na watendaji wote wa Wizara yake kwa jinsi wanavyowajibika kuwahudumia Watanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nijikite katika hoja tatu.
(i) Wakazi waliopo pembezoni mwa Uwanja wa Ndege Njombe.
(ii) Ujenzi wa Uwanja wa Ndege Njombe.
(iii) Ujenzi wa barabara ya Itoni - Manda kwa kiwango cha lami.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wananchi waishio pembezoni mwa Uwanja wa Ndege Njombe Mjini hawatendewi haki na hawajui hatma yao. Naiomba Serikali itoe ufafanuzi juu ya wananchi hawa kwani hawafanyi maendelezo, hawapewi hati na wala hawakopesheki. Hii kwa kweli ni kuwanyima maendeleo, ni vizuri sana Serikali ikatoa ufafanuzi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Uwanja wa Ndege wa Njombe katika Ilani ya CCM umetamkwa kwamba utawekwa lami. Niombe Serikali sasa itekeleze ahadi hii. Njombe sasa inakua kisiwani kwa kukosa huduma ya usafiri wa ndege kwa kukosa uwanja. Naiomba Serikali ituone na sisi Wananjombe tunahitaji uwanja ili tuendane na kasi na mafanikio ya nchi yetu kwa kupata usafiri wa ndege.

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara ya Itoni - Manda nayo imo kwenye Ilani ya CCM. Ukiacha miradi ya kielelezo iliyopo Ludewa, maeneo ambayo barabara hii inapita ndiyo maeneo muhimu sana ya uzalishaji wa chakula, mbao, nguzo na chai. Wakulima na wafanyabiashara wametaabika kwa miaka mingi sana kwa kusafirisha mazao katika barabara hii. Serikali imeanza kazi ya kuweka zege barabara hii eneo la Mkiu hadi Mawengi kilometa 50 ndani ya Jimbo la Ludewa. Niishauri Serikali, kazi hii ianzie Itoni kuelekea Mkiu kwani itasaidia kuondoa ugumu wa usafirishaji wa mazao ya wananchi katika Kata za Uwembe, Luponde, Matola ndani ya Jimbo la Njombe Mjini na Kata ya Madope, Jimbo la Ludewa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuwasilisha na naunga mkono hoja.