Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano

Hon. Augustino Manyanda Masele

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbogwe

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano

MHE. AUGUSTINO M. MASELE: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hotuba ya Mheshimiwa Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano. Wizara hii ndiyo uti wa mgongo wa Tanzania ya Viwanda. Sekta zote za uzalishaji wa kilimo na sekta nyingine zote, za biashara, utalii, miundombinu ya umeme usafirishaji wa bidhaa na watu, vifaa ya ujenzi ili viweze kufikiwa na kusafirishwa Wizara hii ina mchango mkubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa dhati kabisa nampongeza Mheshimiwa Rais, Mheshimiwa Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Naibu Waziri, Makatibu Wakuu na Watumishi wote wa Wizara hii kwa kazi nzuri. Kipekee nimpongeze kwa dhati Mhandisi Patrick Mfugale kwa utumishi wake uliotukuka na mchango wake wa kipekee katika ujenzi wa barabara za lami na sasa amekuwa kiongozi wa timu ya wahandisi ambao wamefanya upembuzi yakinifu na upembuzi wa kina hadi kuanza kwa ujenzi wa reli ya standard gauge unaofanywa na Kampuni za Yapi Merkez Insaat Ve Sanayi na Mota-Engil inayojenga reli aina hii kutoka Dar es Salaam – Morogoro, hongera sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niipongeze Wizara hii kwa kazi nzuri ya ujenzi wa barabara za lami chini ya usimamizi wa Mhandisi Patrick Mfugale. Niiombe Serikali ione uwezekano wa kumpatia nishani kwa ajili ya kuutambua mchango wake kwa Taifa hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niipongeze Serikali kwa ujenzi wa madaraja makubwa pamoja na flyovers, mradi wa DART, pamoja na Daraja la Mwalimu Nyerere – Kigamboni. Niombe pia Mradi wa Daraja la Kigongo – Busisi lisanifiwe na kujengwa ili kurahisisha mawasiliano katika Kanda ya Afrika Mashariki na kuondoa vikwazo vya vivuko kwenye Ziwa Victoria.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niiombe Serikali na Wizara izipandishe hadhi barabara za Bwelwa – Ushirombo – Ivumwa, Nyaruyeye, Nyarugusu, Nyabulolo – Buyegu, Geita. Ujenzi kwa kiwango cha lami barabara ya Butengolumasa, Iparamasa, Mbogwe, Masumbwe. Barabara hii ni kiungo cha barabara ya Isaka – Masumbwe, Mbogwe, Iparamasa, Butengo Lumasa, Chato, Muleba, Bukoba, Mtukula hadi nchini Uganda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ununuzi wa ndege ni hatua maridhawa katika kuitangaza nchi yetu Kimataifa na hivyo kusaidia kukuza sekta ya utalii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naishauri Serikali iendelee kutenga pesa kwa ajili ya Mfuko wa Mawasiliano kwa Wote (UCSAF) ili ujenzi wa minara katika maeneo yenye usikivu hafifu yapatiwe huduma hii hasa katika Kata za Ilolangulu, Ikobe, Isebya, Nyasato, Ikunguigazi (Kagera). Shirika la Simu Tanzania (TTCL) lipatiwe uungaji mkono kifedha ili liwekeze zaidi na limudu ushindani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono.