Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano

Hon. Daimu Iddi Mpakate

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tunduru Kusini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano

MHE. DAIMU I. MPAKATE: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kutoa maelezo yangu ya kuchangia hotuba ya bajeti ya Wizara ya Ujenzi, Mawasiliano na Uchukuzi kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Halmashauri ya Wilaya ya Tunduru kuna uwanja wa ndege ambao kwa sasa umezuiliwa kutumika kwa kuwa upo katika Kata ya Mji. Halmashauri imetenga eneo lingine la kujenga uwanja wa ndege. Hivyo tunaomba uwanja ule wa zamani upewe Halmashauri ili kujenga majengo ya huduma za jamii. Kwa kuwa eneo la Hospitali ya Wilaya limebana sana, hilo eneo linaweza kutumika kuongezea eneo la Hospitali ya Wilaya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, majengo ya Halmashauri ya Wilaya limebana, hivyo sehemu ya uwanja huo inaweza kusaidia Halmashauri ya Wilaya kuongeza majengo kwa ajili ya kutolea huduma. Magereza nao eneo limebana sana kiasi kwamba hawana uwezo wa kujenga chochote. Hivyo eneo hili litasaidia Magereza kupata eneo la kuongeza majengo hasa nyumba za Askari wa Magereza na nyumba za Askari Polisi. Hivyo, tunaliomba sana eneo hili likabidhiwe kwa Halmashauri ili litumike kuongeza majengo mbalimbali ya Halmashauri na Serikali Kuu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Tunduru Kusini imepakana na Msumbiji kupitia Mto Ruvuma, maeneo mengi ya Vijiji hayana huduma ya simu. Maeneo hayo ni Makade, Msinji, Semei, Chikomo, Lukala, Misyaje, Mbati, Nasumba na Likweso. Naomba sana maeneo hayo yajengewe minara ya simu ili iwe rahisi kuwasiliana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna tatizo la usikivu wa redio katika Wilaya ya Tunduru TBC, haipatikani kabisa. Hivyo tunaomba mdau aliyejitokeza kuweka Kituo cha Redio Tunduru, apewe frequency haraka ili wananchi wa Tunduru wapate huduma ya redio, kwani ni muda mrefu sana anapeleka maombi lakini hajapewa kibali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande wa barabara, Jimbo la Tunduru Kusini lina barabara kuu inaunganisha na Wilaya ya Namtumbo kutokea Mtwaro – Pachani – Lusewa – Lingusenguse – Nalasi mpaka Tunduru Mjini. Nashukuru kwa kipande cha Mtwaro – Pachani mpaka Nalasi, kipo katika mchakato wa upembuzi yakinifu. Hivyo naomba kipande kilichobaki cha Nalasi – Mbesa Tunduru chenye urefu wa kilomita 64 nacho kiingie kwenye mpango huu wa kufanya upembuzi yakinifu, tayari kwa kujengwa kwa kiwango cha lami kwani kipande hiki ni korofi na kinasumbua sana wakati wa kifuku na Tarafa hii ndiyo yenye idadi kubwa ya watu ambao wanatumia barabara kufuata huduma za kijamii Tunduru Mjini. Barabara hii ndiyo inayotumiwa na wananchi wa Tunduru kwenda kwenye Hospitali ya Mission Mbesa ambayo inahudumia zaidi ya asilimia 70 ya wananchi wa Wilaya ya Tunduru pamoja na Wilaya jirani ya Namtumbo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara ya Njombe – Songea ina umri wa zaidi ya miaka 30 tangu ianze kutumika na sasa imechakaa sana, ina viraka vingi ambavyo vinaweza kusababisha magari kupata ajali. Barabara hii inapaswa ijengwe upya kwa kuwa ni muda mrefu sana na imechoka sana na sasa magari yanaumia sana kutokana na ubovu wa barabara hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Mji wa Tunduru kuna eneo la makutano ya barabara inayotoka Masasi na Songea (cross road). Mahali hapa panatakiwa kujenga round about, lakini kuna sheli imejengwa hapo kimakosa, kwa sababu ipo ndani ya eneo la barabara. Hivyo tunaomba sheli ile ibomolewe na ijengwe round about, kwa sababu eneo hili limejengwa vibaya na linasababisha ajali za mara kwa mara na kusababisha vifo kutokana na makutano haya kujengwa bila mpangilio wa kiusalama kwa watumiaji.