Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Waziri Mkuu kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

Hon. Amb Dr. Diodorus Buberwa Kamala

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nkenge

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Waziri Mkuu kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

MHE. BALOZI DKT. DIODORUS B. KAMALA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa fursa ya kuchangia hotuba muhimu iliyowasilishwa leo hii.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nianze kwa kutoa pongezi zangu za dhati kwa kazi nzuri inayofanywa na Mheshimiwa Rais, Mheshimiwa Waziri Mkuu na Serikali kwa ujumla kwa kutekeleza kwa ufundi na ustadi mkubwa Ilani ya Uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sote ni mashahidi, yako mambo mengi ya kuthibitisha hilo, mambo mawili yanathibitisha jinsi Ilani inavyotekelezwa vizuri, Serikali imeweza kuongeza mapato kutoka bilioni 870 Novemba, 2015 hadi trilioni 1.3 kwa mwezi ilipofika Machi, 2016. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia Serikali imeweza kuanza kutekeleza mkakati wa elimu bure hata kabla ya bajeti mpya ya 2016/17 haijawekwa, hiyo imewezekana tu kwa kubana matumizi, kupunguza matumizi yasiyokuwa ya lazima, yakaelekezwa kwenye utekelezaji wa elimu bure. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo kubwa tunalojifunza baada ya kuanza kutekeleza elimu bure ni kwamba ukiangalia shule ya awali pamoja na darasa la kwanza uandikishaji wa wanafunzi wameongezeka zaidi ya asilimia 100. Kwa maneno mengine, wako Watanzania wengi walioshindwa kuanza shule ya awali, walioshindwa kuanza darasa la kwanza, kwa sababu ya gharama zisizokuwa na tija ambazo wazazi walikuwa wanalazimishwa kwamba lazima zilipwe hivyo kuna watoto walioshindwa kuendelea na shule, sasa baada ya kuanza kutekeleza elimu bure tunaona vijana wakiongezeka.
Mheshimiwa Mwenyekiti, maana yake ni kwamba wako wengi tuliowapoteza. Ni matarajio yangu katika Wizara inayohusika itakuja na mpango wa kuonesha ni jinsi gani wale tuliowapoteza Watanzania wengi tu ni kwa jinsi gani tutaweza kuwapa elimu ya msingi kwa sababu wao tayari wameshaikosa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nichukue nafasi hii kumshukuru Mheshimiwa Waziri Mkuu, kwa ziara aliyoifanya katika Jimbo langu la Nkenge, na pia kuweza kutembelea Wilaya ya Misenyi, kwa kweli niseme amekuwa Waziri Mkuu wa kwanza kutembelea kata ya Kakunyu katika Wilaya ya Misenyi, nampongeza sana. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri Mkuu, katika ziara ile alitoa maelekeza mbalimbali ambayo yatasaidia kumaliza mgogoro kati ya wakulima, wafugaji wazawa, na wawekezaji mbalimbali waliopewa blocks katika Ranchi ya Misenyi. Matarajio yangu ni kwamba maelekezo hayo yataweza kutusaidia kuondoa mgogoro uliodumu kwa zaidi ya miaka 15 na ningependa kuchukua nafasi hii kushauri baadhi ya mambo yakizingatiwa yatatusaidia kumaliza mgogoro huo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la kwanza ambalo lazima lizingatiwe ni dhana na maneno ya watu ambao wamekuwa wakisema vijiji vilivyo ndani ya Kata Kakunyu, Kilimilile, Nsunga na Mtukula viliingilia maeneo ya Ranchi za Mabale pamoja na Misenyi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, vijiji hivi vilikuwepo kabla ya Ranchi mbili za Mabale na Misenyi hazijaanzishwa. Kwa hiyo, wale wanaosema vijiji viliingilia maeneo ya ranchi kuanzia leo naomba waseme kwamba ni Ranchi za Mabale na Misenyi zilizoingilia maeneo ya vijiji kwa sababu vijiji vilikuwepo na vilishasajiliwa na vinatambulika Kiserikali na vina hati. Kwa kuwa vijiji ndivyo vilitangulia kuwepo kabla ya ranchi ni makosa na dharau kwa wananchi wa Misenyi kusema wameingilia ranchi wakati wao walikuwepo hata kabla ya ranchi haijakuwepo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo nashauri lizingatiwe Mheshimiwa Waziri Mkuu alipotembelea kule na kutoa maelekezo, tunatarajia kwamba Mawaziri watayafanyia kazi na bado wanaendelea kuyafanyia kazi. Kabla hawajamaliza kuyafanyia kazi, wananchi wameshaanza kubugudhiwa, tarehe 17 mwezi uliopita na tarehe 18 mwezi huu, baadhi ya wananchi wamenyang’anywa majembe ili wasiendelee na kilimo. Kufanya hivyo ni kuchelewesha kutekeleza sera ya Hapa Kazi tu! pia ni kutoheshimu maelekezo ya Mheshimiwa Waziri Mkuu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo lazima lizingatiwe ili tupate ufumbuzi wa kudumu ni lazima Waziri wa Mifugo ashirikiane na Waziri wa Ardhi, ashirikiane na Waziri wa Ulinzi na Waziri wa TAMISEMI; nina uhakika hawa wote wakishirikiana kwa pamoja na siyo kila mmoja anakwenda kwa wakati wake na kufanya yanayomhusu eneo lake, tutaweza kupata ufumbuzi wa kudumu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niseme na nisisitize kwamba kuna umuhimu ukiangalia mpango wa pili wa maendeleo wa miaka mitano ambao tunalenga kuutekeleza unabainisha kwamba tunahitaji trilioni 107 kuweza kuutekeleza, na kati ya hizo Serikali itatoa trilioni 59 na zilizobaki zitatolewa na private sector, hivyo, ukiangalia Mpango wa Pili tunaopanga kuutekeleza, sehemu kubwa ya fedha zitatokana na private sector. Sasa ili private sector waweze kufanya kazi lazima tuongeze nguvu za kujenga mazingira wezeshi kama ambavyo imebainishwa katika hotuba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mazingira wezeshi ni muhimu kwa sababu ndiyo yatawezesha private sector kuweza kuchangia vizuri katika utekelezaji wa Mpango wetu. Nitaeleza mambo matatu muhimu kama mfano wa mambo muhimu ambayo yakifanywa na ambayo hayahitaji fedha za kigeni kuyafanya, lakini ukiyafanya unaweza kusaidia kuharakisha utekelezaji wa Mpango wa Pili wa miaka mitano.
Mheshimiwa Mwenyekiti, moja, kwa mfano, hivi sasa hapa Tanzania viwanda vinavyozalisha simenti vikitaka kuuza simenti yake ndani ya Afrika Mashariki vinalazimika kutafuta kibali kutoka kwa Mkemia Mkuu kabla hawajauza, lazima watoe asilimia 2.5 ya thamani ya simenti wanayouza. Ukifanya hivyo unakwamisha viwanda bila sababu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa wananchi wa Mkoa wa Kagera wanapotumia sukari na wengine wa Kanda ya Ziwa na Watanzania wengine kila kilo ya sukari inakatwa kodi ya reli. Sasa mtu unajiuliza, kuna uhusiano gani kati ya sukari na kodi ya reli? Utaratibu huu unaongeza gharama ambazo hazina tija.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia tunaambiwa waliopo kwenye kilimo cha alizeti kama wataanzishiwa utaratibu wa kupata mbegu mpya wataweza kuongeza ajira kutoka milioni moja ya Watanzania wanaopata ajira hivi sasa hadi Watanzania milioni kumi, lakini ili kupata mbegu mpya waliopo kwenye sekta ya alizeti kwa Tanzania unahitaji miaka saba ili kuweza kupata kibali cha kupata hiyo mbegu mpya, wakati Uganda wanahitaji miezi sita tu ya kuweza kupata hiyo mbegu mpya.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niseme kwamba naunga mkono hoja na naomba nimalizie kwa kusisitiza kwamba ili tuweze kujenga Tanzania yenye viwanda, lazima tuhakikishe tunaunga mkono zoezi la Export Processing Zones na tutafanya hivyo kwa kutenga maeneo na kuhakikisha maeneo ya wawekezaji yanapatikana siyo ya kutafutwa. Vilevile kule Nkenge kuna mpango mkubwa wa kujenga uwanja wa Kimataifa wa Mkajunguti natarajia kwenye bajeti hii zitatengwa fedha za kulipa fidia kama tulivyoahidi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kwa kupitia Wizara ya Viwanda tunataka kuanzisha Export Processing Zone ya Kimataifa ili uwanja wa kimataifa wa Mkajunguti usiwe uwanja tu usiyokuwa na cha kusafirisha, vilevile tuwe na Export Processing Zone. Tukifanya hayo tunaweza kupiga hatua na kwenda kwa kasi zaidi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la mwisho tuondoe utitiri wa ukiritimba katika kuratibu masuala mbalimbali. Kwa mfano, mwekezaji yeyote akitaka kuwekeza Tanzania lazima kabla hajaanza kufanya hivyo aende TBS kutafuta kibali, lazima aende TFDA kutafuta kibali cha kitu kile kile, akitoka huko lazima aende kwa Mkemia Mkuu wa Serikali. Sasa ukiangalia yote haya yanaongeza ukiritimba usio kuwa wa lazima na kama Mheshimiwa Waziri Mkuu alivyosema Tanzania ni ya 139 sasa ili tuweze kuboresha mazingira ya wawekezaji, lazima hatua za makusudi zichukuliwe.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.