Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano

Hon. Willy Qulwi Qambalo

Sex

Male

Party

CHADEMA

Constituent

Karatu

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano

MHE. QAMBALO W. QULWI: Mheshimiwa Naibu Spika, Nakushukuru kwa kunipa nafasi jioni hii ya leo ili nami niweze kuchangia Wizara hii muhimu sana katika maendeleo ya watu wetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, nianze na eneo hili la kisera. Suala la kuunga mikoa limesemwa jana katika hotuba zote tatu, wachangiaji tangu jana na leo na hata ripoti zote hizo zimebainisha kwamba kuna mikoa yetu mingi bado haijaungwa. Ukienda Kaskazini, ukienda Magharibi, ukaenda na Kusini hali ni hiyo hiyo. Kwa hiyo, naishauri Serikali kama tulikubaliana tuanze na kuunga mikoa hebu tuunge hiyo mikoa.

Mheshimiwa Naibu Spika, sina uhakika kama miradi yote iliyopo kwenye vitabu hivi ni ya mikoa, kuna miradi ya Wilaya, tusichanganye kama tulikubaliana tuunge mikoa tumalize kuunga mikoa kwanza halafu tushuke kwenye hizo ngazi zingine. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, haiingii akili ya kawaida mtu uko Mahenge, uko Ifakara unataka kwenda Lindi na Mtwara urudi Morogoro, uende Dar es Salaam ndiyo ushuke kwenda kule chini, haiingii akilini kwa kawaida. Mnavyofahamu barabara ya kwenda Dar es Salaam jinsi ambavyo ina changamoto zake nyingi. Hivyo, naishauri Serikali hebu tufanye jambo hilo kwanza. Watanzania wengi tena wale wa hali ya chini usafiri wao siyo ndege, usafiri wao siyo meli, usafiri wao ni treni na barabara. Treni haipiti maeneo yote, twendeni tukajenge hizo barabara zinazounga mikoa yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ninamshukuru Mheshimiwa Chenge asubuhi ya leo, ameongea vizuri sana kuhusu barabara inayounga Mkoa wa Simiyu na Mkoa wa Arusha. Ukiwa Arusha ukitaka kwenda Musoma ni budi upitie Singida
- Mwanza - Musoma. Hakuna barabara inayounga Arusha na Musoma, hakuna barabara inayounga Arusha na Simiyu, hakuna barabara inayounga Manyara na Simiyu, hakuna barabara inayounga Manyara na upande huu wa Tanga.

Tunafanya nini? Kwa hiyo, nadhani tufanya jambo hilo la kisera ambalo tumekubaliana. Barabara ya Oldeani Junction, Mang’ola, Matala hadi Mkoa wa Simiyu na baadae Mkoa wa Shinyanga ni barabara ya siku nyingi sana. Mzee wangu asubuhi ameiongelea vizuri. Mheshimiwa Chenge ule muziki uliousema wa kuucheza, wewe ukianza kucheza huko Simiyu na sisi tutaanza kucheza huku Arusha, halafu Mheshimiwa Mbarawa utatuona. Tufanye mambo ambayo tumekubaliana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri Mbarawa barabara ya Oldeani Junction, Matala hadi Simiyu siyo barabara ya Karatu - Mbulu - Haydom kwenda Simiyu, hizi ni barabara mbili tofauti. Barabara hii kwenye vitabu vyenu mmeiita The Southern Serengeti bypass. Southern Serengeti bypass hata siku moja haiwezi kupita Mbulu ni hii ambayo Mzee Chenge asubuhi ameiongelea. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri juzi nikiwa Jimboni nimekutana na vijana wa ofisini kwenu, hii taarifa sijui wameitoa wapi, sasa wakati mnahitimisha mtuambie hili badiliko la kwamba barabara sasa ni kama inataka kutelekezwa, barabara ambayo imetumia mabilioni ya pesa kwenye upembuzi yakinifu, sasa wanaanza upembuzi yakinifu mwingingine utakaotumia mabilioni ya hela mnapitisha Mbulu - Haydom, Huku ni kuchezea hela.(Makofi)

Mmetumia over bilioni tano kwa ajili ya upembuzi yakinifu na hata sasa hivi pamoja na kwamba kazi ile ya upembuzi yakinifu ilikamilika, bado mmeipa hela iendelee kutumika vibaya. Kwa hiyo, barabara ya kuunga Arusha na Simiyu ni Oldeani Junction - Matala - Mwanhuzi - Lalago na kwenda huko kwingine siyo hii ya Mbulu.

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara ya Karatu - Mbulu - Haydom na kwenda Mto Sibiti, Mheshimiwa Waziri Mbarawa ni barabra iliyochelewa nayo pia kujengwa kwa kiwango cha lami. Wale Wabunge wa siku nyingi mlioko kwenye jengo hili mmesikia, tangu enzi ya Marehemu Mzee Patrick Qorro, akaja Mzee Philip Marmo akaja Mheshimiwa Dkt. Wilbrod Slaa na hawa wengine wa majuzi wameendelea kuongea barabara hiyo lakini hadi leo barabara hiyo ni ya vumbi. Viongozi wote tena wengine wameanzia awamu ya akina Kikwete, barabara ya Karatu - Mbulu - Haydom Marehemu Mzee Rashid Kawawa alipokwenda Maghang miaka hiyo ya 1980 alisema barabara hiyo itajengwa kwa kiwango cha lami, hadi leo ni barabara ambayo kupitika kwake wakati wa mvua ni shida kubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hivyo nakushauri Mheshimiwa Mbarawa, haya mambo nadhani mengine mnayapata mkiwa ofisini, hebu mje field, sijakuona ukija Kanda ile na Naibu wako pia sijamuona, hebu mtembee ili muone jiografia ili muweze kujua hiki ambacho tunakiongea. Naomba barabara hizo mbili mzitambue ni barabara mbili tofauti na zote zina umuhimu wa tofauti. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niseme kuhusu suala la kupandisha hadhi barabara. Mheshimiwa Waziri tunaomba barabara zipande hadhi ili zipunguze mzigo kwenye Halmashauri zetu. Fedha zinazokuja kwenye Halmashauri kwa ajili ya matengenezo ya barabara ni fedha kidogo sana.

Mwaka jana Karatu tulipitishiwa shilingi bilioni 1.5, lakini hadi sasa tunavyoongea tumeletewa shilingi milioni 300, thirty percent na tuna mtandao wa barabara unaozidi kilometa 500, hivi utafanya nini kwa shilingi milioni 300? Kwa hiyo, tunaomba zipande juu ili huu mzigo utoke kwetu uende huko kwako ambako kuna fedha nyingi, huko ambako unapata asilimia kubwa ya fedha.

Kwa hiyo, tunaomba hizi barabara zipande hadhi ili mtusaidie ndugu zetu kubeba mzigo huu, siamini sana kama hoja ya kuanzisha Wakala ndiyo itakuwa suluhisho la kumaliza tatizo hili, tuleteeni fedha, Halmashauri zetu zina uwezo na wataalamu wa kutosha wa kufanya kazi ya barabara. Jambo hili leo mkilitoa pale Halmashauri, wale wataalamu tulionao watakuwa redundant. Kwa hiyo, nadhani suala hili tuleteeni hela sisi tuwasaidie kufanya hizo kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nilisema kidogo kuhusu Reli ya TAZARA, miaka ya 1970 nchi hii ilipata neema ya kupata reli ya kisasa kwa wakati ule. Ilikuwa reli pekee katika Ukanda huu wa Kusini iliyojengwa kwa usasa wa kiasi kile, yaliyoendelea TAZARA tunayafahamu, yanayoendelea TAZARA tunayafahamu. leo kama Nchi tumejitwisha kubeba kujenga reli nyingine ya standard gauge hii inayopita katikati ya nchi. Naomba hayo yaliyotokea kwenye reli ya TAZARA yawe ni somo na darasa kwa ajili ya uendeshaji wetu kwenye reli hii ya kati tunayokwenda kujenga. Tusipoangalia miaka 40 mingine inayokuja tutaimba muziki huu huu ambao leo tunauimba kwenye reli ya TAZARA.

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi ni Mjumbe wa Kamati ya Miundombinu, naamini nchi hii bado inaihitaji reli ya TAZARA, tena inaihitaji reli ya TAZARA sana. Reli ya TAZARA kwa sasa kinachohitajika ni uwekezaji na kupata viongozi wenye weledi basi reli ile inaweza ikajiendesha. Machimbo ya makaa ya mawe yaliyopo pale Songwe yanatosha kabisa kuendesha reli hii. Kwa hiyo, Serikali ikubali kuwekeza fedha kidogo ili reli hii iweze kujiendesha. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niongelee kidogo tena kuhusu reli ya kati….

MHE. QAMBALO W. QULWI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru.