Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano

Hon. Selemani Moshi Kakoso

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mpanda Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano

MHE. MOSHI S. KAKOSO: Mheshimiwa Naibu Spika, nishukuru sana kwa kunipa nafasi hii na mimi niwe sehemu ya mchangiaji kwenye Wizara hii. Awali ya yote nitoe pongezi kwa Serikali kwa kazi kubwa sana ambayo inafanyika hasa kwenye suala la miundombinu. Wapo watu ambao hawaoni kile ambacho kinafanywa na Serikali, lakini tunaipongeza Serikali kupitia kwa Mheshimiwa Rais, Mheshimiwa Waziri Mkuu na Mheshimiwa Waziri mwenye dhamana.(Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, yapo mambo ambayo yamefanyika na yanaonekana ni mapinduzi makubwa ya haraka. Tuna upanuzi wa uwanja wa ndege wa kimataifa pale Dar es salaam. Kwa wale ambao hawajafika wanaona mabadiliko ambayo yapo, ni kazi ambayo inafanywa na Serikali. Kuna ununuzi wa ndege mpya ambazo zinatengeneza sura mpya na historia ya nchi yetu. Ndani ya kipindi kifupi tumepata ndege ambazo zimeanza kutoa huduma kwa wananchi, lakini baadhi ya watu hawaoni yale ambayo yanafanywa na Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini yapo ambayo yamefanywa makubwa, ni ujenzi wa reli ya kati, tayari Mheshimiwa Rais alishaweka jiwe la msingi ambalo linaashiria kuanza kwa ujenzi ambao utatoa unafuu wa maisha ya Watanzania hasa wale ambao ni maskini wa kipato cha chini. Zipo jitihada ambazo Serikali imefanya kama ujenzi wa barabara ambapo karibu kila kona kuna ujenzi wa barabara. Hizi ni shughuli ambazo zimefanywa na Serikali, tuna haki ya kuipongeza.(Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nianze tu kutoa shukrani za dhati kwa Mkoa wetu wa Katavi japo yupo Mbunge mwenzangu ambaye amesema hakuna lolote lililofanywa, nasikitika sana. Tuna uwaja wa ndege ambao umejengwa, lengo la kujenga uwanja wa ndege pale Mpanda ni kuweza kukuza utalii ukanda wa Magharibi, kwa maana ya Mikoa ya Rukwa, Katavi na Kigoma.

Mheshimiwa Naibu Spika, wanapojenga ule uwanja wanahitaji sasa kui-promote mbuga ya Katavi pamoja Mbuga ya Mahale ambayo ipo Mkoa wa Kigoma; ndiyo malengo makubwa ya Serikali. Kwa taarifa tu, ni juzi juzi Watalii kutoka nchi ya Israel wamefika, wana interest kubwa sana ya kwenda Mkoa wa Katavi na kufanya utalii wa Ziwa Tanganyika. Sasa kwa wale ambao hawana uelewa hawajui. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunaipongeza Serikali kwa kutengeneza miundombinu, tunayo barabara ya kutoka Sumbawanga kuja Mpanda tayari iliishaanza kujengwa. Tunachokiomba Serikalini ni kuimaliza ile barabara japo mwenzangu aliyetangulia amefika na kuponda na anasema
zile fedha zilizotengwa hajui kazi yake kwa sababu barabara imekamilika. Lakini kwa taarifa tu ni kwamba ile barabara inahitaji mifereji na vitu vingine ambayo vinahitajika kukamilika kwa barabara ndio maana asilimia 80 imekamilika lakini bado asilimia 20. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nizungumzie suala la bandari. Bandari ni nguzo kubwa sana ya kiuchumi na ni lango kuu la mapato ya Serikali kwa nchi yetu hasa Bandari ya Dar es Salaam. Tunaishauri Serikali ihakikishe inaandaa matengezo ya haraka kuhakikisha upanuzi wa ile bandari unafanywa kwa wakati. Bandari ile ikikamilika itaruhusu kuletwa kwa meli kubwa ambazo ni za kimataifa ambazo zinashindwa kwa sasa kufika kuweka gati pale Dar es Salaam kwa sababu bado miundombinu haijakamilika. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunaomba sana Serikali ishughulikie ujenzi wa bandari sambamba na bandari zingine, Bandari ya Tanga, Bagamoyo na Mtwara ziweze kujengwa. Vilevile bado zipo bandari muhimu sana za Maziwa makuu. Tuna Bandari ya Mwanza inahitaji iboreshwe, tuna bandari ya Kigoma tunahitaji ifanyiwe maboresho makubwa, tuna bandari ya Karema ambayo Serikali iliazimia kwa nia njema kufungua mawasiliano kati ya nchi ya DRC na nchi yetu ili kuweza kujenga bandari ambayo itafanya shughuli za kibiashara kati ya bandari ya Kalemii na bandari ya Karema. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunaiomba sana Serikali ielekeze nguvu, hii bandari ya Karema imekuwa kila Bunge linalopita inazungumzia ujenzi wa bandari, lakini leo hii tunaiomba sasa Serikali ipeleke nguvu ikamilishe ujenzi wa bandari hii ili iweze kutumika na kuwasaidia wananchi sambamba na ujenzi wa reli ule unaojengwa kutoka Mpanda kwenda Karema. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nizungumzie reli. Reli ni kiungo muhimu sana kwa wananchi, hasa ujenzi wa reli ya kati. Serikali imeazimia na tumeona dhamira kubwa ya Serikali ya kujenga miundombinu ya reli, lakini reli ya kati maana yake ni reli inayotoka Dar es Salaam kwenda Kigoma. Tunaomba sana Serikali ijielekeze kuhakikisha inakamilisha ujenzi kwa uelekeo wa kwenda Kigoma. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na matawi yale ambayo yapo katikati kwa maana tawi la kutoka Tabora kwenda Mwanza, tawi la kutoka Kaliua kwenda Mpanda mpaka Karema na tawi jipya ambalo litajengwa kuanzia Uvinza kwenda Msongati. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ujenzi wa reli hii malengo yake ni kuchukua mzigo wa nchi ya Congo kwa maana tuchukue mzigo wa Congo upande wa Kusini na upande wa Mashariki ni sambamba na uboreshaji wa bandari ya Kigoma ili iweze kutumika vizuri. Tunaomba sana Serikali iangalie route itakayoanza ianzie Tabora kwenda Kigoma, ianzie Kaliua kwenda Mpanda ili kuweza ku-cover kwenye maeneo ambayo kiuchumi ndiyo yana nafasi.

Mheshimiwa Naibu Spika, nizungumzie suala la barabara. Tunaishukuru Serikali, barabara sasa hivi zinaanza kujengwa, kutoka Mpanda kwenda Kigoma ilikuwa ni hadithi kwamba huwezi ukaona basi linalotoka Mkoa wa Kigoma likaenda Mpanda au Mbeya, lakini leo hii barabara zinapitika, tunaomba sasa zifanyiwe maboresho. Serikali imetenga fedha kwa ajili ya ujenzi wa barabara ya kutoka Mpanda kwenda Kigoma kwa kuanzia tuna kilometa 35.

Mheshimiwa Naibu Spika, niiombe sasa Serikali kama ilivyokuwa imeahidi iandae utaratibu wa barabara itakayoanzia Uvinza kuja Mishamo, na hii inayoanza kutoka Mpanda kwenda Mishamo iende sambamba na ujenzi ambao upo kwa sasa. Tukifanya hivi tutakuwa tumesaidia wanachi wa Mikoa hii ya Kanda ya Magharibi.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini bado tuna barabara ya kutoka Mpanda kwenda Tabora, tunaomba sana Serikali ianze haraka ujenzi wa barabara hii. Kukamilika kwa barabara hii kutakuwa kumekamilisha mawasiliano ya Mikoa ya Tabora, Kigoma, Katavi na Rukwa, hii ni Mikoa ambayo kimsingi ilisahaulika sana kwa kipindi kirefu, tunaomba barabara hizi ziwekewe kipaumbele kikubwa kama ahadi ya Mheshimiwa Rais alivyokuwa ameahidi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu suala la mawasiliano, yapo maeneo ambayo mawasiliano nchini bado ni duni hasa Mikoa yetu ya Ukanda wa Magharibi. Nizungumzie suala la Jimbo langu, kuna baadhi ya kata hazina mawasiliano. Tunaomba Serikali ipeleke mawasiliano kwenye kata ya Kabungu, Mpanda Ndogo, kata ya Tongwe ambako kuna makao makuu ya Wilaya ya Tanganyika pamoja baadhi ya maeneo ya Mkoa kama kata ya Ilunde; tunaomba mawasiliano yapelekwe ili wananchi waepuke adha ambayo ipo kwa kupata mawasiliano ambayo ni duni.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini lipo jambo mahsusi ambalo kimsingi kwa Mbunge ambaye anaitakia mema nchi yetu amelizungumzia sana Mheshimiwa Zungu. Suala la kuipa nafasi TTCL iweze kumiliki na ikiwezekana Serikali inunue shares zile za Airtel ili imiliki yenyewe, iendeshe na kulisimamia hili Shirika, litaenda vizuri sana na litatoa tija na faida kubwa kwa nchi yetu; tukitengeneza mazingira haya tutakuwa tumewasaidia sana wananchi wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini mwisho nisisitize kwenye suala la reli Wilaya ya Mpanda na Mkoa wa Katavi kwa ujumla bado kuna wasafiri wengi. Tunamuomba Mkurugenzi mhusika wa Shirika hili aongeze mabehewa ili kuwasaidia wananchi wanaopata shida kubwa sana kwa ajili ya usafiri. Mabehewa yanayohitajika yaende yote, yale ya daraja la tatu, la pili na la kwanza yanahitajika. Kwa hiyo, tunaomba wananchi…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji).

MHE. MOSHI S. KAKOSO: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana, naunga mkono hoja.