Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano

Hon. George Malima Lubeleje

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mpwapwa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano

MHE. GEORGE M. LUBELEJE: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nakushukuru kwa kunipa nafasi ili nichangie Wizara hii. Kwanza nampongeza Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri, Katibu Mkuu, Engineer Mfugale ambaye ni CEO wa TANROADs na vilevile nimpongeze Manager wa TANROAD wa Mkoa wangu kwa kazi nzuri wanazofanya. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, leo nitazungumzia barabara moja tu; na hii barabara ni ya kutoka Mbande - Kongwa kwenda Mpwapwa kujengwa kwa kiwango cha lami. Nimeanza kudai barabara hii tangu mwaka 1984. Nimekuwa Diwani miaka 15; Mwenyekiti wa Halmashauri Wilaya ya Mpwapwa miaka 15, nadai barabara hii. Nimeanza Ubunge mwaka 1990 nikiwa kijana, wakati huo nachana afro; ukienda Ofisi ya Makumbusho Dar es Salaam, utakuta picha yangu pale. Sasa mpaka nafika umri huu, nadai barabara. Sasa umri wangu ni mkubwa, tangu kijana nadai barabara hii, lakini Serikali hawanionei huruma, kwa nini? (Kicheko/Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nimekuwa Mbunge miaka 20; 2010 - 2015, nikaenda likizo miaka mitano; sasa nimerejea tena kwa matumaini kwamba wananchi wa Mpwapwa sasa hii barabara itatengenezwa kwa kiwango cha lami. Kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri nakuomba sana ndugu yangu, kijana wangu, sikiliza kilio cha wananchi wa Mpwapwa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, Mpwapwa ni Wilaya ya zamani, tangu mwaka 1905. Sasa umri wake ni miaka 100. Kwa hiyo, Mpwapwa ina sifa zote za kupata barabara ya lami. Ni kilomita 50 zimebaki; Mbande - Kongwa Junction; Kongwa Junction mpaka Kongwa, kilomita tano mmeshajenga tayari, bado kilomita 50. Mbande junction ya Kongwa na junction Kongwa kwenda Mpwapwa kilomita
46. Namwomba sana Mheshimiwa Waziri, Eng. Mfugale unanisikia, wewe ndio CEO wa TANROADs, mnisaidie ndugu zangu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, Mpwapwa kuna uchumi. Hii barabara ndiyo inayounganisha Majimbo matatu; Jimbo la Mheshimiwa Simbachawene, Waziri wa TAMISEMI. Mheshimiwa Spika, Mbunge wa Jimbo la Kongwa na Mheshimiwa Lubeleje, Mbunge wa Mpwapwa. Hii barabara ina umuhimu kwa uchumi na maendeleo ya Wilaya ya Mpwapwa. Hii barabara Mheshimiwa Waziri inapitisha magari zaidi ya 150 kutoka Mbande kwenda Mpwapwa; magari makubwa ya mizigo pamoja na magari madogo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, namwomba sana ndugu yangu, leo nilitamani nilie, lakini namsamehe kwa leo, maana mtu mzima kulia siyo jambo jema. Leo itakuwa ni mara yangu ya mwisho kuomba barabara. Nitakuwa nakaa kimya tu naisikiliza Serikali yangu. (Kicheko/Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, Mpwapwa kuna taasisi zaidi ya nane; kuna taasisi ya utafiti wa Mifugo ya Kitaifa, kuna Chuo cha Mifugo Mpwapwa, Chuo cha Maafisa wa Afya na Chuo cha Ualimu Mpwapwa. Mpwapwa pia kuna mabonde mazuri sana ya kilimo; Bonde la Malolo, Lumuma, Matomondo na Bonde la Chamkoroma. Mpwapwa vile vile ina madini aina ya ruby katika Kijiji cha Uinza. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, namwomba sana Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri, Katibu Mkuu, CEO Mfugale, mnisikilize kilio changu. Wananchi wa Mpwapwa wananipenda na ndiyo maana wananirejesha Bungeni. Sasa nitakuja kuwaachia kumbukumbu gani jamani ndugu zangu?
Wamenirejesha kwa matumaini kwamba safari hii Serikali yangu sikivu itasikia kilio changu, watapata barabara ya lami. Kwa hiyo, nawaomba sana ndugu zangu, viongozi wakubwa watatu; Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Waziri wa TAMISEMI; hivi Mheshimiwa Waziri huwezi kuwaonea huruma hata wakubwa wenzako hawa kweli! (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa nimesema nazungumzia hii barabara, Mheshimiwa Waziri amenisikia kilio changu, Serikali yangu ni sikivu, najua wananchi wa Mpwapwa wananisikiliza na safari hii kwa kweli nina matumaini makubwa kabisa kwa baraka za Mwenyezi Mungu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana, namshukuru sana Waziri wa Ujenzi, Naibu Waziri na CEO Engineer Mfugale, Katibu Mkuu na Viongozi wote wa Wizara hii kwa kazi nzuri. Ahsanteni sana. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja hii kwa asilimia mia moja.