Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mpango wa Pili wa Maendeleo wa Taifa kwa kipindi cha Miaka Mitano kuanzia mwaka 2016/2017 – 2020/2021

Hon. Dr. Mwigulu Lameck Nchemba Madelu

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Iramba Magharibi

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Mpango wa Pili wa Maendeleo wa Taifa kwa kipindi cha Miaka Mitano kuanzia mwaka 2016/2017 – 2020/2021

WAZIRI WA KILIMO, MIFUNGO NA UVUVI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nakushukuru kwa kunipa fursa hii ya kuchangia katika Mpango wa Maendeleo ambao umewekwa mbele yetu.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza niseme tu kwamba sisi kama Wizara tumepokea michango na maoni ya Waheshimiwa Wabunge kuhusu Mpango, na tumepokea maoni na mawazo ya Waheshimiwa Wabunge yanayolenga katika Wizara yetu, yote tumeyapokea na tutayafanyia kazi.
Mheshimiwa Naibu Spika, leo hii huenda nisijibu yote kwa ajili ya muda, lakini niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge mambo mawili kwamba la kwanza tumepokea maoni yao, na pili tutaendelea kujibu kwa sababu bado tutakuwa na fursa ya kufanya hivyo katika majibu ya bajeti za kisekta ambapo Waheshimiwa Wabunge watachangia tena katika bajeti ya Wizara.
Mheshimiwa Naibu Spika, tumepokea wachangiaji wote ambao waliigusa katika Wizara ya Kilimo, lakini pia walipogusa katika Mpango kwa ujumla. Niseme tu kwamba Mpango wa Maendeleo ambao umewekwa mbele yetu umeipa nafasi kubwa sekta ya kilimo, na umeipa nafasi kubwa pale ulipoongelea kwamba mpango unalenga kunufaisha viwanda na kuinua viwanda hasa vinavyotokana na mazao ya kilimo.
Jambo la pili Mpango huu umeipa fursa kubwa sekta ya kilimo, kilimo kwa dhana pana, kwa maana ya kilimo, mifugo na uvuvi pale ulipoongelea kwamba unapanga kuhuianisha maendeleo ya viwanda pamoja na maisha ama maendeleo ya watu. Ikumbukwe kwamba katika nchi yetu kilimo kinaajiri asilimia kubwa ya Watanzania.
Mheshimiwa Naibu Spika, hivyo hata katika maeneo ambayo Mpango huu umeongelea neno kilimo ni kwa maana pana ambapo unaongelea mazao, unaongelea mifugo na unaongelea uvuvi.
Nikienda katika eneo moja moja, machache, Mheshimiwa Ally Saleh alisema kwamba ianzishwe na Benki ya Uvuvi. Katika Benki ya Kilimo inatamkwa kilimo lakini ni kwa dhana pana ambapo uendelezaji wa mazao ya kilimo, kwa maana ya mazao yanayotokana na kilimo mikopo yake inapatikana katika Benki ya Kilimo, lakini pia kwa wale ambao wanaendeleza mazao ya mifugo na wenyewe wanapata fursa hiyo sawa na upande wa mazao, lakini vivyo hivyo kwa upande wa uvuvi. Jambo hili tulilisemea hata tulipokuwa tunajibu swali la jana ambalo lilikuwa linahusisha mambo ya ruzuku.
Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Yahaya Massare aliongelea kuhusu malisho pamoja na Waheshimiwa wengine ambao waliongelea kuhusu malisho ya Mifugo akiwemo ndugu yangu wa Jimbo la Kilindi na ndugu yangu Mheshimiwa Ulega, pamoja na ndugu yangu Mheshimiwa Kakunda na wengine wote ambao waliongelea kuhusu malisho. Jambo hili la malisho kwa mifugo siyo jambo la siku moja, sisi kama Serikali tunaendelea kulifanyia kazi kwa sababu linahusisha Wizara zaidi ya moja.
Mheshimiwa Naibu Spika, ninampongeza Mheshimiwa Lukuvi ambaye tumekuwa tukishirikiana naye mara kwa mara yanapotokea matatizo ya migogoro yanayohusisha matumizi ya bora ya ardhi. Waheshimiwa Wabunge, jambo la matumizi bora ya ardhi halianzii kwenye ngazi ya Wizara bali linaanzia katika Kamati zetu za matumizi bora ya ardhi ambazo ziko katika ngazi ya vijiji. Wabunge kama wawakilishi tushiriki katika kutoa maoni na katika kutenga maeneo katika matumizi bora ya ardhi pale Kamati zetu zinazotenga matumizi bora ya ardhi zinapokutana. Mimi kama Waziri ni dhahiri kwamba naunga mkono jitihada za Kamati zetu zinapokuwa zinakutana kwa ajili ya kutenga maeneo kwa ajili ya matumizi bora ya ardhi.
Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine ambalo liliongelewa na Waheshimiwa Wabunge wengi lilikuwa jambo linalohusu makato katika mazao. Jambo hili pia kwa sababu linahusisha Wizara zaidi ya moja tumeendelea kuyafanyia kazi na tunaamini tunavyoenda katika Bunge hili la Bajeti ambapo mwishoni kabisa tutatengeneza Finance Bill, tunategemea yale ambayo yanahusisha tozo ama makato ambayo yanaangukia katika sheria zinazopita katika Bunge letu tutapata fursa ya kuyangalia, lakini Wizara ya Kilimo pamoja na TAMISEMI pamoja na Wizara ya Fedha tumeendelea kuyafanyia kazi haya kwa sababu tayari uamuzi wa Serikali ulishatoka kuhakikisha kwamba tunawatengenezea mazingira bora wakulima, wafugaji na wavuvi ili waweze kufanya kazi zao na kuweza kujiletea tija.
Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine ambalo tunalifanyia kazi, Waheshimiwa Wabunge ambao wengi wenu mmeliongelea ni kuhusu pembejeo. Jambo la pembejeo linalohusisha ruzuku, Serikali tunaendelea kulifanyia kazi kuangalia utaratibu mzuri ambao utakuwa endelevu na ambao hautaruhusu mianya ya matumizi mabaya ya fedha za umma ambayo yanatokana na baadhi ya mifumo ambayo tumekuwa tukiitumia ya ugawaji wa ruzuku. Kwa hiyo, katika jambo hili, kwanza tunaangalia utaratibu ambao utakuwa endelevu, lakini vilevile tunaangalia utaratibu ambao utagusa watu waliowengi wanaohusika katika sekta hiyo.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika hili tuliangalia uwezekano wa kuangalia kwanza fedha ambazo zinapatika katika kila sekta, tuliangalia hata katika mazoa utaona makato mengi yaliyokuwa yanalalamikiwa ni makato ambayo hayaendi kuendeleza sekta husika, tunaangalia uwezekano wa makato hayo yaweze kunufaisha sekta na ambayo hayanufaishi sekta yasiwekwe kwenya sekta hiyo.
Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja asilimia100 kwa 100, na niendelee kusema kwamba kama mnataka mali mtazipata shambani!
Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante!