Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira

Hon. Luhaga Joelson Mpina

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kisesa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira

NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS (MUUNGANO NA MAZINGIRA): Mheshimiwa Mwenyekiti, muda wangu ni mfupi na naomba nianze kama ifuatavyo:
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza niwashukuru sana wananchi wangu wa Jimbo la Kisesa kwa kuendelea kuniamini na baadhi yao mko hapa kuja kushuhudia. Niendelee kuwaambia tu kwamba, kama ni Mbunge mlikwishapata na nitaendelea kuwawakilisha kikamilifu hapa Bungeni na maeneo mengine. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nianze kujibu hoja kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, moja; kuna suala lililoelezwa na Kamati hapa kuhusu suala la Kamati ya Katiba na Sheria imetupongeza sana kwa hatua tulizozichukua katika suala la upungufu la Jengo la Luthuli Two katika Ofisi ya Makamu wa Rais na hatua tulizozichukua. Sasa hivi nataka niwahakikishie kwamba hatua tunaendelea kuzichukua, moja ni hayo marekebisho ambayo sasa hivi yanafanyika. Pili, baada ya marekebisho hayo kukamilika ambayo yanafanywa kwa sasa hivi tutam-engage PPRA ili aweze kufanya ile value for money ili kuhakikisha kwamba, fedha za Watanzania zilizotumika zimetumika sawasawa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hapa zimekuja hoja za Kiongozi au Msemaji wa Kambi ya Upinzani wakati anawasilisha, alizungumza sana suala la Muungano na kuonesha kwamba, Muungano huu wakati mwingine labda anaona yeye kwamba, hauna faida.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna faida kubwa sana za Muungano na Tanzania tunatakiwa kujivunia sana Muungano huu. Moja, tuna Kifungu kile cha GBS ambayo kila mwaka tunatoa zaidi kati ya bilioni 20 mpaka bilioni 50 kwa ajili ya GBS, pia pay as you earn haikuwepo, leo tunatoa pay as you earn ya bilioni 1.75 kila mwezi na kwa mwaka tunatoa bilioni 21 za pay as you earn(PAYE) na hazina utata wowote katika kutoa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna dividend ya BOT ambayo nayo inatolewa kati ya bilioni mbili mpaka bilioni nane kila mwaka na haina utata katika kutolewa. BOT bado inazikopesha hizi Serikali mbili, Serikali ya Muungano na Serikali ya Mapinduzi Zanzibar kwa ajili ya kuziba pengo la mapato na matumizi. Kwa mfano, Zanzibar katika mwaka huu wa fedha ilikuwa na kiwango ambacho kinafikia mpaka bilioni 45.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Msemaji wa Kambi ya Upinzani alisema hapa kwamba, Muungano huu umeshindwa kuchochea maendeleo na umeshindwa kuchochea mabenki kwenda Zanzibar. Tumeshuhudia wote mwaka 1990 benki Zanzibar zilikuwa mbili tu, lakini sasa benki Zanzibar zimefikia 12. Tafiti nyingi zinafanywa, anasema kwamba, hakuna uchocheaji wa maendeleo, Benki Kuu tu yenyewe imeshafanya tafiti zaidi ya 13 Zanzibar na tafiti hizi ni kwa ajili ya maendeleo na kwa ajili ya uchumi na zimekuwa zikiwa incorporated katika maendeleo ya Zanzibar.
Mheshimiwa Mwenyekiti, amesema pia makampuni mengi hayaendi Zanzibar, tukitolea mfano Makampuni haya ya Simu, hakuna Kampuni ya Simu ambayo ipo Bara hapa haipo Zanzibar. tiGO, Voda, Zain, wote wameanzisha branch kule.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunayo hii Mamlaka ya Uvuvi wa Bahari Kuu. Uvuvi wa Bahari Kuu ambao unatoa faida kubwa tu, mpaka sasa hivi toka uanzishwe tunatoa zaidi ya billion nne. Mfuko wa Jimbo kila mwaka, fedha hizi hazina utata, Mheshimiwa Ngwali alikuwa anasema zina utata, hazina utata wowote, tunapeleka 1.24 billion kila mwaka na hazina utata wowote. TASAF toka tuanze tumepeleka shilingi bilioni 31.5 na miradi mikubwa imefanyika ya ujenzi wa barabara na miundombinu mikubwa ya kiuchumi bilioni 31. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, MIVARF tumepeleka zaidi ya bilioni 13.49 na miradi mikubwa imefanyika Zanzibar, barabara zaidi ya kilometa 83. Tumejenga masoko ya kisasa ambayo mpaka yana cold room Unguja na Pemba, yamejengwa zaidi ya bilioni 13.49 zote zimekwenda, halafu mtu anasema kwamba, haoni shughuli ambayo imefanyika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, COSTECH; tumefanya miradi mikubwa ya COSTECH, miradi mikubwa ya utafiti imefanyika zaidi ya shilingi bilioni tatu zimekwenda katika shughuli hii na tafiti zinafanyika na Zanzibar wananufaika sana na tafiti zinazofanywa na COSTECH katika uzalishaji wa mpunga, uzalishaji wa muhogo na maeneo mengine. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, yapo makampuni yetu yanafanya vizuri sana. Nani asiyejua kwamba, Bodi ya Mikopo inatoa mikopo bila kubagua watu wa kutoka pande zote mbili za Muungano? Nani asiyejua kwamba leo TRA inakusanya kodi pande zote za Muungano tena kwa usahihi na kwa ufanisi mkubwa na pande mbili zote zinanufaika. Taasisi za Muungano 39 tulizonazo, taasisi 30 zote zina ofisi Zanzibar, isipokuwa Taasisi tisa tu ambazo na zenyewe tayari tumeshatoa maelekezo lazima ziwe na ofisi Zanzibar. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, limeongelewa suala kwamba Taasisi hizi za Muungano hazishirikiani, ushirikiano ni mkubwa. Mmeona ushirikiano uliozungumzwa hata na Mheshimiwa Waziri wa Nishati na Madini kuhusu mapato ya ZESCO na TANESCO. Pia Wizara ya Nishati na Madini kubeba mzigo wa asilimia 31 kwa ajili ya kupunguza gharama zinazolipwa Zanzibar yote hayo unasema kwamba Muungano huu hauna manufaa! Tendeeni haki Muungano, mengi yamefanyika, tutaendelea kuyaboresha na sisi tuko hapa, tunatembea kila siku kwenda Zanzibar, kwenda Unguja na kwenda Pemba.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ukienda Pemba hata ukimuuliza tu mtoto mdogo, ukiuliza Mpina, wewe sema Mpina tu, yeye atasema Naibu Waziri Muungano atamalizia. Tunafanya kazi, endeleeni sasa kutuunga mkono, ili tuweze kufanya kazi vizuri zaidi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tumefanya mambo makubwa katika upande wa mazingira. Nani asiyejua hali ya mazingira ilivyokuwa Novemba mwaka 2015, Serikali ya Awamu ya Tano inapoingia madarakani? Nani asiyejua takataka zilivyokuwa zikizagaa kila mahali? Nani asiyejua majitaka yalivyokuwa yakitiririka kila mahali na kuleta athari kubwa kwa wananchi? Nani asiyejua migodi na viwanda vilivyokuwa vikichafua mazingira? Nani asiyejua? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tumefanya mabadiliko makubwa, leo utashuhudia na kuona jinsi maboresho tulivyofanya. Wakati tunaingia mwaka 2016 wagonjwa wa kipindupindu mwaka 2016 walikuwa 11,000 na watu waliofariki mwaka huo walikuwa 163. Leo mwaka 2017 kwa
jitihada tulizozifanya ofisi hii pamoja na Wizara ya Afya wagonjwa wa kipindupindu mwaka huu walikuwa 1,146 tu waliofariki 19. Kwa hiyo, utaona jinsi ambavyo tunafanya. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, hapa wanatokea baadhi ya Wabunge wanataka kuwabeba wahalifu, watu wanaopigwa faini, watu tunaowatoza, lazima mjue kuna suala la utiririshaji wa majitaka kwenye viwanda, nenda kaangalie, wagonjwa wa saratani walivyoongezeka sasa hivi. Mwaka 2006 wagonjwa wa saratani walikuwa 2,416, kila mwaka wamekuwa wakiongezeka wagonjwa wa saratani. Sasa hivi tuna wagonjwa wa saratani toka 2,416 hadi wagonjwa wa saratani 47,415. Kwa hiyo, huwezi ukakinga kifua kwa wahalifu hawa. Wahalifu hao waambiwe kufuata na kuzingatia sheria.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tulivyoingia kwenye ofisi ile tumeongeza kasi ya ukaguzi wa mazingira kuhakikisha kwamba hakuna mtu anachafua mazingira, hakuna mtu anaharibu mazingira. Wakati tunaingia uwezo wa kukagua mazingira kufikia taasisi 425, leo tumefikia taasisi 1,548 hadi kufikia hii Juni.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tumefanya mapinduzi makubwa katika ukusanyaji wa mapato, mapato NEMC sasa yamepanda. Tulikuta wana uwezo wa kukusanya mapato ya bilioni tano, katika muda mfupi tuliokaa tumeweza kuchochea ukusanyaji wa mapato NEMC hadi wamefikia bilioni 12, ongezeko la bilioni saba. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, watu wengine wanakaa hapa wanasema ooh! hili Baraza la Mawaziri halina Mawaziri wa kumshauri Mheshimiwa Rais. Hivi mnataka Mawaziri wa aina gani wa kumshauri Mheshimiwa Rais? Tunayafanya haya tulitakiwa kupongezwa tu. Tumefanya transformation hizi kuhakikisha kwamba, maendeleo yanaweza kupatikana. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tumefanya operations nyingi mbalimbali na tozo nyingi na faini mbalimbali watu wameweza kutozwa kwa ajili ya kuhakikisha tunarejesha mazingira yetu, tutaendelea kufanya hivyo. Ukitaka uepukane na utozwaji wa faini wewe zingatia sheria hakuna mtu ambaye atakugusa, Mpina hutamuona wala NEMC hutawaona. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tumefanya mapinduzi makubwa ya kuleta usafi katika nchi hii. Leo Dar-es-Salaam (DAWASCO) mifumo yao mibovu ilikuwa ikitiririsha taka kila leo, miundombinu imeimarika na leo taka hizo hazitiririshwi tena kwa kiwango kile kilichokuwa kinatiririshwa. Tulikwenda Kahama, tukawakuta wanatiririsha majitaka tena mbugani na kuharibu vyanzo vya maji, leo nenda, wana mfumo mzuri wa ku-contain majitaka hayo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, SBL, Mbunge wa Temeke atanishuhudia, SBL walivyokuwa wanatiririsha majitaka. Tumedhibiti tatizo hilo halipo tena, wananchi hawapati shida tena. Wananchi wa Keko waliokuwa wanakumbwa na mafuriko, leo hayapo tena, tumetatua tumemaliza. Mgodi wa Dhahabu wa North Mara walivyokuwa wakitiririsha maji yenye kemikali, tumepiga marufuku na hali ni nzuri sana. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tumefanya mapinduzi makubwa sana, watu walikuwa wanashuhudia uchafuzi wa mazingira barabarani, mabasi yanatupa taka ovyo, leo tumeweka utaratibu mzuri, mnaona tangazo hilo la SUMATRA ambalo linamtaka kila abiria kuhakikisha kwamba anatunza mazingira, hakuna utupaji taka ovyo. Kwa hiyo, ukiona mazingira yako safi barabarani sasa hivi ujue Vyombo vya Serikali ya Awamu ya Tano viko kazini. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, uchafuzi uliokuwa unafanywa na meli za mafuta na za mizigo katika bahari yetu, leo tumeweka mfumo mzuri wa uchukuaji taka, uzoaji taka na wa utupaji taka ambao unafanywa majini. Tumeweka mfumo mzuri ambao sasa hatuwezi tena kurejea kwenye uchafuzi huo uliokuwa unafanyika. Operesheni za mara kwa mara zinafanyika na hivyo hakuna uchafuzi tena uliokuwa ukiendelea.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kutokana na uimara huu na kazi hii kubwa ambayo tumeifanya tumeweza kuaminiwa. Leo hii wawekezaji na wafadhili wengi ambao wanaidhinisha fedha zao kwa ajili ya kuisaidia Tanzania katika kutengeneza miundombinu ya uondoshaji wa taka na utunzaji wa maji taka wengi wamejitokeza. Hapa ninavyozungumza katika mwaka huu wa fedha kwa mara ya kwanza eneo la majitaka lilikuwa halipewi fedha. Leo kwa DAWASA tu peke yake wafadhili wengi wamejitokeza na tunategemea zaidi ya shilingi bilioni 800 kutoka kwenye taasisi tu moja ya DAWASA. Sasa mtu akisimama hapa na mbwembwe kusema kwamba eti Serikali ya Awamu ya Tano haiaminiki kwa wafadhali, wafadhili gani unaowa-refer wewe kama majitaka tu peke yake mfadhili tu kwa DAWASA peke yake ni zaidi ya shilingi bilioni 800? Tumeaminiwa na miradi inaendelea kujengwa katika majiji na miji kwa ajili ya kuboresha hali ya usafi wa mazingira katika maeneo yetu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Ali King alikuwa anazungumza kuhusu ahadi yangu niliyoitoa nilipokuwa Zanzibar ya kufanya tathmini katika eneo lililodidimia. Nataka nimwambie asome randama nimeshaweka, lile eneo tumekubaliana Wizarani tutalifanyia tathmini katika mwaka huu ujao wa fedha wa 2017/2018.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Kambi ya Upinzani ilitushauri kwamba tufanye audit eneo la Bagamoyo, Pangani, Rufiji na Zanzibar ile miradi ya mabadiliko ya tabianchi. Wakati tunaagizwa bajeti ya mwaka 2016/2017 sehemu kubwa ya miradi hii ilikuwa haijaanza, sisi tulienda kukagua miradi hii yote ilikuwa …
(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS (MUUNGANO NA MAZINGIRA): Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Kwa kifupi niseme kwamba sasa hivi ndiyo tunaipia miradi hii. Mradi mmoja tu ndio umefikiwa kuhakikiwa ni mradi wa Rufiji, tumeukagua na tumeugundua una kasoro na tumemwagiza Mkaguzi wa Ndani kufanya ukaguzi huo. Mkaguzi wa Ndani atakapotuletea taarifa tutawasilisha kwenye Kamati kuona status ya mradi huo ilivyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru sana na naunga mkono hoja na kwamba Serikali ya Awamu ya Tano tuko kazini, tuungwe mkono tufanye kazi ili tuonyeshe uwezo na tuibadilishe Tanzania yetu. Ahsante sana.