Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira

Hon. Angellah Jasmine Mbelwa Kairuki

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Nominated

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, UTUMISHI NA UTAWALA BORA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Nianze kwa kuunga mkono hoja hii iliyowasilishwa na Mheshimiwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais. Nampongeza kwa hotuba yake nzuri ambayo kwa kweli imeeleza masuala mengi kwa kina na mafanikio mbalimbali ambayo wameyapata katika Ofisi ya Makamu wa Rais.
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda nitoe ufafanuzi au maelezo katika hoja ya ajira katika Taasisi za Muungano pamoja na mgawo au utaratibu wa mgawo wa nafasi hizo za ajira katika Taasisi za Muungano. Iko hoja iliyotolewa hapa kwamba, suala hili halijarasimishwa, suala hili haliko kisheria, suala hili watendaji wanaweza wakaharibu wasieleze ukweli katika mgawo huu na mambo mengine. Napenda tu kusema mambo yafuatayo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa utaratibu huu haukuwepo huko nyuma. Ni jitihada katika kuondoa changamoto katika Muungano ikaonekana kuwe na utaratibu mahsusi kabisa kwa ajili ya mgawo wa nafasi za ajira katika taasisi za Muungano. Utaratibu huu pia ni wa muda katika kuhangaikia suluhisho la kudumu ambalo litasaidia kuweka nafasi hizi na utaratibu huu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika nafasi za vyombo vya ulinzi na usalama haziko katika mgawo huu wa asilimia 21 Zanzibar na asilimia 79 katika SMT. Ukiangalia katika mwaka 2013/2014 na 2014/2015, katika nafasi zilizotolewa katika Wizara ya Mambo ya Nje asilimia 25 zilichukuliwa na SMZ na asilimia 75 ndiyo zilichukuliwa na SMT. Kwa hiyo, hata hapo utaweza kuona pia, hata ule mgawo wa asilimia 21 ulizidi mpaka asilimia 25.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia ukienda katika Taasisi za NIDA, ukienda katika Ofisi ya Makamu wa Rais yenyewe, Zanzibar walipata mgawo katika ajira za 2013/2014 asilimia
33. Imezidi hata ile asilimia 21 ambayo ilikuwa imewekwa katika utaratibu wa mgawo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia katika Taasisi nyingine nia ni njema. Nyingine ajira zake zilifanyika kabla ya waraka huu haujatungwa mwaka 2013/2014, lakini bado kama Serikali pande zote mbili tumekuwa tukilifanyia kazi pamoja na Waziri wa Utumishi kutoka SMZ, SMT na Ofisi ya Makamu wa Rais, tumekuwa tukiliangalia suala hili kwa kina na Mheshimiwa Makamu wa Rais amekuwa pia akilifuatilia sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, changamoto kubwa inayokuja katika maombi ya ajira, kwanza wengine unakuta hawajitokezi, hawaziombi. Pili, lazima tuangalie pia na sifa. Huwezi tu pia ukagawa nafasi bila kuangalia sifa na vigezo. Tumekuwa tukiendelea kuhamasisha Wazanzibari waendelee kujitokeza pamoja na Bara ili kuhakikisha kwamba asilimia 79 na asilimia 21 inaweza kufikiwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, siyo hilo tu, changamoto nyingine ambayo tunaipata katika kupata taarifa sahihi, unakuta wapo wanaotoka upande wa Zanzibar wamekuwa pia wakiomba nafasi, lakini unakuta wengine wamekuwa wakitumia anuani za kutoka Tanzania Bara. Kwa hiyo, unajikuta kuweza ku-compute namba kamili imekuwa kidogo ni changamoto.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo, ziko taasisi mbalimbali za kiuhasibu, nafasi nyingine katika sekta ya elimu, nafasi nyingine katika sekta ya afya, ambazo hata siyo taasisi za Muungano, Wazanzibari wamekuwa wakipata fursa na wamekuwa wakiomba, hawakatazwi. Fursa iko wazi kwa sababu, wote ni Watanzania.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kama Serikali tunaendelea kufanya jitihada kupitia Sekretarieti ya Ajira katika Utumishi wa Umma. Tumeshafungua ofisi eneo la Shangani kwa ajili ya kuhakikisha kwamba wanaratibu ajira zote za Taasisi za Muungano pamoja na kurahisisha na kuendesha majukumu yake wakiwa Mjini Zanzibar ili kurahisisha zaidi kwa waombaji kutoka Zanzibar.
Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile tumekuwa tukiendelea kutangaza nafasi za ajira pia kwa kutumia Vyombo vya Habari vikiwemo vya Zanzibar ili kuwahamasisha Wazanzibari kuhakikisha kwamba nafasi zinazotangazwa waweze kuomba. Nia ni njema na tutaendelea kufanya hivyo kila mara inapobidi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuwasilisha.