Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira

Hon. Daimu Iddi Mpakate

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tunduru Kusini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira

MHE. DAIMU I. MPAKATE: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kuchukua nafasi hii kuchangia hoja katika hotuba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais, Mazingira, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kuchangia katika eneo la environmental assessment katika miradi mbalimbali ya uwekezaji wa viwanda na hasa vituo vya mafuta ya petrol (petrol stations). Kuna tatizo kubwa sana juu ya upatikanaji wa vyeti vya mazingira katika miradi mbalimbali ya uwekezaji kutokana na mlolongo mrefu unaotokana na upungufu mkubwa wa wataalam wa mazingira katika halmashauri zetu za wilaya.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mlolongo mrefu wa masharti ya kutimiza katika kuandaa andiko la mazingira kwenye mradi unaofanywa hutengeneza mazingira ya rushwa kubwa kwa wafanyakazi wa Idara ya Mazingira ili vyeti vya mazingira vipatikane.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tozo nyingi na faini kubwa zinazotolewa bila kufuata sheria za mazingira, wakati mwingine vitisho vingi na vikubwa vinavyotolewa na watumishi/wanaohusika na mazingira katika kuhalalisha rushwa inayoambatana na gharama kubwa ya kulipia ili kupata certificate.
Mheshimiwa Mwenyekiti, bureaucracy katika kupatikana kwa vyeti vya mazingira inayochukua muda mrefu, jambo ambalo linakatisha tamaa wawekezaji na hatimaye kuacha kabisa kuwekeza katika sekta mbalimbali.
Mheshimiwa Mwenyekiti, utaratibu ufanyike kila halmashauri kuwa na wataalam wa mazingira ili kurahisisha tathmini za mazingira kwenye halmashauri zetu. Ni vyema kuwa na kiwango cha mradi kinachotakiwa kusainiwa na Waziri ili kuruhusu vyeti vingine viweze kutolewa katika ofisi za mikoa badala ya kutegemea kila cheti kusainiwa na Waziri husika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, elimu itolewe kwa wadau mbalimbali wa mazingira kabla ya kuwapa adhabu/faini ili kutoa fursa kwa wadau kutekeleza miradi yao kwa mujibu wa mahitaji ya masharti ya mazingira.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kutoa masharti ya jumla ya mazingira katika kuanzisha miradi ya uwekezaji hasa petrol stations katika ofisi ya halmashauri, ili kuondoa usumbufu kwa wadau wa mazingira pindi wanapoanzisha miradi ya uwekezaji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, gharama/faini za mazingira ziangaliwe upya ili kurahisisha wadau wengi wa mazingira kuweza kuzilipa bila kikwazo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, uharibifu wa mazingira katika maeneo mbalimbali umekuwa ni wa kutisha sana, hivyo ni vyema kuimarisha Kitengo cha Mazingira katika Halmashauri mbalimbali za Wilaya.
Mheshimiwa Mwenyekiti, semina mbalimbali zitolewe mpaka vijijini ambapo uharibifu wa mazingira umekuwa mkubwa kutokana na shughuli za uchumi kama ufugaji, kilimo na uwindaji. Semina hizi zitasaidia wananchi kuona umuhimu wa kuhifadhi mazingira ili kuzuia tabianchi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mabaraza ya Mazingira yaimarishwe katika kata ili kuepusha na kusimamia vyema uharibifu wa mazingira usiendelee.
Mheshimiwa Mwenyekiti, biashara ya magogo imekuwa ni chanzo kikubwa cha uharibifu wa mazingira kwa kushirikiana na TFS, biashara hii ipigwe marufuku kwa kuwa inaathiri sana mazingira.