Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira

Hon. Oran Manase Njeza

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbeya Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira

MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kumpongeza Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais kwa hotuba nzuri aliyowasilisha Bungeni kwa Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018. Napenda pia kutoa pongezi kwa Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia napenda kutoa pongezi kwa Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Pia napenda kutoa pongezi kwa Mheshimiwa Kassim Majaliwa Majaliwa, Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kazi nzuri sana ya utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya 2015 - 2020.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara hii ni muhimu sana kwa uhai wa Muungano wetu na wamefanya kazi kubwa sana ya kuondoa kero za Muungano. Kwa kiasi kikubwa Muungano wetu umetuletea sifa nyingi kutoka kila pande za dunia; changamoto kubwa tuliyonayo ni uharibifu wa mazingira na tabianchi. Katika maeneo mengi kuna uharibifu mkubwa sana wa mazingira unaotokana na shughuli za kibinadamu. Uharibifu huo unasababisha changamoto za tabianchi ikiwemo upungufu wa mvua na majanga mbalimbali.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ili kukabiliana na changamoto za uharibifu wa mazingira napendekeza Wizara iimarishe elimu ya utunzaji mazingira na pia kuimarisha ofisi na wataalam katika maeneo ya kimkakati, kama vile Mikoa ya Mbeya na Iringa ambayo ni vyanzo vikuu vya mito ikiwemo Mto Ruaha. Pamoja na elimu, wananchi wa maeneo ya kimkakati ya mazingira wanahitaji motisha ili watunze mazingira yao. Motisha kama vile kupewa kipaumbele cha nishati, miundombinu, elimu na hata kupatiwa miche bure itasaidia kwa kiasi kikubwa utunzaji wa mazingira. Maeneo haya yanahitaji upendeleo wa makusudi ili kukuza uchumi wa wananchi katika maeneo haya na kwa kiasi kikubwa kupunguza uharibifu wa mazingira.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na utunzaji wa mazingira Wizara ya Kilimo ishirikishwe ili kuhimiza kilimo cha kuhifadhi ardhi ambapo mkulima ahitaji kulima kwa jembe wala kuchoma moto. Elimu ya kilimo cha hifadhi ardhi kiendane na pembejeo bora zikiwemo mbegu bora ili wakulima waone tija ya hiki kilimo cha kuhifadhi ardhi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, uharibifu wa vyanzo vya mito umesababisha mito mingi kukauka na pia michanga na udongo kujaza maziwa yetu ikiwemo Ziwa Rukwa ambalo limo hatarini kutoweka. Serikali za Mitaa zihimizwe kutafuta maeneo mbadala ya uchimbaji mchanga ili kunusuru vyanzo vyetu vya mito.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.