Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mpango wa Pili wa Maendeleo wa Taifa kwa kipindi cha Miaka Mitano kuanzia mwaka 2016/2017 – 2020/2021

Hon. Zuberi Mohamedi Kuchauka

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Liwale

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Mpango wa Pili wa Maendeleo wa Taifa kwa kipindi cha Miaka Mitano kuanzia mwaka 2016/2017 – 2020/2021

MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Naibu Spika, maelezo yangu kwenye Mpango huu yatajikita katika Wizara zifuatazo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kilimo; ukizingatia mafanikio kidogo kwa ufanisi wa Mpango wa awali kwa maoni yangu tatizo kubwa linaloikabili mipango yetu mingi ni ukosefu wa uadilifu kwa watekelezaji wa mipango yetu. Ikiwa ni pamoja na nchi kukumbwa na tatizo kubwa la rushwa, ukosefu wa miundombinu bora ya reli na barabara kwa maeneo ya uzalishaji mazao ya kilimo. Hatuwezi kuwa na uchumi mzuri mpaka pale tutakapobadilisha mtazamo wetu na kuacha tabia ya uchumi wetu kutumikia siasa, badala ya siasa kutumikia uchumi. Katika kilimo tuna tatizo la masoko ya wakulima wetu, sambamba na ujenzi wa viwanda vidogo vidogo hasa pale ambapo mazao hayo hulimwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu elimu; miongoni mwa sababu za mipango mingi kutofikia malengo ni mfumo mzima wa elimu yetu, elimu inayotoa wahitimu wasiokuwa na uwezo wa kuingia kwenye soko la ajira ya kujitegemea. Elimu ambayo haiwajengei uwezo wa kujitegemea na badala yake wanakuwa mzigo kwa Serikali; vyuo vya VETA pekee ndio ufumbuzi wa hayo.
Mheshimiwa Naibu Spika, maliasili; hatuwezi kukuza sekta ya utalii kama hatupo tayari kufufua vivutio vilivyosahauliwa kama kivutio kilichopo Liwale (Gofu la Mjerumani la vita ya maji maji lililopo Mjini Liwale) hivi ni kweli ili kuingia Selou ni lazima watalii wapitie Morogoro kwa nini Mkoa wa Lindi (Liwale) imeachwa yatima katika utalii wa ndani na nje?
Mheshimiwa Naibu Spika, tunawezaje kuwashirikisha wananchi kushiriki kulinda rasilimali zetu kama hawataona faida ya moja kwa moja itokanayo ya rasilimali zetu. Utatuzi wa migogoro ya mipaka ya hifadhi zetu ni moja ya kikwazo cha sekta hii kushindwa kufikia malengo.
Mheshimiwa Naibu Spika, miundombinu; ugawaji usiozingatia hali halisi wa miradi ya barabara nchini ni moja ya kikwazo katika Mpango huu. Mfano ni Mkoa wa Lindi ambao mpaka leo mkoa huu haujaweza kuunganishwa na Mkoa jirani wa Morogoro kupitia Liwale na Mkoa wa Ruvuma kupitia Wilaya za Tunduru na Liwale. Sio hivyo tu hata barabara ya Nangurukuru-Liwale ambayo ingeendeleza mazao ya korosho na ufuta ambayo sasa yanalimwa kwa wingi katika Mkoa mzima wa Lindi.
Mheshimiwa Naibu Spika, Sekta ya Afya ni sekta muhimu sana ambayo tumeshindwa hata kuboresha afya za watu wetu hasa katika kupunguza vifo vya mama na mtoto. Mfano, katika Wilaya ya Liwale hakuna hadi leo hospitali yenye hadhi ya kuwa hospitali ya Wilaya. Hospitali haina miundombinu yoyote inayofanana na hospitali ya Wilaya. Wilaya nzima ina kituo kimoja tu cha afya Wilaya yenye Kata 20 na Mpango huu haujasema chochote kuhusu ni namna gani ya kupambana na changamoto hizo.
Mheshimiwa Naibu Spika, ushirikishwaji wa wadau ni muhimu ili mipango yetu iweze kutekelezeka, vile vile uadilifu wa watendaji. Tuongeze bidii ya kupambana na rushwa na uwajibikaji wa pamoja.