Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mpango wa Pili wa Maendeleo wa Taifa kwa kipindi cha Miaka Mitano kuanzia mwaka 2016/2017 – 2020/2021

Hon. Prosper Joseph Mbena

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Morogoro Kusini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Mpango wa Pili wa Maendeleo wa Taifa kwa kipindi cha Miaka Mitano kuanzia mwaka 2016/2017 – 2020/2021

MHE. PROSPER J. MBENA: Mheshimiwa Naibu Spika,, naunga mkono hoja. Kujenga msingi wa uchumi wa viwanda utawezesha nchi kukuza uchumi wake haraka na kutoa ajira nyingi kwa vijana wetu. Muhimu hapa ni kuangalia aina gani ya viwanda tunavyovihitaji, masoko yapi ya nje na ndani tunayalenga na lazima viwanda hivi visambazwe kwenye mikoa na wilaya mbalimbali kuwepo na uwiano tusifanye makosa ya upendeleo katika kusambaza viwanda. Fursa iwe sawa kwa wote, sasa tofauti iwepo tu kwenye upatikanaji wa malighafi husika kwa mahitaji ya viwanda, hapo uwekezaji utaangalia eneo lipi lina comparative advantage na hivyo kusukuma maamuzi ya wapi kiwanda kijengwe.
Mheshimiwa Naibu Spika, hata hivyo, ili kujenga viwanda hivi, tunahitaji miundombinu ijengwe pale ambapo haipo na pale ambapo ipo, miundombinu hii iimarishwe. Miundombinu ya barabara, umeme, maji, simu na mawasiliano mengine ya usafirishaji. Jimbo la Morogoro Kusini lina comparative advantage kwa ujenzi wa viwanda vikubwa na vidogo vidogo vitakavyotumia malighafi zinazopatikana hapo hapo Jimboni.
Mheshimiwa Naibu Spika, Jimbo la Morogoro Kusini kuna maeneo makubwa ya kilimo cha mazao mbalimbali ya chakula na biashara kama vile mpunga, mahindi, ufuta, alizeti, karanga, pamba na mazao mengine, matunda aina zote nanasi, maembe, papaya, machungwa, avocado na kadhalika, viwanda vya kusindika vyakula vinaweza kujengwa humo Jimboni.
Mheshimiwa Naibu Spika, Jimbo pia lina mchango mkubwa wa kutoa kwa faida ya nchi kwenye eneo la madini, misitu, lakini barabara kutoka Bigwa hadi Kisaki kwa kiwango cha lami, ndio itakuwa mkombozi. Mradi huo wa kupanua barabara hiyo ya Bigwa – Kisaki na kuwekwa lami ni muhimu kutekelezwa na ni jukumu la Serikali kutoa fedha za kutekeleza miradi hii muhimu, sio suala la kukabidhi wahisani, hapana.
Mheshimiwa Naibu Spika, suala lingine ni fursa za nchi yetu kufanya biashara nje ya nchi. Mpango wa AGOA ambao Serikali ya Marekani imekubali kuongezea muda zaidi wa miaka 15? Sasa lazima nchi yetu inufaike na mpango huu. Utekelezaji wa miaka 10 iliyopita ya AGOA, haukuwa mzuri. Nchi yetu haikunufaika sana na AGOA. Sasa Serikali isimamie vizuri zaidi tuweze kunufaisha nchi angalau kwa asilimia 90 ya AGOA.
Mwisho, kuwepo na mpango maalum kwenye Mpango wa Serikali utakaowasaidia wananchi wetu wanaopatwa na majanga ya mafuriko ya mvua hususan vjijini. Msaada wa chakula, madawa unapaswa kupelekwa kwa waathirika haraka sana. Maeneo hatarishi kwa wananchi kuishi ni vizuri yasiruhusiwe wananchi kuishi humo, lakini liwe jukumu la Serikali kuwagharamia wananchi hao kuhamishiwa maeneo salama. Kata ya Selembala yenye vijiji vya (i) Magogoni (ii) Kiganila (iii) Bwira juu (iv) Bwira Chini (v) Kiburumo, katika Jimbo la Morogoro Kusini sasa ni Kata hatari ya mafuriko ya mvua kila mwaka na ni hatarishi kwa maisha ya wananchi.
Mheshimiwa Naibu Spika, mafuriko makubwa yaliyotokea tarehe 6 Aprili, 2016 na 16 Aprili, 2016 ni ushahidi tosha, vijiji vyote vitano sio salama tena. Serikali ilipe fidia na kuwaondoa wananchi wote wa vijiji vitano vya Kata ya Selembala (na siyo vijiji vitatu vilivyochaguliwa) ili wote wahamie eneo salama ili Kata yote ya Selembala sasa itumike kwa mradi wa bwawa la maji Kidunda. Napendekeza hata zao la miwa sasa lingeweza kupandwa eneo lote hilo kwa ajili ya viwanda vya miwa katika Jimbo la Morogoro Kusini. Mpango wa Maendeleo lazima uangalie usalama na ustawi wa wananchi.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuwasilisha.