Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Fedha za Ofisi ya Waziri Mkuu na taasisi zilizo chini yake pamoja na Mfuko wa Bunge kwa mwaka 2017/2018.

Hon. Amina Nassoro Makilagi

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Fedha za Ofisi ya Waziri Mkuu na taasisi zilizo chini yake pamoja na Mfuko wa Bunge kwa mwaka 2017/2018.

MHE. AMINA N. MAKILAGI: Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote napenda kuchukua nafasi hii kukushukuru wewe na Mwenyezi Mungu muweza wa yote kwa kunipa nafasi ya kusimama na kutoa mchango wangu katika hoja hii muhimu ya mwelekeo wa kazi za Serikali na Makadirio ya Mapato na Matumizi Ofisi ya Waziri Mkuu na Ofisi ya Bunge kwa mwaka wa fedha 2017/2018.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuipongeza Serikali ya CCM kwa kutimiza mwaka mmoja kwa mafanikio makubwa katika kutekeleza Ilani ya Chama cha Mapinduzi ikiwa ni pamoja na Serikali kuhamia Dodoma. Naungana na mpango wa Serikali kuufanya Mji wa Dodoma kuwa mji
wa kisasa uliopangwa vizuri.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nampongeza Mheshimiwa Waziri Mkuu na timu yake kwa kuandaa hotuba nzuri iliyogusa nyanja zote.
Mheshimiwa Mwenyekiti, leo nimejielekeza katika kutoa mchango wangu katika mambo matatu yafuatayo:-
(i) Uwezeshaji wa wanawake kiuchumi;
(ii) Maji; na
(iii) Afya, elimu na kilimo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika ukurasa wa15 – 17 wa hotuba ya Waziri Mkuu taarifa inaonyesha jitihada zilizofanywa na Serikali katika kuwezesha wananchi kupitia mipango na programu mbalimbali kwa kuwekeza nguvu zaidi kwa wanawake na vijana na watu wenye ulemavu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na kupongeza Serikali nina ushauri katika maeneo yafuatayo; wanawake ndio nguvu kazi, wanawake ndio walezi wa familia, unapomkomboa mwanamke kiuchumi unakomboa familia na Taifa kwa ujumla.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu shilingi milioni 50 kwa kila kijiji; katika Mkutano wa Bajeti wa mwaka wa fedha uliopita 2016/2017 Bunge lilipitisha fedha ikiwa ni utekelezaji wa mpango wa kupeleka shilingi milioni 50 kila kijiji katika baadhi ya mikoa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ningependa kujua ni kiasi gani cha fedha kilitolewa na kilipelekwa katika mikoa ipi, na ni vikundi vingapi vilikopeshwa vikiwemo vya wanawake na Vijana?
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia ningependa kujua ni kiasi gani cha fedha kimetengwa na ni mikoa gani na mingapi itapelekewa fedha hizo?
Mheshimiwa Mwenyekiti, Ningependa kujua ni mamlaka gani imepewa jukumu la kusimamia mpango wa shilingi milioni 50 kila kijiji?
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu Mfuko wa Maendeleo ya Wanawake kutoka Serikali Kuu umekuwa ni mkombozi. Kwa vipindi vya miaka ya hivi karibuni na hata bajeti ya mwaka 2017/2018 mfuko huu haukutengewa fedha, naishauri Serikali itenge na kutoa fedha kwa ajili ya mfuko wa maendeleo ya vikundi vya wanawake kama ilivyofanyika kwa vijana, kutotenga fedha kwa ajili ya wanawake ni kurudisha nyuma jitihada za wanawake katika kujikomboa kiuchumi kwa sababu mfuko huu unaotolewa na Wizara ulikuwa ni ukombozi kwa vikundi vya wanawake badala ya kutengewa asilimia 10 ya mfuko wa wanawake na Halmashauri tu ambao pia hakuna uhakika kwa sababu Halmashauri nyingi hazitengi na kutoa fedha hizo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lipo tatizo katika Halmashauri kutotenga asilimia 10 kwa ajili ya mfuko wa vikundi vya maendeleo ya wanawake na vijana katika Halmashauri zetu. Naomba kutoa ushauri kwamba kwa kuwa utaratibu wa kutoa fedha hizo asilimia 10 ya vikundi vya wanawake na vijana ni maagizo yaliyotolewa na Waziri Mkuu miaka zaidi ya 20 iliyopita, naishauri Serikali kuleta muswada ili Bunge litunge sheria itakayoweka utaratibu wa kutenga, kutoa na kurudisha fedha hizo kwa vikundi vya maendeleo ya wanawake na vijana kuliko ilivyo sasa, kwani jambo la kutoa fedha hizo limebaki kama ni jambo la hisani na si jambo la lazima kwa sababu hakuna sheria inayotekelezwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mujibu wa taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) kila unapofanyika ukaguzi linatokea tatizo la kutotoa fedha vikundi vya wanawake na vijana na katika Halmashauri zilizo nyingi zimeonyesha yapo madeni makubwa. Hapa ningependa kusikia kauli yako Mheshimiwa Waziri Mkuu juu ya ulipaji wa madeni haya ili fedha hizi zielekezwe katika kutoa mikopo kwa vikundi vya wanawake na vijana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, riba katika taasisi zinazotoa mikopo kwa vikundi vya wanawake, vijana na wananchi; pamoja na kuzipongeza taasisi za fedha kwa kutoa mikopo midogo na mikubwa kwa vikundi vya wanawake na vijana. Lipo tatizo katika baadhi ya taasisi za fedha viwango vyao vya riba ni vikubwa sana mpaka kufikia asilimia 35 jambo ambalo husababisha wanawake na vijana kushindwa kujikomboa kiuchumi, badala yake wameambulia kufanya kazi za uzalishaji na kuwanufaisha waliowapa mikopo na wao kuambulia kutaifishiwa mali zao kwa mfano vifaa vya nyumbani kama vitanda, magodoro, vyombo na kuuziwa mashamba.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri wangu ni kwamba naiomba Serikali itoe riba elekezi kwa taasisi zote zinazotoa mikopo kwa vikundi vya wanawake na vijana lengo likiwa ni wanawake na vijana wanufaike na mikopo hiyo kuliko ilivyo sasa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Benki ya Wanawake ilianzishwa kuwakomboa wanawake waishio vijijini na mijini ambao hawana fursa za kufika taasisi nyingine za fedha.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri, naomba Serikali itoe fedha kwa Benki hii ili ipate mtaji wa kufungua matawi katika mikoa yote hapa nchini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, masharti ya kutoa mikopo kwa vikundi vya wanawake pia yaangaliwe upya kwa sababu masharti hayatofautiani na masharti ya benki zingine, hivyo wanawake walio wengi hasa waliolengwa na kuanzishwa kwa benki ni wanawake wanyonge ambao hawana mali za kuweka kama dhamana wanashindwa kukopa katika benki hii. Hivyo malengo ya kuanzishwa kwa benki hii bado hayajafikiwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nashauri Serikali irejee upya masharti ya kutoa na kurudisha mikopo ili benki hii ya wanawake iwe ni mkombozi kwa wanawake na Watanzania kiuchumi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sekta ya maji, katika ukurasa 38 – 39 Mheshimiwa Waziri Mkuu ameeleza kwa kina jitihada zinazofanywa na Serikali za kujenga miundombinu ya maji. Naipongeza Serikali kwa kazi kubwa ya kujenga miundombinu ya maji katika miji mbalimbali hapa nchini. Pia katika ukurasa wa 38 – 39 taarifa inaonyesha kuwa kufikia mwezi Julai na Desemba, 2016, miradi 90 ya miundombinu ya maji vijijini ilikamilika na kufanya mradi iliyokamilika kuwa 1,301 na kubakia miradi 509.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na mafanikio yaliyopatikana, suala la maji bado ni tatizo kubwa sana, wanawake bado wanatembea umbali mrefu kwenda kutafuta maji, wanawake bado wameshindwa kushiriki shughuli za kiuchumi kwa sababu wanatumia muda mrefu kwenda kutafuta maji, bado dhamira ya CCM na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya kuwatua wanawake ndoo kichwani bado haijafikiwa kiwango kizuri.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naishauri Serikali yafuatayo:-
(a) Kutafuta fedha za kutosha hata kama ni kwa mkopo kwa ajili ya utekelezaji wa miundombinu ya maji hasa vijijini.
(b) Serikali na Bunge likubali kuongeza tozo ya mafuta ya petroli na dizeli kutoka shilingi 50 kila lita ya mafuta hadi shilingi 100 katika kila lita ya mafuta. Fedha zitakazopatikana zielekezwe katika ujenzi wa miundombinu ya maji hasa vijijini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ipo baadhi ya miradi ya ujenzi wa miundombinu ya maji iliyopangwa kutekelezwa kwa fedha za nje mfano, ujenzi wa mradi wa maji Mwanga, Same hadi Korogwe, ujenzi wa mradi wa maji Mgango, Kiabakari, Butiama, ningepeda kujua fedha za kutekeleza
miradi hii zimekwishapatikana na mradi wa Mwanga, Same na Korogwe upo katika hatua gani? Je, mradi wa Mgango, Kiabakari na Butiama unaanza lini? Kwa sababu mpango wa mradi huu ni wa muda mrefu sana. Mradi wa Muyayango, Sokoni Butiama ni miradi ya muda mrefu lakini mpaka sasa miradi hii ya Mgango, Kiabakari Butiama haijaanza na Mwanga, Same na Korogwe ni wa muda mrefu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sekta ya afya katika ukurasa wa 39 Mheshimiwa Waziri Mkuu ameeleza kazi inayofanywa na Serikali ya kuhakikisha wananchi wanapata afya bora kwa kuboresha miundombinu na upatikanaji wa vifaa tiba pamoja na kuimarisha huduma ya mama na mtoto ili
kupunguza vifo vya wanawake na watoto pamoja na kazi nzuri ya Serikali, naomba kuishauri Serikali kufanya yafuatayo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuweka mikakati itakayopunguza vifo vya wanawake wanaofariki kwa kujifungua kwa mujibu wa utafiti uliofanyika unaonyesha kuwa kila saa moja mwanamke mmoja anafariki kwa tatizo la kujifungua.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ujenzi vituo vya afya ambavyo havijakamilika Serikali ijitahidi kukamilisha vituo vya afya vilivyojengwa ambavyo havijakamilika. Serikali ijitahidi kutafuta fedha na kukamilisha miundombinu ya vituo hivyo ili viweze kuanza kazi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ujenzi wa vituo vipya vya afya kila Kata; naishauri Serikali itafute fedha na kujenga vituo vya afya kila mwaka tuwe na vituo vya afya kila Halmashauri za Wilaya vinavyojengwa ikiwa ni hatua muhimu ya utekelezaji wa Ilani ya CCM.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu elimu; naipongeza Serikali kwa kazi nzuri ya kutoa elimu isiyo na malipo pamoja na pongezi, nashauri Serikali kufanya yafuatayo:-
(i) Kuongeza madarasa katika kila shule ya msingi kwa sababu ongezeko la wanafunzi limeleta tatizo la ukosefu wa madarasa ya kutosha.
(ii) Ujenzi wa mabweni katika shule za sekondari kwa sababu watoto wetu na hasa watoto wa kike wanapata adha kuishi mtaani, kutembea umbali mrefu jambo linasababisha pia mimba za utotoni.
(iii) Kuongeza nyumba za walimu na maslahi ya walimu.
(iv) Upungufu wa walimu wa sayansi, hapa ningependa kujua Serikali kwa sasa ina mkakati gani wa kuongeza walimu hao wa sayansi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kilimo, nashauri Serikali iongeza wigo kwa kilimo cha umwagiliaji katika maeneo yanayozungukwa na maziwa na mito na maeneo yenye ukame ili kuongeza upatikanaji wa chakula kwa uhakika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.