Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Fedha za Ofisi ya Waziri Mkuu na taasisi zilizo chini yake pamoja na Mfuko wa Bunge kwa mwaka 2017/2018.

Hon. Maftaha Abdallah Nachuma

Sex

Male

Party

CUF

Constituent

Mtwara Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Fedha za Ofisi ya Waziri Mkuu na taasisi zilizo chini yake pamoja na Mfuko wa Bunge kwa mwaka 2017/2018.

MHE. MAFTAHA A. NACHUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi hii niweze kuchangia makadirio haya ya bajeti ya Ofisi ya Waziri Mkuu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimshukuru Mwenyezi Mungu ambaye amenijalia kuwa na afya njema na leo hii naweza kuchangia bajeti hii ipasavyo na siyo matusi kama wanavyofanya wachangiaji wengine. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nikianza moja kwa moja na Ofisi ya Msajili wa Vyama vya Siasa…
Taarifa...
MHE. MAFTAHA A. NACHUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeipokea taarifa, wasubiri, wasikilize kwa sababu sichomi sindano nazungumza maneno tu ya kawaida. (Makofi/Kicheko)
Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati niko mwaka wa kwanza Chuo Kikuu cha Dar es Salaam nilikuwa napitia kitabu kimoja kimeandikwa na Ishumi na Nyirenda cha saikolojia. Kuna kipengele kimoja amekieleza kwa kiasi kikubwa sana, kwamba philosophy is the study of fundamental
questions. Wakati anaeleza Mheshimiwa huyu Ishumi na Nyirenda akaliweka neno moja kwamba falsafa maana yake wewe unayesoma lazima uweze kujiuliza swali kwamba hiki unachoelezwa maana yake ni nini?
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, lazima uweke swali, why, kwamba umeelezwa nenda Bungeni, kamtukane Mheshimiwa Sakaya, Mheshimiwa Profesa Lipumba, Mheshimiwa Maftaha na Msajili wa Vyama vya Siasa halafu unabeba kama mbuzi, umebeba kama mzigo kwenye gunia unakuja Bungeni na wewe unakuja kutukana. Hii ni kukosa weledi na kukosa ufahamu wa kielimu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, mimi kama nimesoma shule nimeelimishwa, siwezi kufanya haya. Kila unalotumwa na mtu kwamba kalifanye hili, lazima nijiulize kwa nini eti unanituma niende nikamtukane Mwenyekiti wa Chama Taifa, siwezi kufanya haya kwa sababu nina uelewa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kuna suala hapa limepotoshwa kwa kiasi kikubwa sana. Waheshimiwa Wabunge hapa wamekuwa wakizungumza na hawapo wamekimbia nje, kwamba eti Msajili wa Vyama vya Siasa amemrudisha Mwenyekiti wa Chama Taifa, Profesa Ibarahim Lipumba kuwa Mwenyekiti wa Chama, hili naomba nikanushe na Watanzania na Bunge hili liweze kufahamu sio kweli. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Chama cha Wananchi CUF mwaka jana 2016 mwezi Agosti, tarehe 21, tulikuwa na Mkutano Mkuu wa Chama Taifa. Naomba nizungumze haya ili Watanzania waweze kufahamu kwamba ni nini kinaendelea ndani ya Chama cha Wananchi CUF badala ya kumbebesha mzigo Msajili wa Vyama vya Siasa. Tarehe 21 Agosti 2016 tulipofanya Mkutano Mkuu Chama cha Wananchi CUF kulikuwa na mambo ambayo hayakufanywa sawasawa na Katibu wa Chama kwa makusudi kabisa eti kwa sababu hamuhitaji Profesa Lipumba kuwa Mwenyekiti wa Chama wakati Katiba ya Chama cha Wananchi CUF, Ibara ya 117(1)(2) kinaonesha kabisa kwamba Mwenyekiti wa Chama
cha Wananchi CUF ni Profesa Ibrahim Haruna Lipumba.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tukiwa katika mkutano wetu wa ndani ya chama tuliweza kuona mambo ambayo kimsingi siyo mambo ambayo yanaweza yakafanywa na kiongozi mkubwa kama Katibu Mkuu wetu wa Chama cha Wananchi CUF. Mambo yaliyotokea, kwa sababu
tunazungumza suala la utawala bora hapa na utawala bora pamoja na vyama viendeshe taratibu zao sawasawa. Naipongeza Ofisi ya Msajili wa Vyama vya Siasa na Ofisi ya Waziri Mkuu kwa kusimamia vyama vyetu vya siasa sawasawa kwa sababu watu wanatumia kama SACCOS zao binafsi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tulivyoingia kwenye ukumbi wa mkutano upande wa Katibu Mkuu wa Chama, Maalim Seif Shariff Hamad alileta wajumbe 116 kutoka Zanzibar kinyume na taratibu za Katiba ya CUF eti waje kupiga kura ya hapana. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nilikuwa miongoni mwa watu waliouliza maswali ndani ya ukumbi ule, nikahoji kwamba hawa wajumbe 116 ambao wameongezwa kutoka upande wa Zanzibar wapo kwa mujibu wa Katiba na kama wameongezwa mbona upande wa Bara hawapo? Majibu yalikuwa ni kwamba hao wameongezwa ni wajumbe maalum. Tukamuuliza wajumbe maalum mbona huku Bara haukuwateua wajumbe maalum, wakawa hawana majibu wakasema tutawafukuzeni chama, hivi vyama lazima viangaliwe. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la kusema kwamba eti Msajili kazi yake ni kusajili tu vyama vya siasa na baadaye kuvifuta, Sheria Na. 5 ya mwaka 1992 ilivyoanzisha vyama vya siasa inampa mamlaka Msajili wa Vyama vya Siasa kusajili pamoja na kuvilea. Naomba niulize swali, hivi unavyosema kuvilea maana yake ni nini, ni kwamba kumchukua mtoto kumweka pale na wewe ukatembea zako, si lazima umwangalie mwenendo wake na takwimu zake ziko vipi?
Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi kama Wajumbe wa Mkutano Mkuu Taifa wa Chama cha Wananchi CUF tarehe 21, Agosti, 2016 tulivyoona kwamba yanafanyika mambo ambayo ni kinyume na taratibu za uendeshaji wa vikao vyote duniani tukasema kwamba hatuwezi kukubaliana na haya. Wajumbe asilimia 99 kutoka upande wa Tanzania Bara tulikuwa tunataka marekebisho na utaratibu uendeshwe sawasawa likiwemo suala la kuondolewa wajumbe 116 walioletwa kinyume na taratibu za Katiba ya CUF. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tulivyomueleza Mheshimiwa Katibu akasema hapana hatutakubaliana na hilo. Pia tukamhoji kwamba kuna watu wameongezwa tunaambiwa wanatoka vyama vingine wameongezwa kama wajumbe waje kupiga kura humu ndani tunaomba tufanye uhakiki wa kila wilaya, akakataa akasema hatufanyi uhakiki, mimi ndio Katibu Mkuu, mimi ndiyo mwenye chama. Sisi tulichofanya tukasema hatuwezi kuendelea na mjadala huu mpaka haya yarekebishwe, kama Wajumbe wa Mkutano Mkuu Taifa tuna uhalali wa kuyarekebisha haya. Wakaenda juu wakaleta vyombo vya habari wakasema kwamba tunakwenda kulazimisha kupiga kura wakati wajumbe zaidi ya 400 tulikataa kwamba tusipige kura kwa sababu hoja ya Kujiuzulu kwa Mwenyekiti ni lazima sisi Wajumbe wa Mkutano Mkuu tukubali sasa Mheshimiwa umejaza wajumbe kutoka Zanzibar ambao sio halali ili kuongeza namba, hatuwezi kukubaliana na hilo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, yapo mengi sana, wakaingia wakaita vyombo vya habari wakasema Mkutano Mkuu umeridhia kujiuzulu kwake kitu ambacho siyo sahihi kabisa. Sisi ndani ya ukumbi tukasajili majina yetu, zaidi ya 324 tukaenda kwa Msajili wa Vyama vya Siasa tukilalamika
kwamba taratibu za uendeshaji wa vikao vya Chama hiki cha Siasa cha CUF zimekiukwa kwa makusudi, tunaomba utupe tafsiri. Msajili wa Vyama vya Siasa alituita sisi wote, upande wa walalamikaji sisi Wajumbe wa Mkutano Mkuu zaidi ya 320, upande wa Katibu Mkuu, tukaitwa tukakaa wote tukawa tumepewa miongozo zaidi ya mara nne, mara tano na mwisho wa siku Msajili wa Vyama vya Siasa akatoa mwongozo kwamba kwa mujibu wa Katiba ya CUF Profesa Ibrahim Lipumba ndio Mwenyekiti halali wa Chama cha Wananchi CUF Taifa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nazungumza haya kwa sababu yameelezwa sana, kuna upotoshwaji unaofanywa kwa makusudi eti kwa sababu ya kuwahadaa Watanzania kwa sababu ya kutafuta huruma kupitia Bunge hili wanakuja wanasema uongo eti kwa sababu wametumwa na mtu mmoja. Chama ni taasisi, chama sio mtu mmoja, chama ni uamuzi wa wanachama ndugu zangu na tunasema tutasimamia hili mpaka mwisho wetu na Profesa Lipumba ndiyo Mwenyekiti halali wa Chama cha Wananchi CUF. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna suala hapa limezungumzwa kwamba Msajili wa Vyama vya Siasa eti ametoa ruzuku akishirikiana na wahuni wake. Naomba nizungumze tu kwamba ruzuku ya Chama cha Wananchi CUF imeletwa kwa mujibu wa Sheria ya Ruzuku za Vyama vya Siasa na hivi ninavyozungumza baada ya ruzuku kuletwa kwenye chama, Mheshimiwa Mwenyekiti na Kamati Tendaji Taifa, hata mimi ni mjumbe pia, ni Mkurugenzi wa Mambo ya Nje ya Chama cha Wananchi CUF, tulikaa tukapeleka ruzuku wilayani. Tulivyopeleka ruzuku Wilayani ili ziweze
kujenga chama na kulipia posho, Mheshimiwa Katibu Mkuu wa Chama cha Wananchi CUF akaandika barua kwa Meneja wa Benki Kuu kwamba afungie ruzuku akaunti za wilaya ambazo hata yeye hana mamlaka nazo na tunashangaa sana. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naiomba Ofisi ya Waziri Mkuu ilishughulikie hili suala kwamba kwa nini Meneja wa NMB Tanzania ameandikia barua akaunti zote za wilaya za Chama cha Wananchi CUF ambazo wao ndiyo wamefungua akaunti, hazikufunguliwa na Katibu Mkuu Maalim Seif Shariff Hamad lakini hivi ninavyozungumza zimefungiwa na zile pesa hazifanyi kazi ya chama, ziko kwenye akaunti za NMB Tanzania nzima. Tunaomba sana huyu Meneja wa NMB Taifa achukuliwe hatua kwa nini anaingilia akaunti za Chama cha Wananchi CUF ngazi ya wilaya.
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo nataka nizungumze ni suala hili la viwanda ambalo limeelezwa kwa kiasi kikubwa sana. Miaka ya karibuni Serikali iliweza kupitisha sera kwamba ajira zote hivi sasa ziweze kusimamiwa na wamiliki wa viwanda na taasisi husika. Hata hivyo, pale Mtwara katika kiwanda cha… (Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)
MHE. MAFTAHA A. NACHUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa kunipa nafasi na niseme tu kwamba naunga mkono hoja.