Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Fedha za Ofisi ya Waziri Mkuu na taasisi zilizo chini yake pamoja na Mfuko wa Bunge kwa mwaka 2017/2018.

Hon. Joseph Roman Selasini

Sex

Male

Party

CHADEMA

Constituent

Rombo

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Fedha za Ofisi ya Waziri Mkuu na taasisi zilizo chini yake pamoja na Mfuko wa Bunge kwa mwaka 2017/2018.

MHE. JOSEPH R. SELASINI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi hii.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kabla sijachangia, naomba nichukue nafasi hii kuwatakia Wakristo wote walio hapa Bungeni na kote Tanzania kila la kheri katika siku hizi kuu za Juma kuu zitakazoanza kesho ili ziwe kwao baraka na neema katika maisha na kazi zao.
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, napenda kusema kwamba, mimi ni Mbunge wa Rombo na katika siku mbili, tatu zilizopita jina la Ben Sanane limetajwa sana hapa Bungeni. Ben Sanane ni mpiga kura wangu, amezaliwa Tarafa ya Mashati, Kata ya Katangara Mrere, Kijiji cha Mrere na Kitongoji cha Kilosanjo.
Baba yake ni Mzee Focus Benard Sanane na mama yake ni mama Arinata Ben Sanane. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi watu wa Rombo tuna uchungu wa hali ya juu sana kwa sababu tangu jambo hili liliporipotiwa watu wa Rombo hususan familia na ukoo wa Mzee Focus Ben Sanane umetahayari, hawajui wafanye matanga, hawajui wafanye nini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kabla sijaendelea kusema ninachokusudia kusema kuhusu jambo hili, nichukue nafasi hii kwa niaba ya Mzee Focus Benard Sanane na Mama Arinata Benard Sanane kutoa shukrani za dhati kwa Wabunge wote, vyombo vya habari, viongozi wote na wote wenye mapenzi mema ambao kwa namna moja au nyingine wamekuwa wakiomba, wakishinikiza, wakishauri kwamba jambo hili lifanyiwe kazi na Serikali ili tujue mwisho wake. Waheshimiwa Wabunge sisi wote ni wazazi, akinamama mlio Wabunge mnajua uchungu wa uzazi…
Mnajua uchungu ambao mama Arinata Benard Sanane anaupata. Mheshimiwa Jenista Mhagama dada yangu, fikiria kwa mfano yule
mwanangu Victor angekuwa amekumbwa na sakata kama hili, ungekuwa katika hali gani, unatikisa kichwa kwa
uchungu kwa sababu huu ndiyo uchungu ambao watu wa Rombo wanao, huu ndiyo uchungu ambao mama Arinata anao. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, mwezi Oktoba mwaka jana, kuna mtu aliyejitambulisha kama Joackim, Afisa wa Takwimu wa Halmashauri ya Wilaya ya Rombo. Alikwenda kwenye Ofisi za CHADEMA pale Wilayani. Baada ya kujitambulisha, akaomba kujua kama Ben Sanane ni mwanachama wa CHADEMA. Akaomba kujua kama Ben Sanane huwa anafika maramara katika Ofisi za CHADEMA. Akaomba kujua nyumbani kwa Ben Sanane na baada kukusanya taarifa alizozitaka mwezi wa Novemba tukasikia kupotea kwake, tupo katika lindi kubwa la mashaka.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu hiyo, niishie tu kusema nawaomba Wabunge, naiomba Serikali, nawaomba na Watanzania wote msifanye jambo hili kuwa jambo la siasa. Jambo hili linaumiza watu, jambo hili lina machungu makubwa miongoni mwa mioyo ya watu.
Nawaomba na nawasihi na Warombo wenzangu wananisikia na familia ya Ben, Mzee Focus na Mama Arinata wananisikia, tunaomba sisi watu wa Rombo Serikali tuambieni chochote ambacho mnacho.
Tuambieni kama mmeshindwa tulie, yaishe. Tuambieni kwamba amekufa ili tujue tufanye matanga. Haiwezekani tukakaa kama familia kwenye suspense tu hivi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, nirudi kwa Warombo wenzangu katika mambo mengine ya maendeleo yanayowahusu. Katika kipindi hiki cha mwaka, tulipata bahati ya kutembelewa na Waziri wa Mambo ya Ndani pamoja na Naibu wake, waliutembelea mpaka wa Rombo pamoja na shughuli zinazohusu Wizara ya Mambo ya Ndani. Nataka niwashukuru kwa sababu tuumeendelea kutekeleza yale waliyoshauri.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kwa sababu ya urefu wa mpaka wa Rombo na Kenya, watu wa Rombo wameamua kujenga kwa namna ya kujitolea vituo vya polisi.
Kituo cha Ngoyoni, Mahida, Mengwe, Useri na Kirongo Chini. Wamejenga na wanaendelea kujenga kwa kuchangia ili waweze kukaa katika hali ya usalama kwa sababu mpaka unaingiza mambo mengi na unawahusu sana katika usalama wao. Naiomba Serikali katika bajeti hii iangalie namna ya kusaidia hizi nguvu za wananchi ili hivi vituo viweze kukamilika tuweze kupata huo msaada au tuweze kupata hiyo huduma
kutoka polisi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Naibu Waziri TAMISEMI, Mheshimiwa Jafo pia alitembelea Rombo na tunamshukuru. Alitembelea miradi kadhaa, kati ya mradi uliotembelewa ni ujenzi wa jengo la halmashauri. Nimesikia Wabunge wenzangu ambao halmashauri zao ni mpya wakiomba
majengo ya halmashauri yajengwe na yakamilike. Rombo ni halmashauri ambayo ina umri zaidi ya miaka 30 lakini haina jengo la halmashauri. Jengo wanalotumia lilitaifishwa kutoka kwa Masista wa Shirika la Masista Kilimanjaro. Ujenzi unaendelea lakini umekwama kwa sababu mkandarasi amekosa fedha. Tunaomba fedha zipelekwe ili kuweza kukwamua ujenzi ambao unaendelea.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo ni Hospitali ya Wilaya. Vilevile hatuna Hospitali ya Wilaya.
Hospitali ya Huruma ni Hospitali ya Kanisa Katoliki Jimbo la Moshi. Kituo cha afya cha Karume tuliamua kwa makusudi ijengwe hapo Hospitali ya Wilaya, ujenzi unaendelea nao umekwama kwa sababu ya ukosefu wa fedha. Naomba sana jitihada zifanyike ili jengo hilo liweze kukamilika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu maji. Waziri wa Maji ametusaidia kuifuta Kill Water. Namshukuru Waziri na nimpe taarifa tu kwamba wataalam kwa ajili ya kutusaidia kuanzisha mamlaka wameshafika Rombo wanaendelea na kazi. Naomba msukumo uweze kufanyika ili tupate hiyo
mamlaka, kwa Rombo kuna shida kubwa sana ya maji hasa ukanda wa chini. Mamlaka itatusaidia kwa sababu kuna chanzo cha Ziwa Chala, kuna vyanzo vingine kule Rongai ambavyo tunaambiwa vinapeleka maji Kenya ili kuweza kutatua tatizo la maji katika halmashauri yetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu afya, ni wataalam katika vituo vya afya. Kwa sababu wananchi wa Rombo wamejitahidi kujenga zahanati na kadhalika tunaomba sana waungwe mkono katika hili.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu elimu, tuna uhaba mkubwa sana wa walimu wa sayansi. Rombo tuna shule za kata karibu 41 lakini tangu tumeanza shule za kata hatuwahi kupata mwalimu hata mmoja wa sayansi katika baadhi ya shule.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu maliasili, tunavamiwa sana na nyani, ukanda wa juu. Nimesikia kuna utaratibu wa kuhamisha nyani na kuwapeleka mahali pengine. Tunaomba Serikali ione uwezekano wa kuwasaidia hawa wananchi ambao wanapambana na nyani kila kukicha, wanashindwa kufanya kazi zao kwa sababu ya kupambana na nyani.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho ni suala la njaa. Rombo kwa kawaida tunapata chakula kutokana na mvua za vuli lakini mvua za vuli mwaka huu hazijanyesha. Kwa hiyo, ukanda wa chini wa Rombo sio siri wananchi wana shida kubwa sana ya chakula. Mimi sijatembelea mikoa
mingine Serikali inasema nchi ina chakula, naomba ufanyike utaratibu chakula kilicho katika maeneo mengine ya nchi kiweze kusambazwa ili kusaidia wananchi wa maeneo mengine hususan katika Jimbo langu la Rombo. Watu wa Rombo siyo wavivu, akinamama wanalima kila wanapopata fursa lakini jambo ambalo limetufanya tukaingia katika hali hiyo kwa Ukanda wa Chini ni kwa sababu ya hali ya ukame,
mvua hazikunyesha tukapata shida. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho kabisa ni zao la kahawa ambalo lilikuwa zao la biashara katika Wilaya ya Rombo. Chama cha Ushirika KNCU kilitusaidia sana, lakini kimeingiliwa na mafisadi, wanauza mali za KNCU, wameuza
magari, nyumba na rasilimali zote za KNCU hatimaye wameshindwa kulisaidia zao lile. Matokeo yake gharama za uzalishaji wa zao lile zimekuwa kubwa, kodi imekuwa kubwa…
(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)
MHE. JOSEPH R. SELASINI: Mheshimiwa Mwenyekiti,
ahsante sana, naomba sana Serikali itusaidie katika hayo.