Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Fedha za Ofisi ya Waziri Mkuu na taasisi zilizo chini yake pamoja na Mfuko wa Bunge kwa mwaka 2017/2018.

Hon. Shabani Omari Shekilindi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Lushoto

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Fedha za Ofisi ya Waziri Mkuu na taasisi zilizo chini yake pamoja na Mfuko wa Bunge kwa mwaka 2017/2018.

MHE. SHAABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi hii na mimi niweze kuchangia hoja ambayo ipo mbele yetu.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kabisa nimpongeze Waziri Mkuu kwa hotuba yake nzuri ambayo imesheheni mambo mazuri. Pia nipongeze Kamati zote tatu kwa maana ya Kamati ya UKIMWI, Kamati ya Katiba na Kamati ya Sheria na Bajeti kwa kuwasilisha vizuri maoni yao. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kabisa, nimshukuru Mwenyezi Mungu pamoja na ninyi, ambaye ametujalia afya na nguvu kuweza kuhudhuria na kusema chochote katika Bunge lako hili Tukufu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niende moja kwa moja katika kuchangia na nianze na afya. Kama unavyofahamu Chama chetu cha Mapinduzi ambacho ndiyo chenye Serikali Ilani inasema kila kata itajengwa kituo cha afya na kila kijiji itajengwa zahanati. Kwa kuzingatia hilo
sasa kwenye Jimbo langu la Lushoto nimebahatika kujenga zahanati kumi na tatu na vituo vya afya viwili. Zahanati karibia tatu zimeisha zinahitaji madaktari na nyingine kama tano zimepigwa bati lakini bado usafi na zilizobaki bado zinahitaji kumaliziwa. Kwa hiyo, sasa niombe Serikali yako Tukufu kwamba ipeleke pesa katika halmashauri ili iweze kumalizia zahanati zile. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, Wilaya ya Lushoto ina Majimbo matatu na Hospitali ya Wilaya moja. Takribani Wilaya ya Lushoto ina wakazi zaidi ya laki sita lakini hospitali ile imehemewa yaani inajaza kiasi kwamba kwa kweli sijui nieleze nini. Niiombe Serikali na niishauri katika bajeti hii inayokuja basi watenge bajeti ya kutosha ili Hospitali ile ya Wilaya iweze kupanuliwa hususan chumba cha akina mama wajawazito na chumba cha mama na mtoto. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nielekee kwenye kilimo. Niiombe Serikali yangu tukufu ijielekeze katika sekta ya kilimo kwani kama tunavyofahamu kilimo ndiyo uti wa mgongo wa Taifa letu hili na kimebeba takribani asilimia sabini. Niiombe Serikali yangu itenge mafungu ya kutosha katika
kilimo na pia iwawezeshe wakulima wetu wadogo wadogo hawa hususan wa vijijini. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, Wilaya ya Lushoto ni ya milima na mabonde, ni ya wakulima wa bustani mfano mbogamboga na matunda. Wakulima wale wanachangia asilimia kubwa katika Halmashauri zetu lakini cha kushangaza hawapati pembejeo. Niiombe Serikali sasa kwa jicho la huruma iwaangalie wakulima wale wa mbogamboga hususan wale waishio Lushoto waweze kupata pambejeo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na hayo naiomba Serikali iweze kujenga mabwawa katika Wilaya ya Lushoto kwani mvua nyingi sana zinanyesha kule lakini zinaharibikia baharini. Kwa hiyo, niiombe Serikali sasa ijenge mabwawa ili wananchi wetu waweze kulima kilimo cha
umwagiliaji. Pia hii itakuwa ni fursa kwa vijana wetu na ili wasikimbilie mjini basi tuwajengee miundombinu ili waweze kujiajiri wenyewe na kulima kilimo cha umwagiliaji. Naamini hii italeta tija kwa vijana wetu na wala hawatakimbilia mjini. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nije kwenye miundombinu. Kwanza kabisa nimpongeze Mheshimiwa Mbarawa kwa kazi kubwa anayoifanya. Ila nimuombe sasa kuna barabara hiyo tangu ninasoma darasa la kwanza kila siku naambiwa itapanda hadhi, lakini haipandi. Barabara hiyo imeanzia Mlalo - Ngwelo - Mlola - Makanya ikaenda mpaka kwa mzee wangu Mheshimiwa Kitandula. Nimuombe sasa Mheshimiwa Waziri Mbarawa hebu afumbe macho tu barabara ile ipandishwe hadhi kwani ni muda mrefu sana na kila nikisimama kwenye Bunge lako Tukufu naisemea barabara ile. Kwa heshimiwa kubwa na taadhima niliyokuwa nayo kwake nimuombe basi barabara safari hii ipandishwe hadhi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kuna barabara zetu za mchepuko. Kama unavyofahamu Lushoto ni ya milima na mabonde kwa hiyo Lushoto bila barabara kwa kweli hatuwezi kusafiri. Lushoto kuna barabara kuu moja tu ikipata breakdown basi sisi Lushoto tumekwisha hata mahitaji
tunashindwa kupata. Kwa hiyo, niiombe Serikali yako Tukufu sasa Mheshimiwa Mbarawa kwamba kuna barabara ambayo inatoka Dochi - Ngulwi mpaka Mombo ni ya mchepuko na itakuwa mbadala kwa ajili ya breakdown itakayotokea maeneo ya Soni - Mombo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kuna barabara aliahidi Mheshimiwa Rais wa Awamu ya Nne kilometa nne mpaka sasa sijapata maelezo yake. Niiombe sasa Serikali yako Tukufu hebu tuweze kupatiwa kilometa nne zile angalau tuweze kutengeneza Mji wetu wa Lushoto. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, niiombe sasa Serikali hususan Waziri wa TAMISEMI kwamba zile barabara ambazo zipo Halmashauri zirudi kwa Wakala wa Barabara yaani TANROADS. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile kuna hii Idara ya Ardhi kule Halmashauri nayo irudi kwa Mkuu wa Wilaya kwa sababu ndiye anayesuluhisha migogoro ya ardhi zaidi kuliko Halmashauri. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, elimu; Wilaya ya Lushoto kama nilivyosema ina Majimbo matatu lakini haina chuo cha VETA. Kwa hiyo, nimuombe mama yangu mpendwa Waziri wa Elimu atujengee hata chuo kimoja cha VETA kwani maeneo yapo tayari, kuna karakana, gereji na majengo
mengine. Kwa hiyo, nimuombe Waziri wangu huyu aweze kuliona hilo.
Mheshimiwa Naibu Spika, nimefanikiwa kujenga maboma zaidi ya ishirini, lakini bado hayajaezekwa kwa maana ya kupigwa bati. Sasa basi niiombe Serikali yako na Waziri wa TAMISEMI apeleke pesa za kutosha kule kwenye Halmashauri ili maboma yale ambayo tumeyajenga kwa
nguvu za wananchi tuwape moyo wasije kukata tamaa juu ya hili. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, suala la umeme; kwanza nimpongeze kaka yangu Mheshimiwa Muhongo kwa kazi kubwa anayoifanya na Naibu wake, ila nimuombe kitu kimoja maana tunapata maswali magumu sana kule vijijini, unakaa tu hapa Bungeni unapigiwa simu haya vijiji vingapi
vimepata umeme unawaambia jamani bado hata orodha hatujaipata. Kwa hiyo, nimuombe Waziri wangu sasa niweze kupata ile orodha ya vijiji ili niweze kuwajibu watu wangu wale. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, ajira kwa vijana; kama unavyofahamu sasa hivi vijana ni wengi mno hususan vijana wa bodaboda na wauza mitumba. Kwa hiyo, niiombe Serikali sasa wajengewe uwezo ili waweze kujiajiri wenyewe na kama unavyofahamu sasa hivi vijana wengi wemejiunga na vikundi na wana SACCOS zao. Pia hizi SACCOS naomba ziundwe kisheria ili zitambulike na kukopesha hapa nchini.
Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante naomba kuunga mkono hoja.