Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Fedha za Ofisi ya Waziri Mkuu na taasisi zilizo chini yake pamoja na Mfuko wa Bunge kwa mwaka 2017/2018.

Hon. Jumaa Hamidu Aweso

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Pangani

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Fedha za Ofisi ya Waziri Mkuu na taasisi zilizo chini yake pamoja na Mfuko wa Bunge kwa mwaka 2017/2018.

MHE. JUMAA H. AWESO: Mheshimiwa Naibu Spika, nikushukuru kwa kunipa nafasi hii nami niweze kuchangia hotuba ya Waziri Mkuu iliyopo mbele yetu.
Mheshimiwa Naibu Spika, pia naomba nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunijaalia afya njema ili nami niweze kushiriki Bunge. Tulikuwa na wenzetu ambao walipenda kushiriki nasi lakini wamepoteza roho zao. Namwomba Mwenyezi Mungu azilaze roho za Marehemu mahali pema
peponi. Amina.
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda nimpongeze Rais wangu, Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli kwa kazi kubwa na nzuri anazozifanya katika nchi yetu. Kazi zinaonekana, yapo baadhi ya maneno, lakini nasema, unaweza kuwa na macho lakini usione, unaweza kuwa na masikio usisikie; na unaweza kuwa na pua pia ukashindwa kunusa. Ila kubwa naomba Mwenyezi Mungu aendelee kumpa nguvu kuhakikisha kwamba analeta maendeleo katika nchi yetu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lingine napenda nimpongeze Mheshimiwa Waziri Mkuu pamoja na Baraza lake la Mawaziri kwa kazi kubwa wanayoifanya. Naomba wasonge mbele pamoja na changamoto kubwa, lakini naamini bahari kubwa ndiyo ivukwayo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nimesimama hapa napenda nichangie baadhi ya maeneo hususan katika suala zima la barabara. Ujenzi wa barabara umeweza kuchochea shughuli mbalimbali za kiuchumi na kuwezesha hata kuongeza ajira katika baadhi ya maeneo. Pia natambua
shughuli kubwa inayofanywa na Wizara ya Ujenzi katika kuhakikisha kwamba inaimarisha miundombinu ya ujenzi katika maeneo mbalimbali ya nchi yetu.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nioneshe masikitiko yangu kuhusu kusahaulika ujenzi wa barabara ya Tanga – Pangani – Saadani - Bagamoyo. Ahadi ya ujenzi wa barabara ya Tanga – Pangani - Saadani ni ahadi ambayo tangu sijazaliwa mpaka sasa, leo hii nimeingia Bungeni.
Mheshimiwa Naibu Spika, alikuja hapa Mheshimiwa Rished miaka 15, ameizungumzia barabara ya Tanga – Pangani – Saadani, lakini Serikali
imemwahidi itajenga; amekuja Mheshimiwa Pamba akaambiwa barabara ipo kwenye upembuzi. Leo nimeweza kuibana Serikali, lakini bado inaniambia kwamba Serikali imeonesha nia, itaweza kutengeneza. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, itambulike kabisa, hata ukitaka kufunga Mwezi Mtukufu wa Ramadhani, ni lazima uoneshe nia; lakini ikifika saa 12.00 si unafuturu! Hivi kuna kizungumkuti gani katika kuijenga barabara ya Tanga – Pangani - Saadani?
Mheshimiwa Naibu Spika, binadamu wameumbwa na wivu, binadamu wameumbwa na matamanio; leo tunaona baadhi ya maeneo mbalimbali yanatengenezewa barabara za lami, hivi sisi Pangani tumemkosea nini Mwenyezi Mungu? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, Wilaya yetu ya Pangani uchumi wetu tulikuwa tukitegemea zao la mnazi. Mnazi umekufa, lakini leo ili mtu aje Pangani lazima aje kwa makusudi maalum. Tuna Mbuga ya Saadani, lakini wawekezaji au watalii wanashindwa kuja kwa sababu ya miundombinu mibovu ya barabara. Leo tunaona mvua zinazonyesha, shughuli mbalimbali zimekwama. Naomba Mheshimiwa Waziri Mkuu katika hitimisho lake, kuna barabara ambazo zimeshafanyiwa upembuzi na usanifu, ni nini mkakati wa Serikai kuhakikisha kwamba inajenga barabara hizi ili sasa turudishe imani kwa wananchi? Wakati mwingine wananchi wanasema tumekuja Bungeni kusinzia na kunywa juice.
(Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, mnyonge mnyongeni, haki yake mpeni. Naomba katika bajeti hii Serikali ihakikishe kwamba inatujengea barabara ya Tanga – Pangani – Saadani. Kama tulikuwa pangoni, sasa na sisi tupae angani ili tuweze kupata maendeleo ya dhati kabisa katika nchi yetu.
Mheshimiwa Naibu Spika, lingine ambalo nilikuwa nataka nilizungumzie ni kuhusu suala zima la maji. Tumekuwa na chanzo kikubwa cha maji katika Wilaya yetu ya Pangani. Tuna mto Pangani ambao unatiririsha maji baharini ambao umekata katikati ya mji, lakini tumekuwa na tatizo kubwa la maji. Leo tunaona wananchi wetu wakati mwingine wamepauka; siyo kwamba hawapaki lotion wala mafuta, ni kwa sababu tu ya tatizo la maji. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba tuhakikishe katika Wizara hii, Mheshimiwa atupe majibu, ana mkakati gani wa kuhakikisha kwamba wanatumia vyanzo hivi vya maji ili kuhakikisha kwamba wanawatua ndoo mama zetu katika suala zima la maji. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lingine ambalo nilikuwa nataka nilizungumzie ni kuhusu suala zima la upanuzi wa Shule za Sekondari na Vyuo. Kumesababisha mahitaji makubwa ya ajira hususan kwa vijana wenzetu na tunatambua kabisa sasa hivi kumekuwa na ongezeko kubwa la vijana, lakini wamekuwa na changamoto kubwa ya kukosa ajira. Vijana wenye degree wanashinda maskani, hawana shughuli kubwa ya kufanya, lakini natambua shughuli kubwa anazozifanya mama yangu, Mheshimiwa Jenista Mhagama pamoja na kaka yangu Mheshimiwa Anthony Mavunde kuhakikisha kabisa vijana wetu wanapata mafunzo, lakini Serikali ione kabisa nia yake ya dhati namna gani tunaenda
kutatua tatizo la ajira katika Halmashauri zetu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, pia kuwe na mkakati maalum ambao kutatolewa tamko maalum kwa Halmashauri zilizokuwepo katika Wilaya zetu kuhakikisha kwamba inatengeneza ajira kila mwaka na kutoa taarifa Bungeni ili vijana wetu wenye elimu na wasio na elimu wawe wanapata fursa mbalimbali za ajira. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lingine, naomba Wizara ya ajira iangalie baadhi ya mashamba kuhusu wawekezaji hususan katika mashamba ya Mkonge. Katika Jimbo langu la Pangani tuna mashamba makubwa mawili kwa maana ya shamba la Mwera Estate na Sakura Estate lakini
Watanzania wale maskini ambao wanafanya katika uzalishaji mkubwa wa mikonge, wamekuwa wanapata tabu, wananyanyasika; mikataba yao imekuwa ya ujanja ujanja; hali duni; mazingira mabaya! Kwa hiyo, naiomba Wizara hii, hususan Mheshimiwa Jenista Mhagama apate nafasi ya kupita kule ili kuwapa faraja na waone kwamba na wao ni sehemu ya Tanzania, kwa sababu wamekuwa kama wapo katika ukoloni. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, naiomba Serikali kwa dhati kabisa iende katika maeneo yale ili wawekezaji wale wahakikishe kwamba wanawaboreshea maslahi na kutengeneza ajira ili waweze kunufaika. Wakati mwingine wanaweza kukwambia mkonge haulipi; sasa kama haulipi, kwa nini wasilime mihogo ambayo inaweza ikalipa? Kwa hiyo, unakuta ni ujanja tu wa wawekezaji lakini kubwa tunajua kabisa mkonge unalipa, lakini mkonge uendane na maslahi ya wale wafanyakazi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba pia niipongeze Serikali kuhusu suala zima la elimu bure, lakini pia itambue kuna baadhi ya maeneo katika nchi yetu ilichelewa kuwekeza katika suala zima la elimu. Katika Jimbo langu la Pangani, sisi mpaka mwaka 2005, tulikuwa na shule mbili tu za Serikali, lakini kwa jitihada ya Serikali kuhakikisha kwamba inatengeneza Shule za Kata, leo hata mimi mtoto wa Mama Ntilie nimefika katika Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Kwa hiyo, naipongeza kwa dhati kabisa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kubwa ni kwamba, tuna changamoto mbalimbali hususan ukosefu wa Walimu wa Sayansi. Naiomba Serikali, ili kuhakikisha katika bajeti hii na sisi tunapatiwa Walimu, sisi miaka ya nyuma katika Wilaya yetu ya Pangani tulikuwa tukiitwa KKY kwa maana ya
Kufuma, Kushona, Kupika na Kuzaa ndiyo kazi za watu wa Pangani na kukaa barazani. Kupitia Serikali hii, leo imeweza kuwezesha vijana mbalimbali katika nchi yetu, wameweza kushiriki.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, hilo ni jambo jema na tutaendelea kuliunga mkono, lakini kubwa tunaiomba Serikali iendelee kuhakikisha kwamba inaboresha miundombinu mizuri na kuhakikisha kwamba inatupatia Walimu wa Sayansi ili siku moja Mheshimiwa Dkt. John Pombe
Magufuli atokee katika Jimbo la Pangani. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, sina maneno mengi sana ya kusema, itoshe kusema kwamba naunga mkono hoja na naomba kuwasilisha. Ahsante sana.