Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Fedha za Ofisi ya Waziri Mkuu na taasisi zilizo chini yake pamoja na Mfuko wa Bunge kwa mwaka 2017/2018.

Hon. Edward Franz Mwalongo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Njombe Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Fedha za Ofisi ya Waziri Mkuu na taasisi zilizo chini yake pamoja na Mfuko wa Bunge kwa mwaka 2017/2018.

MHE. EDWARD F. MWALONGO: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi. Nami nachukua fursa hii kwanza kabisa kumpongeza Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa hotuba yake na Mawaziri wote waandamizi wenye Wizara hiyo. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, kwa kweli napenda nianze kabisa na suala la kilimo. Sisi kule Jimbo la Njombe Mjini ni wakulima na hatuna shughuli nyingine zaidi ya kilimo. Katika suala la kilimo nianze kabisa kwanza kwa kuipongeza Serikali na Waziri Mkuu mwenyewe binafsi, kwa kazi kubwa iliyofanyika kudhibiti lumbesa. Leo hii wananchi wa Njombe wanafurahia kilimo chao cha viazi kwa sababu lumbesa imedhibitiwa.
(Makofi)
Mheshimiwa Spika, kwa kuwa kiazi ni zao la msimu, naomba sana mikoa yote inayopokea viazi kutoka kwa wakulima wa viazi wa Mikoa ya Iringa, Njombe na Mbeya iendelee kudhibiti lumbesa katika masoko yao hasa hasa Mikoa ya Dar es Salaam, Dodoma, Ruvuma, Mtwara na
kadhalika, ili tuweze kusaidia wakulima ambao wanalima zao hili la viazi. Leo hii wanafurahia bei ni nzuri na lumbesa imedhibitiwa naipongeza sana Serikali kwa jitihada hizo.
Mheshimiwa Spika, kilimo ndicho kinachoajiri Watanzania walio wengi. Naiomba Serikali, tunayo kazi kubwa sana ya kufikiria namna gani tunaweza tukasaidia vijana wa nchi hii.
Mheshimiwa Spika, ningependa kuishauri Serikali sasa ianzishe makambi maalum ya kilimo kama mashamba darasa makubwa ambayo yataweza kusaidia kuwaweka vijana mahali ambapo pana miundombinu sahihi ya kilimo; kuna maji, makambi ya kuishi, mashine za kilimo ili vijijini vijana waende pale wafundishwe kilimo bora, walime wapate mitaji, halafu baada ya muda watakuwa wamefikia umri wa kuweza kujiendeleza. Warudi sehemu nyingine wakaendelee na shughuli za kilimo. Kuliko leo kuwahamasisha vijana waende wakalime. Vijana hawa
kwenda kulima kwa jembe la mkono kwa maendeleo haya tuliyofikia, hawawezi. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, tunaanzisha Vyuo vya VETA na katika bajeti iliyopita nilisema, vyuo hivi tunavyoanzisha maana yake nini? Tunahamisha vijana kutoka vijijini kupeleka mijini. Tukianzisha makambi maalum ya kilimo kwa vijana na tukawawekea miundombinu sahihi, tutawawezesha
vijana hawa kubaki vijijini na kujishughulisha na kilimo katika mazingira yaliyoboreshwa.
Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, naishauri Serikali sasa iangalie tunapojenga Vyuo vya VETA na tujenge makambi maalum ya kilimo yenye mashamba makubwa ili kusudi vijana waweze kufanya hizo kazi katika mazingira yaliyoboreshwa. Huo ndiyo ushauri ninaoweza kuutoa kwa
Serikali juu ya suala la kilimo.
Mheshimiwa Spika, suala lingine kwenye kilimo linalosumbua ni mbolea. Mbolea ni muhimu sana katika kilimo, lakini iko mbolea ya ruzuku. Naiomba sana Serikali iongeze kiwango cha ruzuku kwenye mbolea hii. Mbolea hii ina matatizo makubwa mawili; kwanza kiwango ni kidogo
sana, lakini pili inafika kwa kuchelewa.
Mheshimiwa Spika, katika Jimbo la Njombe Mjini mbolea inafika mwezi wa kwanza. Sisi Njombe tunapanda mwezi wa Kumi na Mbili mwanzoni. Sasa unapotuletea mbolea kupandia mwezi wa kwanza, maana yake sasa unasababisha hii mbolea iende katika mikono isiyo salama.
Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, naiomba sana Serikali iangalie, wataalam nafikiri wapo; ni nini kinachowashinda kujua kwamba mkoa fulani msimu wa kilimo ni huu; mkoafulani msimu wa kilimo ni huu; matokeo yake wanakulazimisha ununue mbegu mwezi wa kwanza. Utapeleka wapi mbegu mwezi wa kwanza wakati wewe umeshapanda mwezi wa Kumi na Moja mwishoni? Kwa hiyo, naiomba sana Serikali iangalie itoe ruzuku ya kutosha na ihakikishe kwamba inaleta ruzuku hii katika muda ambao ndiyo muda wa kilimo kweli.
Mheshimiwa Spika, kingine ni suala la udhibiti wa mbegu. Mbegu za mazao zinahitajika kudhibitiwa. Pale Njombe kuna taasisi ya udhibiti wa mbegu, ina wataalam saba, ina gari moja inadhibiti mbegu kanda nzima; na hiyo kanda ni Mkoa wa Ruvuma, Njombe, Iringa, Mbeya, Rukwa;
mikoa sita, gari moja; wataalam sita wanadhibiti mbegu. Ni jambo ambalo haliwezekani.
Mheshimiwa Spika, naiomba sana Serikali iangalie utaratibu mzuri wa kuhakikisha kwamba Kitengo hiki cha Udhibiti wa Mbegu na Ubora wa Mbegu kinapewa huduma inayotosha ili kusudi kiweza kutoa huduma.
Mheshimiwa Spika, vilevile hata sheria yake naomba iangaliwe, kwa sababu sheria ukikutwa na mbegu ambayo siyo mbegu halali, siyo mbegu safi, mbegu fake, faini yake ni ndogo sana. Kwa hiyo, mtu yuko tayari kuzalisha mbegu fake na kuuzia wakulima, kwa sababu anajua kwamba nikipigwa faini, itakuwa Shilingi bilioni 50 nami nimeshauza mbegu zaidi ya mabilioni ya pesa. Kwa hiyo, kwangu siyo tatizo.
Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, naiomba sana Serikali iangalie Sheria ya Udhibiti wa Mbegu na ikiwezeshe kitengo hiki pale Njombe. Hawana hata maabara, wala store ya kutunzia mbegu. Wametunza tu mbegu hovyo hovyo. Mbegu ikileta tatizo kwa mkulima ukirudi taasisi ya mbegu,
ukichukua ile sampuli ya mbegu ambayo ililetwa na mzalishaji wa mbegu, ilishaliwa na panya. Kwa hiyo, hilo ni tatizo kubwa sana. Naiomba sana Serikali ikiangalie kwa jicho la pekee kile Kitengo cha Udhibiti wa Mbegu pale Njombe.
Mheshimiwa Spika, nizungumzie suala lingine linalohusiana na mambo ya maliasili na hasa Kitengo hiki cha TFS. Sisi Njombe ni wazalishaji wakubwa sana wa mbao, miti, mijengo na makaa ya kupikia majumbani na kadhalika. Kitengo hiki hakijawa makini. Moja ya umakini ambao
nauona unaleta tatizo kwa kitengo hiki ni kwamba, kinaeleza Sheria ile ya Udhibiti wa Misitu na hasa suala la mkaa, kama vile nchi nzima tunafanana katika mazingira yetu. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, sisi Njombe tuna mazao ya misitu ya kupanda; tunalo zao la mti mmoja unaoitwa uoto au mlingo au muwati. Miti hii inapandwa kwa muda wa miaka mitatu mpaka minne inavunwa. Mazao yanayotoka hapo kwenye huo mti ni maganda ambayo yanachukuliwa
yanapelekwa viwandani kwa ajili ya ku-process mambo mengine huko viwandani. Vilevile matokeo mengine ni kuni, pia unaweza ukatengeneza mkaa. Sasa taasisi hii inasema kwamba mkaa sasa ni marufuku kuvuka Wilaya. Sisi Njombe milingo ni zao. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, nilidhani kwamba Tanzania Forest Service wanatakiwa waje Njombe walete nguvu za kutosha, wananchi wa Njombe wapande milingo mingi zaidi ili tufidie uzalishaji wa mkaa katika eneo lingine la nchi kusudi wananchi wengine waweze kupata mkaa. Huwezi kuzuia mkaa halafu hujaweka mbadala wa mkaa. Wananchi hawa watapikia nini; hasa wananchi kama wa miji mikubwa? Njombe kuna fursa ya kuzalisha hii miti. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, naomba niombe TFS waje Njombe tushirikiane tuzalishe miti mingi, tuzalishe mkaa, wananchi katika nchi hii waendelee kutumia mkaa wakati tukiendelea kutafuta nguvu nyingine ya matumizi ya kupikia na kadhalika.
Mheshimiwa Spika, vilevile wanaleta marufuku nyingine ambazo zinaleta kero kweli kwa wananchi. Wanasema ni marufuku kupakia mazao ya misitu kwenye pikipiki. Hivi hawa watu wa TFS wanaelewa maana ya mazao ya msitu? Maana yake kuna korosho humo ndani, ni marufuku
kupakia korosho kwenye pikipiki. Kuna kuni, ni marufuku kupakia kuni kwenye pikipiki; kuna mkaa. Sisi hatuharibu sana mazingira kwa maana ya kwamba tunatumia miti ya asili.
Kwa hiyo, wanapotoa hizi sheria au maelekezo naomba sana Serikali iangalie hii taasisi iweze kutoa maelekezo ambayo hayasababishi kero kwa wananchi. Unapotoa maelekezo kama haya kwamba ni marufuku kupakia mkaa au kuni kwenye pikipiki matokeo yake ni kwamba anapokuja Afisa mwingine wa Serikali, yeye anasema hii ni sheria, huruhusiwi kupakia mkaa kwenye pikipiki. Kwa hiyo, wananchi wananyanyasika kwa sababu tu hawa TFS wanatoa maelekezo ya jumla kwa nchi nzima. Mimi kama mwakilishi wa wananchi wa Jimbo la Njombe Mjini, siwezi kukubaliana kabisa na hili jambo, naiomba kabisa Serikali iweze kuwapa maelekezo ya kutosha.
Mheshimiwa Spika, kingine, kuna kitu kinaitwa TP (Transit Pass). Naomba sana Serikali itusaidie sisi watu wa Njombe. Sisi ndio tunaozalisha mbao, miti, mijengo na kadhalika. Tukisafirisha mabanzi tu ndani ya Halmashauri ya Njombe, tunatozwa kitu kinaitwa Transit Pass. Sasa manufaa ya sisi kuwa na misitu ni nini? Tunapanda ile miti kwa jasho letu, tunazalisha miti kwa ajili ya wananchi wote, mbao na kadhalika; tukikutwa tu tumepakia kuni kwenye gari, pickup tani moja; Tanzania Forest Service wanataka tuwe na TP. Naomba Serikali iangalie tuweze kuondolewa TP wananchi wa Njombe ili kusudi tuendelee kuzalisha zaidi misitu, kwa sababu misitu tunayozalisha pale ndiyo inawasaidia
wananchi wote.
Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi, naunga mkono hoja ya Waziri Mkuu, ahsante sana.