Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Masuala ya UKIMWI na Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii kwa Kipindi cha Januari, 2016 hadi Januari, 2017

Hon. Ummy Ally Mwalimu

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Tanga Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Masuala ya UKIMWI na Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii kwa Kipindi cha Januari, 2016 hadi Januari, 2017

WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nami jianze kwa kuishukuru Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii kwa Taarifa yao, lakini nawashukuru kwa ushauri na maoni ambayo wamekuwa wakitupatia mara kwa mara katika kuboresha utendaji wa Wizara.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika hatua hii niseme kwamba Wizara yangu inapokea maoni na ushauri wa Kamati kama walivyoyawasilisha hapa na ninaahidi kwamba tutayafanyia kazi masuala yote waliyoyabainisha.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, napenda kutoa ufafanuzi katika masuala makuu matatu kama muda utatosha na suala la kwanza ni kuhusu hali ya upatikanaji wa dawa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, changamoto kubwa ya upatikanaji wa dawa nchini ilikuwa inasababishwa na upatikanaji wa fedha, lakini hivi ninavyosema tumetoka katika kutaja bajeti ya Afya ya shilingi bilioni 251 na kusema pesa ambazo Wizara ya Afya imepokea; mpaka sasa hivi tumepokea shilingi bilioni 91 kwa ajili ya kununua dawa, vifaa na vifaa tiba.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tukiangalia mwaka 2016 MSD ilipokea shilingi bilioni 24 tu kwa mwaka mzima kwa ajili ya kununua dawa. Sasa hivi kila mwezi Wizara ya Fedha inatuletea shilingi bilioni 20. Tumetoka kwenye kupokea shilingi bilioni mbili kila mwezi tunapokea shilingi bilioni 20 kila mwezi kwa ajili ya dawa. Kwa hiyo, baada ya kuwa tunapata fedha, hali ya dawa kwa kiasi kikubwa inazidi kuimarika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, labda niseme tunapimaje upatikanaji wa dawa? Tunaangalia upatikanaji wa dawa katika Bohari Kuu ya Dawa. Hivi sasa MSD ana aina za dawa 105 kati ya dawa 135 muhimu za kuokoa maisha. Hii ni sawa na 78%. Nakiri kwamba sasa hivi kazi inayoendelea ni kuhakikisha dawa hizi sasa zinashuka katika zahanati zetu na vituo vya afya.
Waheshimiwa Wabunge, nimewaandikia barua na kesho mtaipata kuainisha mchanganuo wa kila fedha ya dawa ambayo tumebajeti katika Halmashauri yako ili uweze kupima. Kubwa tunawaomba msimamie matumizi ya fedha za dawa na matumizi ya dawa. Hali ya upatikanaji wa dawa kama wote hatutaimarisha Kamati za Vituo, basi hatutaweza kuwa na upatikanaji wa dawa hasa katika ngazi za chini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia naomba nitoe angalizo, hatuwezi kuwa na upatikanaji wa dawa kwa asilimia 100 kwa sababu ya ongezeko la watu kila siku, ongezeko la magonjwa na vituo. Kwa hiyo, kubwa ambalo Wizara ya Afya tunalifanya sasa hivi ni kujikita kwenye kinga badala ya tiba. Maana inakuwa ni Taifa la kujikita kwenye tiba badala ya kinga.
Mheshimiwa Mwenyekiti, changamoto nyingine ambayo tumeibaini ni MSD anabajeti fedha ya kununua dawa kutoka kwenye Fungu 52 - Wizara ya Afya, lakini kuna fedha za Mfuko wa Pamoja wa Afya, kuna vyanzo vya makusanyo tumeomba wenzetu wa TAMISEMI, maana MSD ananunua dawa za wateja za shilingi bilioni 70, lakini wateja wake wana fedha za kununua dawa za shilingi bilioni 300. Kwa hiyo, haiwezekani MSD kuweza kutosheleza soko lake. Nawaahidi Waheshimiwa Wabunge kwamba tutafanyia kazi suala hili la kuhakikisha dawa zinafika kwa wananchi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la kwamba MSD ipewe fungu, tulipokea ushauri wa Kamati na tukamwandikia Waziri anayehusika na masuala ya Utumishi na Utawala Bora kwa sababu wao ndio wanatoa Vote. Wakatushauri tuombe line item. Sasa hivi tuna line item katika Bajeti ya Wizara ya Afya kwa ajili ya MSD.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu suala la Halmashauri ambazo zinadaiwa fedha na MSD ziruhusiwe zilipe kidogo kidogo; tumepokea pia ushauri wa Kamati. Sasa hivi katika ile fedha ambayo tunaingiza katika bajeti ya Halmshauri, tunakata asilimia 25 tu, asilimia 75 tunawapa kwa ajili ya kusaidia upatikanaji wa dawa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu deni la MSD, mpaka sasa hivi tumelipa shilingi bilioni 11, lakini tumeona chanzo kinachofanya deni hili likawa kubwa ni tozo. Kwa hiyo, tayari tumewaelekeza tupitie tozo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la pili ni Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya. Kamati inashauri kwamba i-cover magonjwa yote. Nataka kuwathibitishia Waheshimiwa Wabunge kwamba kuanzia mwezi Septemba tumeingiza kitita cha huduma za upasuaji wa moyo na matibabu mengine ya hali ya juu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu NHIF kusimamia kuweza kutumika Bima zao mpaka nchi za Afrika Mashariki, sheria iliyoanzisha NHIF inaruhusu NHIF kufanya kazi ndani ya nchi. Tumepokea ushauri na tutaleta. Waheshimiwa Wabunge ni mapendekezo yenu, tutayaleta hapa ili NHIF itumike ndani ya nchi za Afrika Mashariki, nasi tuko tayari na ninaamini kwamba Muswada huu mtaweza kuupitisha.
Mheshimiwa Mwenyekiti,…
(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)
MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa Waziri.
WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nimalize neno moja tu. Kuhusu uzazi wa mpango, nakubaliana na ushauri wa Kamati kwamba ni changamoto kubwa, Waheshimiwa Wabunge mtuunge mkono. Ni asilimia 32 tu ya wanawake wanaotumia uzazi wa mpango. Lengo letu ni kuhakikisha huduma hizi zinapatikana mitaani badala tu ya kwenye vituo vya afya na hospitali.
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la uzazi salama ni kipaumbele chetu. Nawathibitishia Waheshimiwa Wabunge, nikiwa Waziri mwanamke na mama wa watoto wawili, tutasaidiana kupunguza vifo vya akina mama. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana na ninawashukuru sana Waheshimiwa Wabunge.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru na ahsante kwa kunipa nafasi. Nianze kwa kuishukuru sana Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Maendeleo ya Jamii kwa jinsi ambavyo wameandika ripoti yao vizuri na ushirikiano wanaotupa katika kufanya na kutimiza majukumu yetu. Niwahakikishie kwamba mapendekezo yao mazuri sana waliyoyatoa kwenye ripoti yao tutayafanyia kazi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naungana na Mheshimiwa Kadutu kuwapongeza sana Serengeti Boys kwa mafanikio makubwa waliyoyapata na kuipa heshima nchi yetu kwa kufanikiwa kwenda kwenye fainali za Afrika kwa vijana chini ya umri wa miaka 17. Niwahakikishie tu Waheshimiwa Wabunge kwamba hata kufika pale walipofika kuna mkono mkubwa sana wa Serikali. Wakati mwingine siyo kila jambo unalisema hadharani, lakini ni hakika kwamba mkono wa Serikali umesaidia wao kucheza na kufika pale walipofika, lakini pia kusukuma rufaa yao mpaka wakapata kushinda na kwenda kwenye fainali za mashindano haya. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, niwahakikishie Watanzania kwa pamoja, bila kujali tofauti zetu tuungane kwa pamoja, tuwatie moyo vijana hawa na kuwasaidia. Tunaamini watafanya vizuri kwenye mashindano haya na bila shaka tunaweza tukarudi na kombe. Wakifika nusu fainali, basi tuna uhakika wa kwenda kwenye Kombe la Dunia la Vijana chini ya miaka 17. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na maelezo mazuri ya Kamati na wameainisha humu changamoto ambazo zinaikabili sekta ya michezo, niseme tu moja ya eneo kubwa ambalo linatusumbua sana ni namna ya ku-finance michezo katika nchi yetu. Niahidi katika Bunge hili kwamba tutaleta hapa Bungeni mpango mahsusi wa ku-finance michezo katika nchi yetu na hili litakuwa jibu la tatizo hili la kuendelea kwa michezo katika nchi yetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunapitia Sera ya Michezo kama walivyoeleza katika taarifa yao na baada ya muda sera hii itakamilika, iko katika michakato ya mwisho. Ikikamilika, tutaleta sheria na kanuni zake hapa na bila shaka itasaidia sana katika ukuaji wa sekta ya michezo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, moja la mwisho ambalo nilipenda nilizungumzie ni suala la usikivu na utendaji kazi wa Shirika la Utangazaji la Taifa. Ni kweli kama ilivyooneshwa kwenye ripoti ya Kamati, Wilaya 81 za nchi yetu TBC haisikiki kabisa. Waheshimiwa Wabunge, tukumbuke wakati fulani TBC ilikuwa inasikika nchi nzima wakati tukitumia teknolojia ya zamani. Bahati mbaya wakati wa mabadiliko haya ya teknolojia mpya, vifaa vingi vile vya zamani sasa havifanyi kazi tena na uwekezaji ulikuwa haujafanyika wa kutosha na ndiyo maana ukweli ni huo kwamba nusu ya nchi yetu inasikika na nusu ya nchi yetu haisikiki. Sasa kwa Shirika la Utangazaji la Taifa kusikika nusu ya nchi, nadhani ni tatizo kubwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nilihakikishie Bunge lako kwamba bajeti ijayo nadhani tutafanikiwa kuleta hapa mpango wa kupata fedha za kutosha wa ku-finance TBC. Uwekezaji mkubwa unahitajika ili kusaidia katika teknolojia, lakini pia kuboresha studio zao na vipindi vyao. Nina hakika Bunge hili likituunga mkono tutakapoleta mapendekezo hayo tutapata pesa za kutosha na tutaliondoa Shirika letu la Utangazaji pale lilipo na ndoto zetu kwamba liwe shirika bora kabisa katika nchi yetu. Inahitajika uwekezaji mkubwa, naamini Bunge litatuunga mkono wakati utakapofika na tutakapoleta hapa wakituunga mkono, tunaamini Watanzania watafurahia huduma nzuri na kazi nzuri ya Shirika la Utangazaji la Taifa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimalizie kwa kuunga mkono mapendekezo mengi yaliyoletwa na Kamati ya Kudumu ya Bunge. Nakushukuru sana kwa nafasi uliyonipa. Ahsante sana.