Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Masuala ya UKIMWI na Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii kwa Kipindi cha Januari, 2016 hadi Januari, 2017

Hon. John Peter Kadutu

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ulyankulu

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Masuala ya UKIMWI na Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii kwa Kipindi cha Januari, 2016 hadi Januari, 2017

MHE. JOHN P. KADUTU: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru kunipa fursa hii ya kuchangia jioni hii kwa ajili ya ripoti ya Kamati zetu hizi mbili, Kamati ya Kudumu ya masuala ya UKIMWI pamoja na Huduma na Maendeleo ya Jamii. Nizipongeze sana Kamati hizi mbili kwa kuja na taarifa ambayo inatupa mwanga nini kinaendelea kwenye Kamati hizi lakini ndani ya Serikali pia.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba mimi nichangie eneo ambalo nadhani ndani ya Bunge humu leo au siku mbili, tatu halijazungumzwa. Kwa niaba ya wanamichezo wote tuipongeze timu ya Serengeti Boys kwa kufaulu rufaa yake na sasa itashiriki fainali za under 17 kule Cameroon. Fainali hizi zilikuwa zifanyike Madagascar na sasa zitafanyika Cameroon. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka kutoa ushauri kwa Serikali na bahati nzuri mdogo wangu Mheshimiwa Nape yupo, ni vyema yakafanyiwa kazi haya tunayosema. Tumekuwa watu wa kufurahia matokeo. Tunapokuwa na matokeo mazuri kila mmoja anafurahia. Juzi tulipopata taarifa ya Serengeti Boys kufaulu kwenda kucheza fainali tumepongezana sana, lakini hatufikirii maandalizi sasa ya michuano hii. Ni juu ya Serikali kuanza kuona ni namna gani inaweza kuweka mkono wake.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka 1980 kwa wale mliokuwepo, Serikali yetu ilikuwa bado ina matatizo ya uchumi. Tutakumbuka tulikuwa tumetoka kwenye vita ya Uganda ya Nduli Iddi Amin, uchumi wetu ulikuwa umeparaganyika sana na Mwalimu alikuwa ametupa miezi 18 ya kufunga mkanda.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, Serikali ya Mwalimu ambaye tulidhani labda hapendi michezo, ilitia mkono wake tukafika Lagos kwa ajili ya AFCON, wakati ule tunaita fainali za nchi huru za Afrika. Hata matokeo tunayoyaona ya Cameroon, Ghana na nchi nyingine hazipati matokeo mazuri tu kwa kuachia vyama vya mpira, Serikali lazima iweke mkono wake.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, mimi nashauri, tuanze sasa. Mheshimiwa Nape wakati wa bajeti lete mapendekezo hapa tuone kama yatakwama. Tupo Wabunge tuta-support ili Serikali itie mkono wake isiwe Serikali ya kusubiri matokeo mazuri. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nitawapa mfano, mwaka 2014 mimi niliongoza msafara kwenda Brazil na kikosi cha watoto wanaoishi katika mazingira magumu kwenye World Cup. Mashindano hayo huwa yanatangulia World Cup yenyewe. Tulikwenda na tukachukua ubingwa wa dunia na tukakaribishwa hapa Bungeni, Waziri Mkuu wakati ule alikuwa Mzee Pinda, Serikali ikatoa ahadi nyingi tu mpaka leo hata ahadi moja haijatekelezwa. Sasa tunaanza kujiandaa kwa kombe la dunia lingine mwaka kesho. Mwaka kesho ni World Cup, sisi tutatangulia kwenda Urusi na timu ile kwenda kutetea ubingwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tuiombe Serikali basi itie mkono pale tutakapohitaji msaada hata nauli. Maana yake tunagharamia wenyewe, tunakuja na kikombe tunafurahia wote kwa pamoja. Iko haja ya Serikai kuliona hilo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kama kweli tunataka kushinda, tunataka kwenda kufanya vizuri kule Cameroon na watoto hawa wa under 17…..
(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru na naunga mkono hoja, ahsante.