Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Masuala ya UKIMWI na Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii kwa Kipindi cha Januari, 2016 hadi Januari, 2017

Hon. Pascal Yohana Haonga

Sex

Male

Party

CHADEMA

Constituent

Mbozi

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Masuala ya UKIMWI na Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii kwa Kipindi cha Januari, 2016 hadi Januari, 2017

MHE. PASCAL Y. HAONGA: Mheshimiwa Mwenyekiti na mimi naomba nichangie, lakini naomba nianze kwa kusema kwamba taarifa hii ya Kamati, vitu vingi wamezungumza kusema ule ukweli kabisa vitu ambavyo ni vya ukweli japo kuna baadhi ya vitu naona kwamba kidogo kuna shida.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika taarifa hii ukurasa wa nane, wamegusia Bodi ya Mikopo ya Elimu ya Juu na Waziri wa Elimu yuko hapa. Miongoni mwa vitu ambavyo Mheshimiwa Waziri vitakuja kukuondoa siku za hivi karibuni nadhani ni Bodi ya Mikopo ya Elimu ya Juu. Mheshimiwa Waziri kusema ule ukweli kabisa ameshawahi kuzungumza na ndugu yangu Heche hapa Bungeni, ulipokuwa Baraza la mitihani pale ulikuwa na heshima kubwa sana Mheshimiwa Waziri lakini leo umeletwa kuwa Waziri wa Elimu kwa kweli to be honestly heshima yako imeshuka sana kutokana na yale ambayo yanaendelea katika Taifa hili hasa kwenye elimu yetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, leo wale watoto wetu ambao walikuwa wanadahiliwa siku za nyuma kwa mfano mwaka 2014/2015 walidahiliwa wanafunzi 58,000 na TCU; lakini waliopata mikopo ni zaidi ya 40,000 zaidi ya nusu ya wanafunzi walipata mikopo. 2016/2017, wamedahiliwa wanafunzi 58,000 waliopata mkopo ni wanafunzi 20,000. Ukiangalia Awamu ya Nne walifanya vizuri zaidi katika suala hili la kutoa mikopo kwenye elimu ya juu lakini Awamu ya Tano ime-prove failure kabisa na Mheshimiwa Ndalichako hili unatakiwa ujipime, ujitathmini uone kama unatosha kuendelea kuiongoza Wizara hii. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kusema ule ukweli wako wanafunzi ambao walikuwa wanaendelea na masomo, wameshakopeshwa, yupo mwaka wa pili, mwaka wa tatu leo unasema kwamba hana sifa, unamuondoa kwenye mkopo. Sijajua vizuri kama hizi ni akili au ni matope lakini najua kabisa kwamba ni Serikali ambayo haipo makini kabisa katika kuhakikisha kwamba wanaboresha elimu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kusema ukweli kabisa kwenye hii mikopo wapo wanafunzi ambao wanadai haki baada ya kuona mikopo imecheleweshwa, wanapokuwa wanadai haki wanafunzi hawa wanafukuzwa chuo, wanaonekana kwamba ni wakorofi, hawafai kuendelea kusoma. Kuna mwanafunzi mmoja anaitwa Alphonce Lusako, huyu kijana amefukuzwa chuo mwaka 2011 kwa sababu alikuwa anadai fedha za wale ambao wamecheleweshewa mkopo mwaka 2011, kijana huyu amerudishwa chuoni mwaka jana 2016, lakini mwaka huu 2017 amefukuzwa tena kwa sababu ya kudai haki ya wanafunzi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri leo ulitakiwa uwe wa kwanza kuondolewa kwenye nafasi yako kuliko kusimamisha wanafunzi wanaodai mkopo, chanzo cha kudai mkopo ni kwa sababu ninyi mnachelewesha, mikopo yenyewe haitoshi, wanapokuwa wanadai haki mnawafukuza badala ya kwamba Serikali iweze kuwajibika.(Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Bodi ya Elimu ya Juu kwa kweli hapa lazima iondoke na watu, kama Taifa tuweze kujitathmini upya tuangalie ni akina nani wanaweza wakaongoza. Naomba niseme tu kwamba yapo mambo mengi na madudu mengi sana kwenye Bodi ya Elimu ya Juu wamezungumza wengi sitaki nirudie sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie suala lingine japokuwa kuna mmoja amesema suala hili la TAMISEMI ni kweli kabisa. Kuna mambo ya TAMISEMI na kuna mambo mengine ya Wizara ya Elimu, lakini mambo haya ni kama mapacha yanaenda pamoja. Leo watoto wetu wanafeli kwa sababu walimu walishakata tamaa. Leo walimu wanaidai Serikali fedha nyingi sana. Serikali inawaambia walimu kwamba asiyetaka kazi aache. Ni kweli walimu wengi leo wameacha kazi wamebaki na utumishi. Kilichotufikisha leo hapa ni kwa sababu ya walimu kukata tamaa na ndiyo maana mmoja ametoa takwimu hapa shule za binafsi zinafanya vizuri kwa sababu kule hakuna madai. Shule zetu za Serikali, hizi za umma zinafanya hovyo kwa sababu walimu wetu tunawakatisha tamaa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, leo ukiangalia kwa mfano Mkoa wa Songwe madai zaidi ya shilingi bilioni mbili hayajalipwa kwa walimu wetu, Wilaya ya Momba, Wilaya ya Mbozi na Wilaya ya Ileje, shilingi bilioni mbili hawajalipwa. Waziri ninaomba katika hili tafadhali muweze kuliangalia muone kama mnaenda sawasawa.
MWENYEKITI: Ahsante, Mheshimiwa Haonga muda wako umeisha.
MHE. PASCAL Y. HAONGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la mwisho ni kuhusu TBC..
Mheshimiwa Mwenyekiti, TBC tunailipia kodi zetu lakini inatangaza habari za Chama cha Mapinduzi.