Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Masuala ya UKIMWI na Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii kwa Kipindi cha Januari, 2016 hadi Januari, 2017

Hon. Edward Franz Mwalongo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Njombe Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Masuala ya UKIMWI na Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii kwa Kipindi cha Januari, 2016 hadi Januari, 2017

MHE. EDWARD F. MWALONGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi niweze kuchangia kwa Kamati ambazo zimewasilishwa mbele yetu leo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze na suala la elimu. Kwanza kabisa niwaondoe wasiwasi Waheshimiwa Wabunge wenzangu na tuipongeze Serikali yetu kwamba mfumo wetu wa elimu ni mzuri sana, mfumo wa elimu ni mzuri sana. Tatizo kubwa tulilonalo ni jinsi ya kuusimamia, hapo ndipo shida inapoanzia kwamba uwezo wetu wa kuusimamia mfumo mzuri huu uko chini mno, hatuwezi kabisa kuusimamia huu mfumo. Kwa hiyo, sasa kinachokuja kutokea baadaye ndio maana tunapata matokeo mabaya. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano watu wanalalamika kusema watoto ujasiriamali, watu wanatoka wanamaliza mpaka vyuo vikuu hawawezi kujitegemea, sio kweli. Wasioweza kujitegemea baada ya kumaliza elimu hizi katika mfumo tulionao ni kwamba wao wenyewe tu hawako tayari kujituma, kwa sababu wanalazimisha kufanya vitu ambavyo wamesomea vilevile tu kama yeye amesoma degree ya sheria analazimisha akawe mwanasheria, lakini tunachosema kwenye elimu maana yake umepanua maarifa, licha ya kufanya hiyo taaluma maalum uliyosomea, lakini maarifa uliyapata, njia nzima uliyopita yanakuwezesha kuishi maisha mengine. Kwa hiyo, kila msomi anapaswa kuongeza akili ili aweze kutumia maarifa aliyopata.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mfumo huu wa elimu ambao sasa tumeanza tunaita elimu msingi lipo jambo ambalo naiomba sana Serikali iangalie na ijaribu kutoa taarifa za mara kwa mara na kuna wakati nilishauri hapa kwamba kingekuwepo chombo fulani kinachoweza kuzungumza mara kwa mara juu ya hii elimu msingi; kwa sababu katika elimu msingi ifikapo mwaka 2021 itakuwa kwamba kidato cha kwanza kutakuwa na mikondo miwili, maana yake kutakuwa na wale walioishia darasa la saba na kutakuwa na wale walioishia darasa la sita na hawa wote wanaenda kusomea shule hiyo hiyo ya sekondari.
Mheshimiwa Mwenyekiti, leo hii ukiwauliza wataalam wa elimu wanasema kwa sababu tumefikia asilimia 75 ya ku-recruit watoto wote shuleni. Definetly watakapokuja hao wengine na wenyewe wataingia kwenye mfumo huo, lakini miundombinu tuliyonayo kwenye shule zetu za sekondari bado ni kidogo mno, hatuna madarasa ya kutosha, maabara zile hazitakaa zitoshe kama ni ma-hall au mabwalo yatakuwa hayatoshi. Lakini vilevile shule nyingi mpaka leo bado zinajengwa mpaka leo bado zinajengwa; shule nyingi hazina madarasa, misalani ya kutosha na miundombinu chungu mzima ambayo inatakiwa watoto hawa iwatosheleze. Sasa tunaenda na huu mfumo wa elimu msingi ambao watoto wote sasa kufikia mwaka 2021 wote watakuwa wanaendelea na sekondari bila kuwabakiza au bila kuchagua pale katikati.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ni muhimu sana serikali ikaona ni namna gani itajipanga vizuri. Niipongeze imejaribu kuwaelimisha walimu, tumeona; pamoja na changamoto zilizokuwepo za walimu kufanya migomo hawapati posho za kutosha na nini kwenye yale mafunzo ya kuwapa hii elimu msingi, lakini angalau mmeliona hilo na katika sera mpya ya elimu mnajaribu kulifanyia kazi. Lakini kazi iliyobaki sasa ni kufanya maandalizi ya kutosha kuandaa, miundombinu ya kutosha na kuelimisha wananchi kwasababu watoto wale na wazazi hawaelewi mpaka sasa kama wataishia darasa la sita; ni vizuri sasa wakaelimishwa wakajiweka tayari kwamba tunaishia darasa la sita halafu tunaendelea na kidato cha kwanza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kingine ni kwamba Wizara ya elimu iache mikanganyiko; wapo maafisa kwenye Wizara ya Elimu wakiulizwa na wenyewe hawajui. Mahali kama Wizara ya Elimu na TAMISEMI ndipo tunapotegemea tupate majibu sahihi, wananchi wanapouliza maswali kama haya ya elimu msingi ni lazima watumishi na watendaji katika Wizara ya Elimu na TAMISEMI wawe na majibu sahihi. Kwa hiyo, nafikiri pamoja na hii sera ya elimu msingi ni vizuri sasa Wizara ya Elimu ikatengeneza hata vipeperushi tu kutoa hii elimu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ni kuwa ipo Idara ya Ukaguzi ambayo ni idara ya udhibiti wa elimu; idara hii hatujaitendea haki; kwanza haina vitendea kazi na pili ina wakaguzi wachache sana. Sasa katika kuendesha elimu ndipo tunaposema mfumo wetu ndio wenye matatizo, kwenye elimu kuna mtaala, udhibiti ubora halafu kuna Baraza la Mitihani kwa ajili ya kutoa mitihani. Hawa wanaodhibiti ubora wao ndio wanaosimamia kuona mitaala inatekelezwa vilivyo? Halafu Baraza la Mitihani kazi yake ni kuleta mtihani na kufanyisha mitihani. Sasa unakuta kwamba hii Idara ya Ukaguzi haifanyi chochote na matokeo yake ni kwamba hawa wanaosimamia mitaala kwa maana ya walimu, shule na wanafunzi wenyewe wanaosoma halafu wanakuja baraza wanatoa mtihani.
Sasa naomba Serikali iangalie itafanyaje kuwezesha hii Idara ya Udhibiti Ubora kweli iwe Idara ya Udhibiti Ubora, kinyume chake idara hii kama isipopewa vitendea kazi, wasipokuwepo wakaguzi wa kutosha haina uwezo wa kusimamia elimu yetu. Kwa hiyo, mapungufu mengi tunayoyaona yapo kwenye hii Idara ya Udhibiti Ubora.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nikiacha suala la elimu, nije kwenye suala la afya. Suala la afya yapo matatizo sio makubwa sana lakini ningependa niyasemee kidogo kwamba ipo shida ya tiba kwa watoto, huduma ya bure kwa watoto, wazee na akinamama wajawazito. Huduma hizi zinapotolewa zinaingiza gharama na wanaoingia gharama ni wale wanaosimamia ile hospitali kama ni Halmashauri ndio inaingia gharama. Sasa utaratibu wa Serikali kurejesha zile gharama ambazo Halmasahauri zimeingia upo chini sana. Kwa hiyo, niombe sana Serikali ione ilete zile fedha ambazo Halmashauri zimeingia gharama kutoa huduma kwa watoto, wazee na wajawazito.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini jambo lingine ambalo ningependa kuishauri Serikali itusaidie linaweza likawa ni la kwenye Halmashauri lakini tamko la Serikali lingeweza kutusaidia; matumizi ya magari ya wagonjwa. Mara nyingi sana tumeona magari ya wagonjwa ndio yanatumika kusafirishia wafu, sasa ni kinyume kabisa cha utaratibu yaani haiwezekani Halmashauri ina ambulance moja halafu ambulance hiyo hiyo bahati mbaya mtumishi amefariki inaondoka inaenda kilometa 800 kusafirisha mwili wa mtumishi aliyefariki, halafu Halamsahuri inabaki bila gari la mgonjwa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ningeomba sana tamko la Serikali litolewe kwamba magari ya wagonjwayatumike kubebea wagonjwa, iwe ni bahati mbaya tu huyo ndugu yetu tunayemsafirisha kama mgonjwa amefariki ndio tunaweza kusema gari hiyo itumike kumrudisha alipotoka. Lakini kutumia gari la wagonjwa kwa lengo la kumpeleka marehemu kumsitiri hii sio sawa na wala sio sahihi kwa sababu inaacha pengo halafu Halmashauri inabaki haina gari la wagonjwa. Ningeomba sana Serikali ione hili na iweze kulikemea.
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingineā€¦
(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)
MHE. EDWARD F. MWALONGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante naunga mkono hoja za Kamati kama zilivyowasilishwa.