Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara na Mazingira na Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji na Mitaji ya Umma kwa Kipindi cha Januari, 2016 hadi Januari, 2017

Hon. Omary Tebweta Mgumba

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Morogoro Kusini Mashariki

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara na Mazingira na Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji na Mitaji ya Umma kwa Kipindi cha Januari, 2016 hadi Januari, 2017

MHE. OMARY T. MGUMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana nami kupata fursa ya kuchangia Kamati hizi mbili.
Mheshimiwa Mwenyekiti, la kwanza nitoe shukrani kwa Mwenyezi Mungu aliyetupa afya na uzima hata tumekutana jioni hii ya leo. Lakini pili, nikushukuru wewe kwa kunipa nafasi hii na mimi kuchangia.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kwanza nichukue fursa hii kuipongeza sana Serikali ya Awamu ya Tano kwa sera yake ya viwanda na kwa kuanza kwa vitendo, natoa mfano kwenye jimbo langu. Mwaka wa jana wakati nakuja hapa watu wengi majirani zangu hapa walikuwa wananiambia kwamba Mgumba Mkulazi, lakini kilio kile kimemfikia Dkt. John Pombe Magufuli, ameweka mazingira mazuri na tumepata mwekezaji, Mkulazi Holding Company Limited, kampuni tanzu ya Mifuko ya Jamii ya NSSF na PPF inawekeza kiwanda kikubwa cha uzalishaji wa sukari katika Jimbo letu la Morogoro Kusini Mashariki, chenye uwezo wa kuzalisha tani 150,000 kwa mwaka na kuondoa adha ya sukari hapa nchini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naipongeza sana Serikali yetu ya Chama cha Mapinduzi kwa kwenda kwa vitendo utekelezaji wa sera ya viwanda. Haya sio maneno, kama mtu anabisha aje kule Mkulazi anaona ujenzi unavyoanza mara moja. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya utangulizi huo sasa niende moja kwa moja kwenye ushauri. La kwanza, naomba kuishauri Serikali hasa kwenye suala hili la TFA (Shirika la Mbolea) na kama walivyosema Kamati, suala kubwa hili shirika ni muhimu sana hasa kwenye sekta ya kilimo. Hili shirika ndio tunalitegemea kwa ajili ya usambazaji wa mbolea kwenye zana za kilimo, lakini kama Serikali haiwezi kulilea vizuri lazima madeni haya yataendelea kuongezeka na shirika hili litakufa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, niiombe tu Serikali, leo hii kwa mujibu wa Taarifa ya Kamati, shirika hili lilianza na mtaji wa shilingi bilioni 17.9 leo wana mtaji wa negative billion 12.3.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hii maana yake nini na sababu ni nini? Ni kwa sababu, mara nyingi Serikali, hasa kwenye taasisi zake hasa inapopata huduma kwenye ulipaji au fidia ya ile ruzuku ambayo inaagiza taasisi zake itumie inachelewa kwa muda mrefu sana, athari yake inakuwa kubwa na matokeo yake haya mashirika yanapoteza uaminifu kwa wadau na taasisi nyingine za fedha, hata kwa wasambazaji wengine wa mbolea kule wanakochukulia mbolea hizi na matokeo yake wanashindwa kukopesheka, athari kubwa inaenda kwa wakulima wetu kutokupata mbolea kwa wakati. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa niishauri Serikali inapohitaji huduma kwenye shirika lake, kwa mfano kama hapa, shirika hili linaweza kwenda kununua mfuko labda wa mbolea shilingi 50,000 lakini Serikali kwa ajili ya kurahisisha ipatikane kwa bei nafuu, ikaiambia TFC uzeni shilingi 30,000 nyingine ni ruzuku. Sasa ile ruzuku ambayo Serikali ina top up ni vizuri ikaipeleka kwa wakati ili kufidia shirika liweze kujiendesha kibiashara na ziweze kulipa madeni yake kule ambako inakopa. Badala ya kutoa miongozo kwamba toeni ruzuku, shirika linatoa ruzuku, lakini hela haziendi kwa wakati, ndio matatizo haya ya negative ya mtaji yanapatikana. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini la pili niishauri Serikali kuhusu kwenye Bodi za Mazao. Bodi za Mazao zimekuwa nyingi na mara nyingi tunavyoziona nyingine hazipo kwa ajili ya manufaa ya kilimo chetu wala kwa wakulima wa Tanzania. Sasa ushauri wangu kwa Serikali, ni vizuri tukaunda bodi mbili tu, moja ikawa kwa ajili ya mazao ya biashara ambayo itasimamia mazao yote ya biashara yale makubwa yaliyokuwa na bodi kwa sasa; kwa mfano labda ile Bodi ya Korosho, Bodi ya Kahawa, Bodi ya Pareto, Bodi ya Pamba, zote zikaunganishwa zikawa bodi moja na bodi ya pili ikawa Bodi ya Mazao Mchanganyiko. Hizi zikiwa mbili itakuwa ni rahisi, moja inashughulikia mazao mchanganyiko nyingine mazao ya biashara, kwa kufanya hivyo hata menejimenti yake inakuwa ni rahisi zaidi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, la tatu ni kuhusu Mifuko ya Jamii. Katika hili nakubaliana na mapendekezo ya Kamati, wanapozungumza kwamba Msajili wa Hazina (TR) anatakiwa atambulike kisheria kwenye mifuko hii. Nilikuwa naomba tu Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati wa kuja kufunga hoja yake; bado mimi sijaelewa vizuri. Kwa uelewa wangu mdogo najua hii Mifuko ya Jamii ni mali ya wanachama. Sasa kama mali ni ya wanachama Serikali ipo kama mdhamini lakini si moja kwa moja kama ilivyo kwenye yale mashirika ya Serikali kwa mfano kama TTCL na mashirika kama hayo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, unapozungumzia mali ya wanachama labda TR aingie moja kwa moja kule kama msimamizi mali ya Serikali wakati ile si mali ya Serikali moja kwa moja ni mali ya wanachama, naomba ufafanuzi katika hili ili tuweze kupata uelewa wa pamoja.
Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho kuhusu Shirika la Nyumba la Taifa. Pamoja na kazi nzuri inayofanywa na Shirika la Nyumba la Taifa katika kujenga nyumba kwa ajili ya kupangisha na uwekezeji, lakini pamoja na nia nzuri ya kupunguza matumizi, bado utaalam na ubora unatakiwa uzingatiwe, sasa kumezuka tabia moja hasa kwenye mashirika haya ya Serikali, iwe NHC au TBA utakuta mwenyewe ndiye mkandarasi, wakati huo huo ni mshauri mwelekezi wa mradi na pia ndiye msimamizi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hali hii haipo kisheria, kwasababu pamoja na yote kuna mambo ya Kisheria. Lazima iwe kwamba engineer awe mwingine, msimamizi awe mwingine, ili kuonesha kama kazi inayotekelezwa inakidhi ubora unaotakiwa. Tukiachia hali hii iendelee, pamoja na nia nzuri ya kupunguza matumizi, lakini kuna uwezekano mkubwa wa kuja kupata miradi ambayo inakuwa chini ya kiwango, baadaye hata tija au value for money ikakosa kuonekena huko mbele. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, naunga mkono hoja, ahsante sana kwa kunipa nafasi.