Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara na Mazingira na Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji na Mitaji ya Umma kwa Kipindi cha Januari, 2016 hadi Januari, 2017

Hon. Stanslaus Haroon Nyongo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Maswa Mashariki

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara na Mazingira na Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji na Mitaji ya Umma kwa Kipindi cha Januari, 2016 hadi Januari, 2017

MHE. STANSLAUS H. NYONGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi hii niweze kutoa mchango wangu. Kwanza kabisa naomba ku-declare interest kwamba ni Mjumbe wa Kamati hii ya Viwanda na Biashara pamoja na Mazingira.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia napenda kutoa pongezi zangu za dhati kabisa kwa Mwenyekiti wangu kwa uwasilisho wake mzuri, amewasilisha vizuri na kwa kweli aliyoyaeleza ndiyo ambayo Kamati imeyasema niko hapa tu kwa ajili ya kusisitiza kwa baadhi ya mambo fulani ambayo nadhani ni muhimu tukayasisitiza na Serikali ikajua na Bunge likatambua nini cha kufanya.
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la viwanda na biashara kwanza ni suala mtambuka ambalo si kazi pekee inayomwelemea Waziri mhusika wa Viwanda na Biashara lakini ni suala mtambuka ambalo kama Serikali au nchi nzima kupitia sekta nyingine basi inabidi tushikamane bega kwa bega kuhakikisha kwamba tunaipeleka nchi yetu kwenda kwenye nchi ya viwanda kama Sera ya Chama cha Mapinduzi inavyosema.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna mambo mengi yamezungumzwa katika Kamati na katika kusisitiza, ni suala la upelekaji wa fedha za maendeleo katika Wizara zilivyopangiwa bajeti zake yaani katika Wizara husika. Kwa mfano, Wizara ya Viwanda na Biashara, pesa walizopata ni asilimia saba nukta tano tu na leo tuko quarter ya tatu tunakwenda kwenye quarter ya mwisho. Asilimia saba nukta tano Wizara ya Mazingira chini ya Ofisi ya Makamu wa Rais wenyewe hata sifuri, yaani hata percent kadhaa hawajapata wao ni sifuri kabisa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kwa kweli hii inawanyong‟onyesha watendaji wetu na Serikali iangalie namna ya kupeleka pesa za maendeleo kwenye sekta husika kwa muda unaostahili ili kusudi yale yaliyopangwa yaweze kutekelezwa. Ucheleweshaji huu sijui Waziri atafanya muujiza wa namna gani, sijui watendaji watafanya miujiza ya namna gani, kazi wamepewa, pesa za mishahara wanapelekewa, pesa za mishahara wanakula lakini pesa za kufanyia kazi hawapati, ina maana kama pesa ya maendeleo haijaenda ina maana hawa wafanyakazi wanapewa mishahara ya bure. Tunataka pesa ziende kwa wakati ili waweze kutekeleza yale ambayo yamepangwa na yale ambayo yanatakiwa yatekelezwe kwa muda uliostahili au muda uliopangwa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika ripoti hii imeelezea kuhusu kodi, tunapiga kelele sana kuhusu kodi na tozo mbalimbali, tunaomba vyombo husika muangalie upya kuhusu hizi kodi na hasa kwenye kodi ya capital investment, kwenye capital investment kuna VAT, kuna VAT hadi kwenye vyombo vya Serikali. TBS anapokwenda kuagiza vifaa vya maabara ili aweze kukagua bidhaa mbalimbali kwa usalama wa Mtanzania, maabara zao wanapoagiza vifaa zinatozwa kodi ya VAT, haya masuala tunakwenda kwenye bajeti inayokuja wayaondoe, Serikali iondoe VAT kwenye kodi za maabara. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, mwekezaji mkubwa anayetaka kuwekeza kwenye kiwanda cha kukamua bidhaa za mkulima anapoagiza bidhaa kubwa kwa maana ya mashine za kuchakata bidhaa mbalimbali za kilimo na zenyewe ana kodi kubwa amewekewa, tunaomba hizi kodi ziondolewe. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna masuala ya Sheria ya Manunuzi, ukienda pale TANELEC unakuta kabisa kwamba mmiliki wa TANELEC mmoja wa shareholders ni NDC na TANESCO ikiwemo, wana asilimia 10 mle ndani. Kutokana na Sheria hii ya Manunuzi inawafanya hawa TANELEC wakose biashara kwa TANESCO, yaani Mjumbe wa Bodi ya TANESCO ambaye ni Mkurugenzi wa TANESCO anaingia kwenye Board of Directors lakini biashara badala ya kuipa TANELEC ambayo yeye mwenyewe ndio mhusika mle ndani, TANESCO pamoja na REA wananunua transfoma na waya kutoka nje, wanaikosesha biashara pale. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, hii tumetazama katika nchi za jirani, tuliangalia tender board iliyotolewa kule Kenya kwenye shirika la umeme vilevile, wana-favour kampuni zao kwa kutoa tenda maalum kwamba tenda hii ijazwe na watu wanaofanya uzalishaji ndani ya nchi ile lakini sisi tunapeleka biashara nje. Sheria ya Manunuzi bado tunaendelea kuipigia kelele tuirekebishe na irekebishwe, kwa kweli inasikitisha sana. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la umeme nilishaliongelea, umeme sio wa uhakika. Quantity na quality ya umeme wetu bado ni tatizo kubwa, hatuwezi kwenda kwenye viwanda kama umeme wetu unaendelea kukatika namna hii na uzalishaji ukawa ni wa shida na bado umeme wetu ni bei ya juu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nijikite kwenye bandari, bandari yetu ni kivutio kikubwa sana cha watu kufanya biashara na naomba niseme kwamba bandari ipo chini ya Wizara ya Miundombinu, lakini bandari utekelezaji wake kikubwa ni kufanya biashara. Biashara ndicho chanzo kikubwa cha kuwepo kwa bandari pale, lakini ufanisi wa biashara wa bandari yetu hauvutii na ndiyo maana watu wanakwenda kuwekeza au kutumia bandari nyingine za jirani. Matatizo tumeyazungumza mengi – kuna single customer territory, tumeyaongea masuala ya kodi on auxiliary goods, yote tumekwishaongea, lakini ninachotaka kuzungumza leo, hata bandari yenyewe ndani ina matatizo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ukitazama toka mwaka 2012 mpaka 2017 wakurugenzi wa bandari wamebadilishwa watano, alikuwepo mzee Mgawe, alikuwepo Kipande, Massawe, Matei na mpaka leo yupo Injinia Kakoko, kila siku wanabadilishwa, kwa watumiaji inatia wasiwasi. Ukimtazama hata huyu aliyepo sasa hivi Mheshimiwa Engineer Kakoko amefanya mabadiliko ndani ya bandari, katika ile top management kabadilisha watu saba, kamwondoa bwana Gawire Mkurugenzi wa Utumishi, kapiga chini, Kilian Kaimu Mkurugenzi wa TEHAMA kafukuza, Magesa Kaimu Mkurugenzi wa Utekelezaji kafukuza, bwana Masoud Kaimu Meneja wa Fedha kafukuza, bwana Muhanga Kaimu Meneja wa Bandari kafukuza, bwana Mosha Meneja Msaidizi wa Bandari kafukuza, bwana Macha Meneja wa Utumishi kafukuza. Cha ajabu kabisa badala ya kufukuza kuweka watu competent, kaondoa hapa Msaidizi Operations Manager katoa kaweka mlinzi kuwa Operations Manager. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, maana yake ni nini, kuna siku atapakua mzigo kwenye bandari upande mmoja upande mwingine meli inazama, tuwe makini, haya mabadiliko yanatia wasiwasi, wafanyabiashara hawawezi kuja bandarini watakwenda sehemu nyingine, mtu wa security anakuwa Operations Manager, tunaomba tuwe serious. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine, meneja halipi watu on time. Wapakuaji wa mizigo, wanasema ile ni casual labour, wale wapakua mizigo hawana mkataba wa kupakua mizigo, sio wafanyakazi wa kudumu, wanapakua kama vibarua, wanapakua leo wapewe pesa zao leo, anayesafisha leo apewe pesa yake ya kibarua leo, Mheshimiwa huyu hawalipi wale watu alio-outsource, wale watu wenye kampuni ambazo zinaendesha zile shughuli hawalipwi, wanalipwa kidogo kidogo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, wanamwandikia barua awalipe anachelewa kuwalipa, hapa nina barua amepokea tarehe 23, mwezi wa kwanza, wanamwomba tulipe hela. Kuna kampuni inawadai hawalipi, ina maana wale wapakuaji, huyu mwenye kampuni itafika atashindwa kupata cash ya kuwalipa watu on a daily basis, atakosa ile pesa na akikosa pesa wale wafanyakazi watagoma na wakigoma hiyo habari itatoka nje, itakwenda Congo, itakwenda na nchi nyingine kwamba wafanyakazi wa Bandari ya Dar es Salaam wamegoma hawajalipwa, at the end of the day watumiaji wa bandari wanakwenda Beira, watakwenda Durban, watakwenda Mombasa, haya ndiyo yanayotuletea matatizo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Meneja wa Bandari mwingine katolewa Mhasibu kutoka TANROADS amekwenda kuwa meneja pale, that’s a professional job, ni watu wataalam wanatakiwa wafanye zile kazi. Jana sikupata muda wa kuongea kwa watu wa miundombinu – chunguzeni hili, kuna kampuni nyingine pale zinaonewa, kuna wengine wamepewa kazi tatu, moja anapakua mizigo ya kontena wanamu-underpay kwa sababu ana kazi nyingine mbili, wana…
(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuunga mkono hoja, ahsante sana.