Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara na Mazingira na Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji na Mitaji ya Umma kwa Kipindi cha Januari, 2016 hadi Januari, 2017

Hon. Hawa Abdulrahiman Ghasia

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Mtwara Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara na Mazingira na Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji na Mitaji ya Umma kwa Kipindi cha Januari, 2016 hadi Januari, 2017

MHE. HAWA A. GHASIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nikushukuru kwa kunipa nafasi ya kuweza kuchangia katika taarifa za Kamati hizi mbili. Pia nichukue fursa hii kuwapongeza sana Wenyeviti wa Kamati kwa kazi nzuri waliyoifanya kwa ajili ya kuishauri Serikali. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, mpango wa kwanza wa miaka mitano wa maendeleo ulikuwa na lengo la kutoa vikwazo vya kimaendeleo ambavyo vilikuwepo kipindi kile ikiwa ni pamoja kuongeza upatikanaji wa umeme, kuboresha miundombinu ikiwa ni pamoja na ujenzi wa reli na barabara pamoja ya kuboresha bandari zetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mpango wa Pili ambao tunao ambao una lengo la kuhakikisha kwamba tunakuwa na uchumi wa viwanda. Naliunga mkono sana hilo lakini wasiwasi wangu nahisi tunaweza tusifike mbali kwa sababu bado vile vikwazo ambavyo vilikuwepo katika mpango wa kwanza vinaelekea kwamba bado tunaendelea kuwa navyo na vingine si kwamba vikwazo halisi vipo lakini baadhi tu ya watu wanaamua kuvifanya viwe vikwazo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimpongeze sana Waziri wa Viwanda na Biashara, vile viwanda wanavyosema anatembea navyo mfukoni kwangu kwa kweli amenisaidia sana na tumefikia hatua nzuri. Nilimwomba kiwanda kwa ajili ya sulphur kwa sababu sisi kule ni wakulima wa korosho na sulphur kwa kiasi kikubwa tunaagiza kutoka nje, basi tuliomba angalau hata kufunga waje waifungie kule kwetu lakini pia tunaweza kutengeneza kwa sababu tunayo gesi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tayari mwekezaji amekuja, Mtwara amekwenda, ardhi tumempatia sasa hivi yuko hatua za mwisho na nina imani kabisa huko TIC atamaliza lakini wasiwasi wangu ni upande wa nishati, upande wa upatikanaji wa gesi na upande wa umeme, ndiyo maana nikasema kwamba vile vikwazo bado vipo. Gesi inatoka Mtwara lakini mpaka tunapozungumza hapa tunavyo viwanda zaidi ya viwili, vingine vinashindwa kujengwa; bado Wizara haina nia ya dhati ya kusaidia wawekezaji kuwapatia gesi au kuwapatia umeme wale ambao wanataka kuwekeza Mtwara. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, mapendekezo yangu; mwakani tutakapokuwa tunajadili Kamati ya Viwanda na Biashara iunganishwe na Nishati na Madini kwa sababu tulikotoka tulikuwa na changamoto sana ya ardhi kwa wawekezaji wetu kwenye viwanda. Sasa hivi hatuna tatizo kwenye ardhi, hatuna tatizo na Wizara ya Viwanda na Biashara, tatizo kubwa lililopo ni upande wa Wizara ya Nishati na Madini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mtwara tunavyozungumza sasa hivi umeme ni wa shida, mitambo inakufa kila mara, megawati 18 zinazozalishwa mahitaji zimeshazidi megawati 18 na hatuoni mipango ya uhakika ya kuhakikisha tatizo hilo linakufa. Tunacho kiwanda cha mbolea, tayari wamekuja Wizara ya Viwanda na Biashara imewasaidia imetoa eneo lake la EPZA, Wizara ya Miundombinu wamejenga barabara ya lami mpaka katika hilo eneo, lakini mpaka sasa hivi watu wa Wizara ya Nishati hawajaonesha nia ya dhati ya kuhakikisha kwamba kiwanda kile kinakuwepo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ndani ya Serikali kwa mtazamo wangu, wenyewe kwa wenyewe wanakwamishana na kwa kiasi kikubwa nahisi hata vile viwanda tunavyovihisi kwamba viko mfukoni si ajabu vinakwama kwenye nishati. Kwa hiyo, tuseme bila kigugumizi kwamba Wizara ya Nishati isaidie Wizara nyingine katika kuhakikisha kwamba viwanda, kama uchumi wetu ni wa viwanda, nishati kwa kiasi kikubwa itatumika. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, haiingii akilini kwamba Mtwara ile mpaka sasa hivi hawajamuingizia umeme hata mtu mmoja, hawajamuingizia gesi hata mtu mmoja na wala hawana mpango. Pia nimuombe Waziri wa Viwanda na Biashara atuelezee mpango mkakati wa kuendeleza viwanda katika Mji wa Mtwara. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunayo ardhi, eneo la EPZA, wengine wanalia fidia sisi fidia ilishatolewa tangu mwaka 2000, eneo lipo kuzunguka bandari, hakuna matatizo ya fidia wala nini, wanasubiriwa wawekezaji. Eneo ambalo Dangote amejenga kiwanda ni hekta 17,000, yeye amepewa 4,000 tu nyingine zipo za kumwaga hazihitaji fidia, hazihitaji kitu chochote, Mheshimiwa Waziri wa Viwanda na Biashara atuelezee na Waziri wa Nishati na Madini mikakati yao ya kuhakikisha gesi inatumika katika viwanda katika Mji wa Mtwara. Ni haki yetu watu wa Mtwara na sisi kupata maendeleo ya nchi hii na wala hatuombi favour. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ninalotaka nizungumzie, kama nilivyotangulia kusema eneo la EPZA Mtwara tunalo fidia ilishalipwa tangu kipindi cha Mheshimiwa Benjamin William Mkapa, eneo lipo wazi. Sambamba na EPZA ya Mtwara, tunayo Kurasini, tunayo pale Benjamin Mkapa na katika mikoa maeneo mbalimbali, EPZA ndiyo njia rahisi kama walivyotangulia kusema, ya kuhakikisha nchi inaendelea kwa haraka. Watu wanakuja na mitaji yao, wanakuja na teknolojia yao, sisi tunachopata pale, kwanza tunapata ajira, tunapata teknolojia mpya na pia tunapata pesa za kigeni. Hivi kwa nini tusihakikishe kwamba hii EPZA inakwenda kwa kasi, hata China tunaosema wameendelea walianzia na EPZA, kule akina Shenzhen, maeneo mengi, akina Guangzhou, kote walianza kama EPZA, kwa nini tusiige hayo mambo mazuri na sisi tukaweza kunufaika. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, niungane na wale wanaosema kwamba viwanda vile ambavyo vilibinafsishwa vihakikishe vinafanya kazi iliyokusudiwa. Kule kwetu Mtwara viwanda vya korosho watu walipewa kwa bei ya kutupa lakini hakuna hata mtu mmoja anayebangua korosho, wengi kazi yao wamefanya maghala wanayakodisha kipindi cha ununuzi wa korosho wanaona inawalipa kuliko kufanya viwanda, korosho zetu zinakwenda nje zikiwa hazijabanguliwa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, niungane na Mheshimiwa Rais, Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli, kuhakikisha kwamba viwanda vile kama watu madhumuni waliyopewa, kwa sababu hawakupewa kwa bei ya soko, walipewa kwa bei ya kutupa, wahakikishe aidha, wafanye kazi iliyokusudiwa au wanyang‟anywe wapewe watu wengine ili waweze kufanya kazi iliyokusudiwa. Haiwezekani kiwanda cha korosho leo kinageuzwa ghala la kuhifadhia korosho, kwa kweli hilo tulisimamie. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nampongeza sana Waziri wa Viwanda na Biashara, anahangaika katika kutafuta viwanda. Sisi kama Wabunge katika maeneo yetu lazima na sisi tumuunge mkono, amenipa mwekezaji nimekwenda naye nimemtembeza katika maeneo yote ya ardhi na akachagua eneo analolipenda na tumefikia hatua nzuri, nina uhakika kile kiwanda kitafika, lakini wasiwasi wangu Wizara ya Nishati na Madini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimpongeze Waziri wa Ardhi kwa sababu ili uweze kuwekeza vitu vikubwa muhimu ni ardhi, nishati na wenzetu hao Wizara ya Viwanda na Biashara ambao tunategemea waweke mazingira mazuri. Kwa sababu hawezi kujenga viwanda Waziri wa Viwanda na Biashara. Kazi ya Waziri wa Viwanda na Biashara ni kuweka mazingira mazuri ambayo anayaweka, Waziri wa Ardhi hana matatizo kwenye uwekezaji, ardhi, migogoro anatusaidia kutatua, lakini Nishati na Madini kwa kweli kama tunataka tuwe na uchumi wa viwanda Wizara ya Nishati na Madini kwa kweli iamke. Ndiyo tunapata umeme wa REA vijijini, lakini ule ni kuwasha tu vikoroboi badala ya vikoroboi sasa tunaleta bulb, tunahitaji umeme uzalishe, uinue uchumi wa nchi hii.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.