Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji na Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii kwa Kipindi cha Januari, 2016 hadi Januari, 2017

Hon. Dr. Mary Michael Nagu

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Hanang'

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji na Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii kwa Kipindi cha Januari, 2016 hadi Januari, 2017

MHE. DKT. MARY M. NAGU – MWENYEKITI WA KAMATI YA KUDUMU YA BUNGE YA KILIMO, MIFUGO NA MAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote, napenda kukushukuru kwa kunipa nafasi hii ili niweze kufanya majumuisho ya hoja mbalimbali zilizotolewa na Waheshimiwa Wabunge wakati wa kujadili taarifa ya Kamati ya Kilimo, Mifugo na Maji. Namshukuru Makamu Mwenyekiti kwa kuwasilisha taarifa vizuri asubuhi na nawashukuru Wajumbe kwa maandalizi mazuri ya taarifa yetu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kuwashukuru Waheshimiwa Mawaziri, Waziri wa Kilimo, Mifugo na Uvuvi pamoja na Waziri wa Maji na Umwagiliaji kwa kutoa ufafanuzi kwa hoja mbalimbali ambazo zilizotolewa na Waheshimiwa Wabunge. Napenda kuwashukuru Waheshimiwa Wabunge waliopata nafasi ya kuchangia kwa maandishi na kwa kuzungumza. Wingi wao umeonesha jinsi sekta hii ilivyo muhimu na nyeti sana kwa wananchi na kwa maendeleo ya Taifa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Waheshimiwa Wabunge 60 wamechangia ambapo 25 walichangia kwa maandishi na 35 walichangia kwa kuzungumza. Kwa muda ulionipa, naomba nisipitie orodha hiyo lakini nimeihifadhi na Waheshimiwa wanaweza kuja kuona ili waone kwamba mchango wa kila mmoja umechukuliwa na unafanyiwa kazi kuboresha taarifa ya sekta hii. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kuhitimisha hoja za Kamati kama ifuatavyo. Kwanza, nikiri kwamba hoja zile zilizotolewa kwa kweli zimeboresha taarifa yetu. Kuna Wabunge wawili walioleta ammendments ambazo tutaziongeza na nitapenda kusema ni kwa namna gani tutaziongeza. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, hoja zote zilijadiliwa lakini naomba niongelee hoja chache tu kwa sababu ya muda na ninyi wote mnajua muda huu ni mfupi sana. Nitajitahidi kama muda utaniruhusu nitakwenda kwenye hoja kadri ambavyo zitakuja kwenye taarifa hii.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze na mgogoro wa wakulima na wafugaji. Mimi nakubaliana na Waheshimiwa Wabunge kwamba si jambo dogo, ni kubwa. Wananchi wa Tanzania walio wengi ni wakulima na wafugaji na kama wao hawatakuwa wanapatana, ni migogoro kila wakati mfahamu ya kwamba na wao wenyewe wataathirika lakini maendeleo ya nchi yatakuwa yameathirika kwa kiasi kikubwa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, migogoro ya wakulima na wafugaji na watumiaji wengine wa ardhi inatokana na ardhi. Suala la mgogoro wa ardhi linahusisha wakulima na wafugaji kwa kiasi kikubwa. Nataka niseme kwamba kuna mgogoro wa wakulima au wafugaji na hifadhi, kuna mgogoro wa wakulima na wafugaji na wawekezaji, hakuna namna nyingine ya kumaliza migogoro hii bila ya Serikali kutekeleza kwa vitendo mpango wa matumizi bora ya ardhi kwa kupima na kutenga maeneo kwa ajili ya shughuli za kilimo, mifugo, uhifadhi na shughuli nyingine za binadamu kama Sheria ya Ardhi ya Vijiji Namba 5 ya mwaka 1999 inavyotaka. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Mchengerwa ameleta hoja hapa, yeye ametaka tuondoe hoja ya Kamati. Mimi naomba hoja ya Kamati ibaki kwamba Bunge liazimie Serikali iongeze kasi ya kutekeleza kwa vitendo mpango wa matumizi bora ya ardhi kama ilivyoainishwa kwenye Sheria ya Ardhi ya Vijiji Namba 5 ya mwaka 1999 na Bunge linaazimia kwamba mgogoro wa wakulima na wafugaji sasa ushughulikiwe katika ngazi ya Kitaifa chini ya Ofisi ya Waziri Mkuu, lakini kwa kuwashirikisha wadau wenyewe. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ndugu zangu nataka kusema kwamba Watanzania ni vizuri sana wafahamu kwamba ardhi ni mali ya asili na mali ya asili ambayo inatupa sisi maisha. Mifugo ni mali ya mtu mmoja-mmoja, lakini hata hivyo mifugo ni mali ya asili ya Taifa vilevile. Ni kweli kwamba kuna maeneo ambayo hayana utamaduni wa kuwa na mifugo, lakini kwa mujibu wa Katiba ya nchi yetu, Watanzania wana uhuru wa kwenda kila mahali lakini kwa utaratibu uliowekwa. Na mimi naona suala hili ambalo linawapa taabu hasa Mikoa ya Kusini na ile ambayo haikuwa na utamaduni wa mifugo, Serikali na wadau wanaohusika tujaribu kuangalia matumizi bora ya ardhi yanatekelezwa na sio kusema kwa mdomo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nasema hivi ndugu zangu kwa sababu Ethiopia ina ng’ombe milioni 55, Sudan ina milioni 38, sisi tuna milioni 25.8, tuna ng’ombe wachache kuliko wenzetu na ukiangalia nchi zile zina jangwa kuliko hata Tanzania. Kwa hiyo, jambo kubwa ni kwamba sisi hatujajipanga na tukijipanga tutaondoa migogoro hii, wakulima walime kwa amani na wafugaji wafuge kwa amani kwa manufaa ya Taifa letu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ambalo nataka nilisemee hapa ni kuhusu ruzuku ya pembejeo. Ndugu zangu kama tunataka tuwe na tija kwenye kilimo suala la pembejeo halina mjadala. Kwa kweli, Wabunge waliochangia hoja hii wameeleza jinsi pembejeo za kilimo zisivyowafikia wakulima kwa wakati na hivyo kukwamisha shughuli za kilimo. Wamependekeza pembejeo za kilimo ziuzwe madukani ili kuwapa wakulima fursa ya kununua pembejeo wakati wowote wanapohitaji na tozo yoyote iondolewe kwenye pembejeo ili waweze kumudu bei ya kununua na hivyo kuhakikisha kwamba tija ya kilimo inakuwepo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye pembejeo kuna suala la mawakala, naomba mmalize uhakiki Mheshimiwa Waziri. Hatuwezi kuendelea na uhakiki kwa mwaka mzima. Tukishahakiki tuwalipe mawakala wale ambao wanastahili kulipwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ni vyanzo vya mapato kwa Mfuko wa Taifa wa Maji. Waheshimiwa Wabunge wengi wamekubaliana na mapendekezo ya Kamati, lakini hapa Mheshimiwa Zitto alileta mabadiliko kidogo. Sisi tunacholilia ni kwamba Mfuko wa Maji uliopo hautoshelezi mahitaji na hasa ukizingatia kwamba mwaka huu fedha nyingi zilizoenda kwenye Wilaya zetu ni zile zinazotokana na mfuko na hela ya bajeti iliyotolewa ni kidogo sana. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, Wabunge wengi kwanza wameitaka Serikali itoe fedha hizo kwa sababu suala la maji kama alivyosema Mheshimiwa Waziri ni uhai, ni uchumi na bila maji hakuna viwanda, hakuna uhai na hakuna kuishi kule nyumbani. Kwa kweli wanaoteseka ni akina mama na ambapo wanapotumia muda mrefu kutafuta maji watoto wanaanguka au wanaungua kwa moto na gharama za afya na usalama wa watoto unakuwa hatarini. Kwa hiyo, naiomba Serikali ilione hilo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo ndugu zangu naomba Kauli Mbiu hii ya maji tuipokee. Pia kama alivyoleta mapendekezo Mheshimiwa Zitto, niwaombe wataalam waliangalie na wakati wa bajeti tuli-effect. Kwa hiyo, tumepokea mpendekezo yake, lakini inatakiwa kufanyiwa kazi na nina hakika itapita. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo nataka kuliongelea ni umuhimu wa kilimo cha umwagiliaji katika kukabiliana na ukame na mabadiliko ya tabianchi. Waheshimiwa Wabunge sisi na Watanzania wote ni mashahidi kuhusu ukame wa mwaka huu ulivyoleta frustration, umeleta hofu na ndiyo maana bei ya vyakula mbalimbali imepanda. Najua kuna Wilaya ambazo zina chakula, kuna Wilaya ambazo hazina chakula na zimesemwa kwamba ni 55, lakini hata wale wenye chakula kidogo kutokana na hofu iliyoletwa na ukame huu, bei ya chakula imepanda na kwa kawaida itachangia kwenye mfumuko wa bei.
Kwa hiyo, namuomba Mheshimiwa Waziri wa Kilimo na wengine wote wanaohusika kwa kweli tutafute na tusambaze chakula ili tu-stabilise bei ya chakula na kuondoa hofu ya watu na watu waishi kwa amani.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ili miaka ijayo tuweze kuondokana na hofu hii ya ukame, hatuna njia nyingine, Kamati inasisitiza umuhimu wa Tume ya Umwagiliaji kutegewa fedha za kutosha na kupelekewa fedha zilizoidhinishwa na Bunge kwa wakati ili iweze kutekeleza vyema miradi inayohusu kilimo cha umwagiliaji. Tunachoona ni kwamba Tume haijapelekewa fedha yoyote, tunamuomba Mheshimiwa Waziri wa Maji afuatilie kwa Waziri wa Fedha. Kilimo cha umwagiliaji kitasaidia kupunguza tatizo la uhaba wa chakula na njaa na itaifanya nchi hii iishi kwa amani zaidi kuliko kama tunakuwa na hofu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna mambo mengi ambayo ningeweza kusema ila nawaaomba sana Waheshimiwa Wabunge mapendekezo yaliyomo kwenye Maazimio ambayo Kamati imeyaandaa ambayo yamechukua mambo yote muhimu muyaunge mkono. Vilevile kama walivyosema Wenyeviti walionitangulia tutafute namna ya kuona kwamba Serikali inafanyia kazi Maazimio haya. Inaonesha kwamba taarifa za Kamati zimeleta manufaa makubwa sana na utaona kwamba Wabunge wengi wamebakia hapa na Mawaziri wamechukua muda wao kutoa ufafanuzi, lakini haitakuwa na manufaa kama kweli maazimio haya hayatafanyiwa kazi na Serikali na wale wote wanaohusika na tukiyafanyia kazi kila mwaka, ndivyo tutakavyopiga hatua.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hayo niliyoyasema, narudia tena kutoa hoja kwamba muunge mkono Maazimio ya Kamati hii ya Kilimo, Mifugo na Maji na ahsanteni sana kwa usikivu wenu.
MWENYEKITI: Toa hoja.
MHE. DKT. MARY M. NAGU – MWENYEKITI WA WA KAMATI YA KUDUMU YA BUNGE YA KILIMO, MIFUGO NA MAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nimetoa hoja lakini naomba nirudie. Natoa hoja tupitishe Mapendekezo na Maazimio ya Kamati ya Bunge.