Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji na Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii kwa Kipindi cha Januari, 2016 hadi Januari, 2017

Hon. Zuberi Mohamedi Kuchauka

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Liwale

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji na Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii kwa Kipindi cha Januari, 2016 hadi Januari, 2017

MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi hii na mimi nichangie kwenye hotuba hizi mbili. Awali ya yote nichukue fursa hii kuwashukuru sana Wenyeviti wa Kamati kwa hotuba nzuri walizotuletea.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba mchango wangu niuelekeze kwanza kwenye upande wa maji. Asubuhi nimeuliza swali la nyongeza hapa jibu nililolipata ni tofauti na matarajio. Mimi nimeongelea Mradi wa Ngongowele nimejibiwa mradi wa kijiji kingine tofauti kabisa na mtaa wangu. Mradi wa Ngongowele umegharimu shilingi bilioni nne mpaka sasa hivi hauna maendelezo yoyote yale na hautegemei kuendelea.
Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile katika Mji wa Liwale kuna mradi wa World Bank pale kutafuta chanzo mbadala cha maji umegharimu shilingi milioni 200 nao mpaka leo hii unasuasua mradi huo haujaendelea. Kwa hiyo, kwa ujumla wake katika Halmashauri ile kuna shilingi 4,200,000,000, naomba Kamati inayohusika hebu nendeni mkaangalie ili muweze kuishauri Serikali nini cha kufanya. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile katika ule mradi wa maji wa vijiji kumi, Liwale nimepata vijiji vitatu tu, kijiji cha Barikiwa, Namiu na Mpigamiti lakini kuna miradi ambayo mpaka sasa hivi imesimama na hakuna kinachoendelea ambayo ni miradi ya kijiji cha Kipule, Kiangara, Mikunya, Mpengele, Kimambi, Nangorongopa, Nahoro na Kitogoro. Kwa hiyo, naiomba Kamati hii kama itapata wasaa hebu iweze kutembelea Jimbo lile la Liwale muone pesa za nchi hii zinavyoharibika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naenda Idara ya Maliasili. Nimeshasimama hapa mara nyingi na nimeshaongea sana, lakini nataka niongelee mgao wa asilimia 25. Kwenye Jimbo langu la Liwale hatujapata huu mgao wa asilimia 25 pamoja na kwamba hatujui asilimia 25 inatokana na mauzo gani lakini walituambia kwamba Halmashauri zote zinazozunguka Hifadhi tutapata mgao wa asilimia 25 kutoka kwenye Serikali Kuu kama ruzuku inayotokana na mauzo ya maliasili ya misitu lakini mpaka leo hii jambo hili halijatekelezwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile kwenye upande wa Maliasili nikiongelea upande wa malikale. Sisi pale tuna jengo lile la Wajerumani ambalo ni kumbukumbu ya Vita ya Majimaji mpaka leo hii yapo majina kwenye zile kuta, lakini Mheshimiwa Waziri nilisikitika sana nilipouliza hili swali akaniambia kwamba Halmashauri ndiyo tuifanye hiyo kazi ya kuendeleza lile jengo ili kuweka kumbukumbu. Sijui ana maana kwamba sisi tufungue website yetu, tuutangaze utalii wa Liwale kwa kutangaza maliasili ile, mimi sijaelewa. Kwa hiyo, naomba Waziri mwenye dhamana hebu atueleze ile malikale inayopotea pale mpango wake kwa Serikali hii ni nini?
Mheshimiwa Mwenyekiti, nakuja kwenye upande wa kilimo ambapo tuna tatizo la pembejeo, wengi wameshaliongea kwanza haziji kwa wakati. Mkoa wa Lindi na Wilaya ya Liwale kwa ujumla wake safari hii tumepata viatilifu fake ambavyo vimetupelekea kupata mazao hafifu ya korosho. Ukienda kwa mawakala wale wanaouza pembejeo za kilimo, utakuta ana stock mbili; maana kule kiatilifu kikubwa ni sulphur, anakwambia hii ni sulphur ya ruzuku na hii hapaya kununua. Ukichukua ile sulphur ya ruzuku ni kwamba umeumia, lakini ukichukua ile sulphur ambayo inauzwa cash ndiyo inaweza ikakuletea mazao mazuri.