Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji na Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii kwa Kipindi cha Januari, 2016 hadi Januari, 2017

Hon. Shabani Omari Shekilindi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Lushoto

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji na Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii kwa Kipindi cha Januari, 2016 hadi Januari, 2017

MHE. SHABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi hii na mimi niweze kuchangia hoja ambayo iko mbele yetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kuwapongeza Wenyeviti wa Kamati wote wawili kwa kuwasilisha hoja zao vizuri. Pia ni-declare interest kwamba na mimi ni Mjumbe wa Kamati ya Ardhi, Maliasili na Utalii.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Kamati yetu tulitembelea mradi wa ujenzi wa Ofisi ya Mji Mpya Kigamboni, lakini mradi ule haujatengewa hata shilingi tano. Sasa basi niishauri Serikali ili jengo lile lisiendelee kulipa kodi wala wafanyakazi basi nadhani mradi ule urudishwe sasa kwenye Halmashauri ya Kigamboni. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia tulitembelea mradi wa utafiti wa nyumba bora na vifaa vya ujenzi. Kwa kweli kama tuna nia ya dhati tuwezeshe wakala wale wa nyumba na vifaa vya ujenzi. Tulifika pale wataalam walikuwa hata sita hawafiki, lakini vitu wanavyofanya ni vitu vikubwa sana. Sasa niishauri Serikali yangu kwamba wataalam wale wapewe uwezo ili waongezeke, waende mpaka Wilayani, naamini kabisa kwamba wataalam wale wakiongezeka na wakifika Wilayani vijana wetu watapata ajira. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimefika pale wanatengeneza vigae na tofali. Vigae vile wanatengeneza kwa nyuzi za katani, huoni sasa wataalam wale wakiwa wengi wataenda Wilayani mpaka vijijini na kwenda kufundisha vijana wetu wale na hao vijana wakishapata taaluma ile basi waende kwenye Halmashauri wajisajili ili kazi za Halmashauri zikitokea waanze kupewa kazi na kuanzakujenga majengo kama ya zahanati, maabara, shule na kadhalika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ule mradi nimeuona ni mradi mzuri sana. Naamini kama kweli Serikali yetu tukufu ina nia ya dhati basi iwekeze kwenye mradi ule. Wakala wale ni wa kweli wanafanya kazi nzuri sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, niongelee suala la migogoro ya ardhi. Migogoro ya ardhi ni kitu ambacho kimekithiri hapa nchini kwetu Tanzania. Sina imani kabisa kwamba migogoro hii inaweza kuisha kwa jinsi tunavyoenda sasa. Niishauri tu Serikali yangu kwamba kama tunataka migogoro hii iishe basi tuhakikishe kwamba tunaandaa utaratibu mzima wa maeneo yote ya hapa nchini yanapimwa na watu wanapata hati zao. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia tuhakikishe kwamba watu wetu wa Wilayani hususan Maafisa Ardhi wanapewa zana na vifaa vya kutosha kuweza kupima ardhi hii kwa haraka. Mheshimiwa Waziri wa Ardhi na Dada yangu Naibu Waziri wa Ardhi Mheshimiwa Angeline Mabula wanafanya kazi moja nzuri sana kiasi kwamba hata Watanzania walio wengi wanaimani kubwa sana nao. Walitutangazia kwamba wameshafuta mashamba zaidi ya 200 lakini kuna shamba la mwekezaji mmoja kule Mnazi anaitwa Renash Enterprises Plot No. 292, title deed 11,247 ekari 2,442; na title deed 1746 ekari 1,188; title deed 4144 yenye ekari 562.
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la kushangaza mwekezaji yule analima tu eneo hili tena eneo kidogo sana ambalo ni ekari 562. Eneo lote lililobaki amelitelekeza, ni vichaka, kuna mapori makubwa ambayo kwa kweli hayastahili kuwa pale wakati watu wana shida ya ardhi. Nimuombe Waziri wangu na Naibu Waziri wa Ardhi, title hizi zifutwe na mpaka sasa taratibu zilishafuatiliwa lakini naambiwa kwamba Ofisi ya Ardhi Kanda ya Kaskazini bado hati ile haijafutwa. Sasa nimuombe Waziri wangu atakapoamka ku-wind up basi aniambie kwamba hati ile itapatikana lini ili Halmashauri yangu iendele kupata mapato yale.
Mheshimiwa Mwenyekiti, niingie kwenye kilimo, naishauri tu moja kwa moja Serikali ijenge mabwawa mengi ya kutosha hapa nchini kwa ajili ya wakulima waweze kulima kilimo cha kisasa na cha umwagiliaji. Pamoja na hayo, wapeleke pembejeo kwa wakati pia hakuna asiyefahamu kwamba Lushoto ni ya wakulima wa matunda na mboga mboga, wakulima wale wanachangia sana kwa kutoa ushuru mwingi Halmashauri, lakini Serikali sijawahi kusikia Serikali inatenga ruzuku za pembejeo kuwapa wakulima wale wa matunda na mboga mboga. Ninaishauri Serikali yangu kwamba iwatengee wakulima wale wa mboga mboga na matunda nao waweze kupata ruzuku ya pembejeo.(Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, niongelee suala la maji. Kama inavyofahamika maji ni janga la Kitaifa basi nashauri kwa kuwa EWURA wanatoza pesa kupitia nishati hii ya mafuta, niiombe sasa EWURA itenge asilimia 50 kwa ajili ya kupeleka maji vijijini.