Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji na Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii kwa Kipindi cha Januari, 2016 hadi Januari, 2017

Hon. Katani Ahmadi Katani

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tandahimba

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji na Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii kwa Kipindi cha Januari, 2016 hadi Januari, 2017

MHE. KATANI A. KATANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru sana lakini pia niombe nitumie dakika saba ili dakika tatu atumie ndugu yangu Hamidu Hassan Bobali. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nikianza na Wizara hii ya Kilimo, kwanza nianze na suala la mfumo wa stakabadhi ghalani ambao umetumika kwenye korosho. Kwa namna moja au nyingine tumeona kabisa kwamba kwa wakulima wa korosho mfumo huu umewasaidia sana. Naishauri Serikali na Wizara kwamba mfumo huu usiwe kwenye korosho tu, kwa sababu Mikoa ya Kusini tunalima ufuta, mbaazi na mazao mengine. Sasa kwa sababu mfumo huu kwenye korosho umekuwa bora sana ingependeza sasa mfumo huu uelekezwe pia kwenye mazao mengine kama ufuta, mbaazi na mazao mengine kama tumbaku ili uweze kuwanufaisha na Watanzania wengine. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kumekuwa na jambo kwenye korosho linaitwa export levy, ushuru huu ni ushuru mkubwa sana. Kwenye korosho Serikali inachukua asilimia 15 ya market price, lakini kwenye maelekezo wakati wanaunda mfuko ule wa kuendeleza zao la korosho katika mambo ambayo wameyasahau sana sikuona pesa zinatengwa kwa ajili ya kuwanufaisha wakulima wa korosho kwenye suala la elimu. Leo kama kungekuwa na mkakati mzuri kwenye suala la elimu, ilivyotokea wanafunzi wa vyuo vikuu wamekosa mikopo na kwenye korosho kuna pesa asilimia 15 za export levy zingeweza kusaidia Mikoa ya Lindi na Mtwara kuongeza wadahiliwa wale wanaokwenda vyuo vikuu kwa kupata pesa za kutosha zinazotokana na hii export levy. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kumekuwa na changamoto nyingine kwenye Vyama vya Msingi vya Ushirika ambavyo vinachukua shilingi 60 kwa kila kilo moja kama ushuru wao. Pesa zile hazina maelekezo. Sasa ningemuomba Waziri kwa sababu jamii zetu zina matatizo mengi sana, wakati anatoa maelekezo yake aweke mkakati kwenye pesa za Vyama vya Msingi tuone zinaweza kusaidia jamii kwenye mambo ya msingi, leo tunakaa kuhangaika kutafuta pesa shilingi 10,000 kwa ajili ya CHF, wakati kwa mfano Mkoa wa Mtwara tuna Vyama vya Msingi ambavyo vinakusanya mamilioni ya pesa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mfano chama kimoja cha kwangu KITAMA kina uwezo wa kukusanya zaidi ya shilingi milioni 80,000 pesa ambazo ukienda kwenye mkutano mkuu wa chama cha msingi watu wanagawana shilingi 5,000 au 10,000 ambazo hazimsaidii chochote mkulima wa korosho.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa mapendekezo yangu kwa Wizara na kwa Waziri mwenye dhamana, aone ni namna gani pesa zile za Vyama vya Msingi za ushuru, inachukuliwa angalau kiasi fulani cha pesa zinawekezwa kwenye mambo ambayo yanaweza kusaidia jamii mfano hiyo CHF au la, hata wale watoto wanaofaulu kidato cha tano na kwenda cha sita kama wanakosa ada basi ielekezwe kwamba kila Chama cha Msingi cha Ushirika angalau kisomeshe watoto watano kuwapeleka form five na six. Ingesaidia sana, badala ya pesa hizi kuendelea kutumika kwa malengo ambayo siyo ya msingi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka jana tulikaa hapa tukawa tumezungumza jambo la stock exchange, jambo hili Mheshimiwa Waziri nilidhani kwenye majaribio haya tusiyafanye kwenye korosho tu kwanza. Mfumo wenyewe wa stakabadhi ghalani Mheshimiwa Waziri kama utakumbuka umeanza mwaka 2007 tumekuja kutekeleza mfumo wa stakabadhi ghalani 2016/2017 mwaka huu ambao wewe ndiyo Waziri! Maana yake miaka iliyopita yote mfumo wa stakabadhi ghalani haujatekelezwa Mkoa wa Lindi na Mtwara na maeneo mengine yote. Wakulima walikuwa wanaendelea kwa kutumia Vyama vya Msingi, kukopa pesa benki wakawa wanalipa pesa nyingi ambazo mpaka leo ukienda Tandahimba kule kuna vyama vinadai pesa nyingi kwa sababu ya mfumo ule mbovu ambao hatukuutekeleza kama tunavyoenda sasa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kwa sababu tumeanza mwaka huu kuutekeleza mfumo wa stakabadhi ghalani hii stock exchange naomba Mheshimiwa Waziri tuendelee kwanza na mfumo huu, tuwe tumejifunza vya kutosha angalau miaka mitatu, minne, tukijiridhisha kwamba tunakwenda vizuri ndiyo twende kwenye mifumo hii ya kisasa ambayo inahitaji capacity kubwa ya uelewa mkubwa, tofauti na watu wetu wa Mtwara. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, niingie sasa kwenye Wizara ya Ardhi. Alizungumzia Kaka yangu Mchengerwa pale. Nilipata fursa kukaa na wakulima pamoja na wafugaji. Suala linalozungumzwa na Mheshimiwa Mchengerwa pale lile la Rufiji ni jambo zito sana. Waziri wa Ardhi aangalie namna ya pekee sana na Wizara nyingine muone namna gani jambo hili la migogoro ya wafugaji na wakulima mnaweza mkalimaliza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Mwigulu akiwa Waziri wa Kilimo kipindi kifupi kile alianza michakato ya kuona migogoro hii inaishaje. Sasa siyo vibaya Mheshimiwa Waziri ukamfuata Mheshimiwa Mwigulu ukaangalia mikakati ambayo alikuwa anaiweka badala ya kila Waziri anaekuja anakuja na mkakati mpya, na mambo mapya mkayasahau hata yale mazuri ambayo wengine walianza kuyafikiria.
Mheshimiwa Mwenyekiti, niendelee kuomba Mheshimiwa Waziri kwenye jambo hili la Vyama vya Ushirika ambalo nilizungumza mwanzo uliangalie kwa mapana sana. Tuna madeni ya wakulima ambao wanadai pesa za korosho za mwaka 2012/2013 na mwaka 2013/2014 na hii kwa Wabunge ambao ni wawakilishi wa wanachi hatuna neno jema kwao ambalo tunaweza tukawajibu. Tumeshadanganya sana na ikiwezekana urudi mwenyewe uje Jimboni kwangu Tandahimba kuna wakulima wanadai pesa zao za mwaka 2012/2013, mwaka 2014/2015 mpaka leo hawajui hatma ya pesa zao zinapatikana namna gani. Kwa hiyo, niombe sana wakati wa majumuisho uone jambo hili unaliwekaje ili tuwe na majibu hata tunaporudi majimboni tuseme tulifikisha kwa Serikali na Serikali imetujibu moja, mbili, tatu, nne.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakushukuru sana.