Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini kwa Kipindi cha Januari, 2016 hadi Januari, 2017

Hon. Prof. Makame Mnyaa Mbarawa

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mkoani

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini kwa Kipindi cha Januari, 2016 hadi Januari, 2017

WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO: Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote
na mimi napenda kuchukua fursa hii kumshukuru Mwenyezi Mungu na naunga mkono hoja kwa
asilimia mia moja. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, mimi nitajielekeza kwanza kwenye Reli ya Kati. Kama
tunavyojua reli hii ya kati imejengwa mwaka 1905 na imechoka sana kwa sasa; na ina uwezo a
kuchukua tani milioni tano tu; na kutoka Da r es Salaam kwa mfano kwenda mwanza
unachukua takribani masaa 30. Serikali ya Awamu ya Tano chini ya kiongozi wetu Dkt. John
Pombe Joseph Magufuli aliamua sasa tujenge reli ya kisasa, reli ambayo itakuwa na uwezo wa
kuchukua mizigo tani milioni 17. Pia itakuwa na uwezo wa kukimbia kwa speed ya kilometa 160
kwa saa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, hii ina maana kuwa kutoka Dar es Salaam kwenda Morogoro
tutatumia saa moja na dakika kumi na sita, kutoka Dar es Salaam kuja Dodoma tutatumia
masaa mawili na nusu na kutoka Dar es Salaam kwenda Mwanza tutatumia masaa saba na
nusu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, katika Afrika kuna nchi tatu zilizojenga standard gauge, ya
kwanza Kenya, Ethiopia na Nigeria; lakini zote hizo treni zake zinakwenda speed ya 120 si 160
kama Tanzania. Na katika nchi hizo ni Ethiopia tu ndiyo inatumia umeme na sisi Tanzania. Katika
Bara la Afrika ni treni moja tu sasa hivi inayokwenda kilometa 160 ambayo ni Gautrain, ni ile
iliyopo pale Johannesburg na ile ni treni ya mjini inakwenda kilometa 80 tu; lakini ya Tanzania
itakwenda kilometa takribani 1,600. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kama mlivyosikia tarehe tatu tulisaini mkataba kati ya RAHCO
kwa niaba ya Serikali na kampuni ya Kituruki ambayo tunaita Yapi Merkezi na Kampuni ya Mota-
Engil ya huko Ureno kwa gharama ya dola za Kimarekani bilioni 1.2 sawa na kila kilometa moja
tutajenga kwa dola za Kimarekani milioni nne, hiyo ni pamoja na VAT. Ukiondoa ushuru kwa kila
kilometa moja tutajenga kwa dola milioni 3.4.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini naomba niwachukue Waheshimiwa Wabunge kwa
wenzetu majirani. Kenya wanajenga reli yenye urefu wa kilometa 605, wao wanatumia dola za
Kimarekani bilioni 3.1 sawa na kwa kila kilometa dola za Kimarekani milioni 5.3 wakati Tanzania
tunatumia dola za Kimarekani milioni 4. Ethiopia na wao wanajenga treni kama hii, wao
wanatumia kwa kila kilometa moja dola za Kimarekani milioni 4.5. Kwa hiyo, Tanzania tumeweza
kufanya wajibu wetu vizuri na tumepata kwa bei nzuri kuliko wenzetu wote. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kukawia kwingine ni kuzuri sana, unaweza kuwahi mwisho
wake ukaenda ukaangukia pabaya. Tunaamini Tanzania na timu yetu iliyofanya kazi hii ilifanya kwa uadilifu mkubwa na tumepata good deal tunasema. Na kazi hii ya ujenzi itaanza mwisho
wa mwezi Machi na itachukua takribani miezi 30. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, wakati huo huo tumetangaza tender kwa ajili ya Morogoro -
Makutupora; tumetangaza tender nyingine kwa ajili ya Makutupora hadi Tabora, kutoka Tabora
hadi Isaka na tender ya mwisho kutoka Isaka hadi Mwanza. Nia yetu ni kuwapata wakandarasi
mbalimbali ili kazi hii iende haraka na Tabora - Kigoma inakuja. Lakini kama kazi hii tutampa
mkandarasi mmoja anaweza kuchukua hata miaka minne ama mitano. Kwa vile Serikali
tumefanya uamuzi sahihi kwa watanzania. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa naomba nijikite haraka haraka kwenye Mamlaka ya
Bandari. Ni kweli Mamlaka ya Bandari katika robo ya kwanza ya mwaka huu wa fedha mizigo
ilipungua wala hakuna mjadala kuhusu hilo. Lakini kuanzia mwezi Oktoba, Novemba na
Disemba meli ziliongezeka na mzigo ulianza kuimarika. Ni kweli sasa hali ya bandari inaendelea
vizuri kuhusu mizigo na tunategemea hali hiyo itaendelea vizuri kila tunapoendelea. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa upande wa ujenzi wa miundombinu, tayari tumemepata
mkandarasi kwa ajili ya ujenzi au ukarabati wa Bandari ya Dar es Salaam gati namba moja
mpaka namba saba; na tunategemea baada ya mwezi mmoja na nusu kazi ya ujenzi itaanza.
World Bank wanataka kutoa pesa, lakini kama watachelewa tayari tumejipanga, tunazo pesa
bandari na tutaanza kufanya kazi hiyo mara moja. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa upande wa Bandari ya Mtwara tayari vile vile
tumeshampata mkandarasi na sasa hivi tunaanza kujipanga ili kazi ianze. Tumepeleka
document Ofisi ya Mwanasheria Mkuu kwa ajili ya vetting na tunafanya due diligence ya
mkandarasi huyo ili aweze kuanza kazi mara moja na gharama kwa ajili ya ujenzi wa gati hiyo
italipwa na Mamlaka ya Bandari kwa asilimia mia moja. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu flow meter. Tulitangaza tender lakini kwa bahati
mbaya sana tulipata wakandarasi wawili lakini wote hawakukidhi vigezo, kwa hiyo, tukaamua
tuanze mchakato upya na mchakato unaendelea vizuri kama alivyosema Mwenyekiti wa
Kamati yetu.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa upande wa scanner bandarini tayari tumetoa order ya
scanner kama tano kwa ajili ya kuimarisha ulinzi kwenye bandari zetu.
Mheshimiwa Naibu Spika, nitajikita kidogo kwenye shirika la ndege. Kama mnavyojua
shirika letu la ndege linaimarika vizuri na Wabunge wengi sasa mmefaidi matunda ya
Bombardier Q400, si kibajaji tena, sasa zimekuwa ndege. Serikali tunaamini tunaendelea
kujipanga kuleta ndege nyingine mpya nne ambayo Bombardier moja itakuja mwezi wa tano;
C series ambayo ni jet engine itakuja mwakani; kila moja itakuwa na uwezo wa kubeba abiria
150. Mwakani vile tutaleta ndege nyingine Boeing Dreamliner yenye uwezo wa kubeba abiria
262. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, tuna mpango wa kuibadilisha au ku-trade in ndege yetu
Bombardier Q300 ile ambayo ni mzee tuweze kupata ndege mpya Bombardier
Q400. Itakapofika mwisho wa mwaka 2018 shirika la ndege la Air Tanzania litakuwa na ndege
saba mpya. (Makofi)
Katika kuboresha utendaji kazi na utoaji huduma wa Air Tanzania wamenunua progamu
mpya sasa kwa ajili ya kufanya reservation na booking kwa wateja wake. Sasa wateja wote wa Air Tanzania wanaweza ku-book kupitia kwenye computer au hata kwenye smartphone.
Tumejipanga vizuri kuhakikisha kwamba tunatoa huduma iliyotukuka. (Makofi)
(Hapa kengele ya kwanza ililia)
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu marubani tunajipanga tulete marubani na kila sehemu
ya Tanzania tunataka kuhakikisha kwamba Bombardier Q400 inatua. Mheshimiwa Hawa Ghasia
tumekusikia na tutakuletea ndege hiyo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho kabisa niwahakikishie tu Waheshimiwa Wabunge
tumesikia malalamiko yao kuhusu barabara, Serikali ya Awamu ya Tano tumejipanga sana na
tunataka kuibadilisha nchi yetu kupitia miundombinu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho kabisa kuhusu sekta ya mawasiliano; tumebadilisha
kanuni za Mfuko wa Mawasiliano kwa Wote kuhakikisha kwamba tunapeleka huduma ya
mawasiliano kila eneo la Tanzania hasa yale maeneo ya mpakani ambayo hayana mawasiliano.
Mheshimiwa Naibu Spika, ushauri wa kuhusu TAZARA umepokelewa na mwisho kabisa kama nilivyoanza mwanzo ninaomba kuunga mkono hoja hii asilimia mia moja, ahsanteni sana.