Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini kwa Kipindi cha Januari, 2016 hadi Januari, 2017

Hon. Eng. Edwin Amandus Ngonyani

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Namtumbo

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini kwa Kipindi cha Januari, 2016 hadi Januari, 2017

NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO: Mheshimiwa Naibu Spika,
nakushukuru kwa kunipa nafasi, na niseme mapema kabla sijagongewa kengele,
nimefurahishwa sana na Taarifa ya Kamati ya Miundombinu na yote mliyoyaandika
tutayazingatia kwa umakini kabisa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nichukue nafasi hii kuwahakikishia Waheshimiwa Wabunge
wote kwamba mambo yote ambayo mmetuambia iwe kuhusu barabara, mawasiliano,
tutayafatilia kama ambavyo mmetuelekeza. Najua hii ni taarifa ya Kamati, lakini mmetupa fursa
na sisi tusikie yale ambayo mnahitaji kuyasikia. Na tumeyasikia, tutayachukua na tutayafanyia
kazi.
Mheshimiwa Naibu Spika, labda tu niende kwa haraka sana katika maeneo machache.
Kwanza naomba sana Waheshimiwa Wabunge wale wa upande wa Mtwara, walioongelea
barabara ya Mtwara hadi Mnivata, naomba nitoe taarifa rasmi kwamba ni kweli mkataba
umesainiwa tarehe 19 Januari. Taarifa ambayo tulikuwa tumetoa mwanzo ilikuwa inazingatia
taarifa mpaka tarehe 31 Disemba, 2016, ambacho ndicho kipindi tulichokuwa tunakitolea
taarifa. Naomba nitoe taarifa rasmi kwamba huo mkataba umesainiwa. Na ninamshukuru sana
AG personally kwa namna alivyofuatilia kuhakikisha kazi ya kukamilisha kile kipengele kidogo
ambacho kilikuwa kinaleta matatizo amekishughulikia kwa haraka sana. Nakushukuru sana AG.
(Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, Waheshimiwa Wabunge, ningependa vilevile kuongelea suala
la ukarabati na upanuzi wa kiwanja cha ndege cha Mtwara nikianzia na cha Mtwara, kazi ya
usanifu imeshakamilika hivi sasa taarifa ya mwisho inafanyiwa kazi na wataalam na mara
watakapoikamilisha tutaenda kwenye hatua inayofuata ya kutafuta fedha kuanza ukarabati.
Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile kwa viwanja vya Tabora, Sumbawanga, Shinyanga na
Kigoma, fedha tunazo kwa sababu tuna hela kutoka European Investiment Bank na suala la
mikataba hivi sasa tunavyoongeelea ndio tupo katika hatua ya mwisho ya kukamilisha
uchambuzi, umeshafanyika, muda sio mrefu watatoa taarifa ya akina nani watakuwa
wameshinda katika maeneo hayo na kazi ya ukarabati wa viwanja hivyo vinne ianze. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, ndugu zangu kwa viwanja vya Musoma, Iringa na Songea,
usanifu na ukarabati pamoja na usanifu kwa ajili ya ukarabati na upanuzi wa viwanja hivyo nao
upo katika hatua ya mwisho. Taarifa itakapokamilika zabuni zitatangazwa kwa ajili ya ukarabati
na upanuzi wa viwanja hivyo.
Mheshimiwa Naibu Spika, nikija kwenye kiwanja cha Mwanza, walisimama muda mrefu.
Nimshukuru Mheshimiwa Philip Mpango, Waziri wa Fedha na Mipango, ametuwezesha tumelipa
shilingi bilioni 7.6 na kazi ya ujenzi wa kiwanja kile cha Mwanza sasa imeanza kuchangamka
zaidi. Tunashukuru sana kwa hilo na tunaomba wenzetu wa Fedha waendelee kutupa hela zaidi
tuondoe maeneo yale yote ambayo tunadaiwa, ili kazi hii ya kujenga miundombinu kwa ajili ya
Watanzania tuweze kuikamilisha kwa haraka kwa sababu tunataka tufanye hivyo, lakini wenzetu wa Hazina ndio wanaotuwezesha. Nishukuru kwa kiwango hicho mlichotuwezesha
hadi sasa na ninaamini mtaendelea kutuwezesha zaidi.
Mheshimiwa Naibu Spika, na vivyo hivyo kwa Kiwanja cha Songwe tulichokamilisha,
kwanza ni usimikaji wa Taa za kuongozea ndege, hiyo tumekamilisha. Kilichobakia ni ujenzi wa
jengo la abiria na ambalo tulikuwa na ubishani kidogo au kuna mgogoro kidogo wa malipo.
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa nashukuru suala la mgogoro huo limekaribia kukamilika,
tupo katika hatua ya mwisho ya kusainiana kwamba, ni kiasi gani tuliwalipa zaidi na hivyo
waanze sasa kujenga kwa kiasi kile tulichowalipa zaidi, na bahati nzuri sasa tumeanza
kuelewana. Mwanzo tulikuwa hatuelewani na ndio maana tumechelewa kidogo katika kuanza
kujenga kiwanja hicho cha Songwe, sasa tumefikia mahali pazuri, naamini tutafika mahali sasa
kiwanja hiki nacho kitakamilika.
Mheshimiwa Naibu Spika, niongelee kidogo kuhusu TCAA; labda kitu kimoja tu, kuhusu
radar. Najua kuna wachangiaji wa maandishi wanatuletea, naomba tu nao niwathibitishie
kuwa ujenzi wa radar au usimikaji wa radar katika sehemu kuu nne za Tanzania, kwa maana ya
Dar es Salaam, Kilimanjaro, Mwanza na Songwe, mkataba wake tunatarajia muda si mrefu, sasa
hivi zipo katika process za procurement, nina uhakika katika kipindi kisichozidi wiki mbili tutakuwa
tumefika hatua nzuri na mwezi Machi mjenzi wa hizo radar itapatikana.
Mheshimiwa Naibu Spika, lengo letu ni kuhakikisha Tanzania yetu inakuwa covered na
radar. Si sahihi nchi yetu iwe inaangaliwa na Kenya, iwe inaangaliwa na Rwanda na sisi
wenyewe tupo kwenye giza. Hatutakubali hilo, na tunahakikisha katika miaka miwili ijayo
Tanzania yote tutakuwa tumei-cover kwa radar na tutakuwa tume-recover yale maeneo
ambayo wenzetu walikuwa wajanja, waliwahi kuwekeza katika radar na wakaanza kupata
mapato ambayo kwa kweli, yalistahili kuja katika nchi yetu; tutahakikisha mapato hayo
tunayarudisha.
Mheshimiwa Naibu Spika, ndugu zangu kwa upande wa mawasiliano; ninawashukuruni
sana kwa mambo mengi mnayotusaidia. Kulikuwa na tatizo kubwa sana kwenye Kampuni ya
Halotel, tumewapa mikataba ya kuweka mawasiliano katika vijiji mbalimbali karibu 4,000 lakini
mmekuwa mkitupa taarifa (mrejesho) kwamba hapa wanasema wameweka na wakati
mwingine ninyi Wabunge mnatuambia kwamba mawasiliano hayapo. Sasa nashukuru
kuwaambia kwamba tuna mitambo imeagizwa na taasisi yetu ya TCRA sasa ina uwezo wa
kupita kuhakiki katika kila maeneo ambayo wenzetu makampuni ya simu yamepewa kazi ya
kuweka mitandao hiyo, hawawezi kutudanganya tena kwa kuwa tutakuwa na uwezo wa
kuhakiki.
Mheshimiwa Naibu Spika, tunawashukuru sana Waheshimiwa Wabunge kwa hilo na
tunawahakikishia hivi vijiji 4,000 lazima tukamilishe itakapofika mwezi Novemba, kama mkataba
ambavyo tulikubaliana na watu wa Halotel. Vilevile niwambie tu kwamba hata Vodacom, Airtel
na TiGo, mwanzo waliokuwa wanadai kwamba, vijijini hakuna fedha kwa hiyo, hawataki
kwenda, sasa hivi wanavyoona jinsi Halotel wanavyochangamkia maeneo ya vijijini na jinsi
anavyo…
(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)
Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kweli, naunga mkono sana na sasa naelewa
kwa nini nina Maprofesa upande wa Kamati na upande wa Wizara. Nawashukuruni sana kwa
kazi kubwa mnayoifanya.