Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini kwa Kipindi cha Januari, 2016 hadi Januari, 2017

Hon. Selemani Moshi Kakoso

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mpanda Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini kwa Kipindi cha Januari, 2016 hadi Januari, 2017

MHE. MOSHI S. KAKOSO: Mheshimiwa Naibu Spika, nishukuru sana kunipa nafasi hii.
Kwanza awali ya yote niwapongeze sana Waheshimiwa Wabunge wote ambao
wamechangia, lakini ninanyongeza ya mambo ambayo tunahitaji kuishauri Serikali.
Mheshimiwa Naibu Spika, tatizo la fedha kwa Wizara husika ambayo imepewa
dhamana ya miundombinu bado ni ndogo, tunaomba sana Serikali ihakikishe inapeleka fedha
kwa wakati ili miundombinu iliyolengwa iweze kujengwa kwa wakati. Lakini tunaipongeza
Serikali kwa kufikia maamuzi ya ujenzi wa reli hasa reli ya kati ambayo kwa kuanzia Serikali
imesaini na Kampuni za Waturuki kuweza kujenga reli ambayo itakuwa na manufaa zaidi. Ombi
langu kwa Serikali ihakikishe inatengeneza mazingira mazuri ili kushawishi na makampuni
mengine yaweze kuomba tender ili iweze kujengwa reli ambayo itaenda kwa haraka,
ipambane na mazingira ambayo ni ya ushindani.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kitendo cha kujenga reli ambayo itaanzia Dar es Salaam
kuishia Morogoro bado tuna kilometa nyingi ambazo zinahitaji kujengwa kwa wakati. Ni vyema
Serikali ikajipanga kuhakikisha maeneo hayo yanatengewa fedha ili tupate fedha zitakazojenga
reli kuanzia Morogoro kuja Dodoma, Dodoma - Tabora, Tabora - Kigoma, Kaliua - Mpanda hadi
kule Kalema.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini bado kuna maeneo ya kuanzia Tabora kwenda Isaka
mpaka maeneo ya Kezya kule Rwanda ili yaweze kuendana na mazingira halisi ambayo
kimsingi tutakuwa tumeteka soko. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, eneo lingine ambalo tunahitaji kuishauri Serikali ni kufanya
maboresho ya ujenzi wa bandari hasa zile gati ambazo zinahitajika ziwe kwenye maeneo
ambayo yataenda kibiashara zaidi. Kwa sasa bandari bado haina uwezo mkubwa sana wa
kupokea meli nyingi, tunahitaji Serikali ielekeze nguvu kwenye maeneo husika.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini bado tunahitaji Serikali iboreshe bandari za mikoani hasa
kwenye maziwa makuu. Bandari zile zitachangia uchumi kwenye maeneo husika. Tunazo
bandari ambazo zimesemwa sana na Waheshimiwa Wabunge, Bandari ya Dar es Salaam
inahitaji maboresho, Bandari ya Tanga ambayo kimsingi itategemea kuchukua mzigo mkubwa
sana kutoka nchi ya Uganda inahitaji iboreshwe. Bandari ya Kigoma ikiboreshwa itasaidia sana
kukuza uchumi wa nchi hii kwa sababu iko jirani na DRC. Bandari ile ikitumika sambamba na
bandari ambayo inategemewa kujengwa Kalema itasaidia sana kukuza uchumi wa nchi na
sehemu kubwa na mzigo wa Congo ambao tunautarajia sana kutumika kwenye reli na Bandari
ya Dar es Salaam zitafanya kazi vizuri. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho...
(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzazji)
Mheshimiwa Naibu Spika, nishauri kwamba barabara zitengewe fedha za kutosha kwa
ajili ya kuunganisha mikoa yote ya nchi yetu. Ahsante.