Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mpango wa Pili wa Maendeleo wa Taifa kwa kipindi cha Miaka Mitano kuanzia mwaka 2016/2017 – 2020/2021

Hon. Issaay Zacharia Paulo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbulu Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Mpango wa Pili wa Maendeleo wa Taifa kwa kipindi cha Miaka Mitano kuanzia mwaka 2016/2017 – 2020/2021

MHE. ZACHARIA P. ISSAAY: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Nami naomba nitoe sehemu ya mchango wangu kwenye Mpango huu. Kwanza nachukua nafasi hii kumshukuru Mheshimiwa Rais John Pombe Magufuli kwa mchango wake wa kuitetea nchi hii katika kufanikisha azma nzima ya kuwaletea maendeleo Watanzania wote. Mheshimiwa Rais amefanya kazi kubwa sana, Waheshimiwa Wabunge na Watanzania tumwombee aweze kufanya kazi hii na tuweze kusogea kutoka hatua hii tuliyonayo tuweze kwenda mbele. (Makofi)
Pili, nachukua nafasi hii kuwapongeza Waheshimiwa Mawaziri kwa kazi kubwa wanayofanya. Nawaalika njooni Mbulu, msinitafute mimi, nendeni Mbulu. Mnahitajika sana. Mbulu tuna mahitaji makubwa, tuna kero nyingi. Nakupongeza sana Mheshimiwa Lukuvi kwa jinsi ulivyoshughulikia suala lililokaa miaka 10, sasa limetatuliwa, Wanambulu wana amani, wanakuombea. Waheshimiwa Mawaziri wengine baada ya Mkutano huu tunawaomba njooni Mbulu mtusaidie kwa jinsi ambavyo tuna matatizo mengi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nachukua nafasi hii kuungana pia na Waheshimiwa Wabunge wote na kuwashukuru kwa jinsi walivyochangia Mpang huu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza tusimamie mapato. Azma nzima ya Rais wetu kusema Tanzania inastahili kusaidia siyo kusaidiwa, ni ya kweli kabisa. Tusimamie mapato, tusimamie huu Mpango, ifike mahali Mpango huu uletwe tena mbele yetu, tuujadili jinsi ambavyo unahitaji kurekebishwa na kuondoa dosari zinazokinzana na mafanikio ya Mpango huu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa mpango wowote unapoletwa mbele ya Bunge hili tukiujadili, tukaupitisha, baadaye ukirejeshwa tunaweza kufanya marekebisho yanayohitajika katika Mpango kwa kufanyia utafiti kupitia kwa wataalam wetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ninalopenda kulizungumzia ni mahitaji makubwa ya wananchi kuliko uwezo wa Serikali. Hii itaondolewa pale ambapo mahitaji makubwa yanatokea ya kutazama tena upya Mpango huu ili uweze kuleta tija katika huduma za umma na sehemu mbalimbali kwa jinsi ambavyo umewasilishwa kwetu na Waziri wa Fedha.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana Waziri wa Fedha na wadau wote waliohangaikia Mpango huu ambapo ni dira ya Taifa letu kwa mmwaka huu katika kuleta maendeleo kwa Watanzania wote. Umuhimu mkubwa wa Mpango huu unamgusa kila mdau hasa yule wa chini. Kwa jinsi ambavyo tunahangaika wakati wote na Bunge letu linahangaika na sisi Wabunge kule Majimboni tumeahidi mambo makubwa sana, rai yangu kwetu sote ni kila mmoja atimize wajibu wake katika Mpango huu na aone ni kwa jinsi gani atahangaikia suala hili ili pengine Mpango huu kwa miaka mitano uweze kutoa matokeo makubwa sana yenye kuweza kufanyiwa kazi hasa katika maeneo yenye changamoto nyingi ambapo kwa namna yoyote ile kila mmoja wetu anastahili kutimiza wajibu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia tuone changamoto inayotokana na pato la Taifa kuwa dogo na jinsi ambavyo mahitaji yanakuwa makubwa, mengine yanaingia baada ya mahitaji ya dharura kutokea kama vile mafuriko, baa la njaa na mambo mengine kama magonjwa. Kwa hiyo, tunapopanga mpango tukienda miaka mitano bila kuwa na muda wa tathmini na muda wa kati na muda mrefu wa kuutazama Mpango huu umekinzana na mambo gani katika kufanikisha jambo lile ambalo limetokea na yale yaliyotokea katika Mpango, kwa kweli tunahitaji sana Bunge lipate kutazama upya na vikao vya tathmini vifanyike.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie pia eneo la Mkoa mzima wa Manyara jinsi ambavyo hatuna kiwanda, hatuna reli, hatuna pia miundombinu ya barabara ambazo zinaunganisha mkoa wetu hasa eneo la juu la bonde la ufa ikiwemo Wilaya ya Mbulu na Wilaya nyingine ya Hanang jinsi ambavyo tunahangaika kutafuta namna gani tunaweza tukanufaika na hali hii ya miaka mitano katika kufanikisha azma hii, ambapo kila mwananchi anahitaji afanikiwe.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naishauri Serikali, kwa jinsi ambavyo tunahangaika na kwa jinsi ambavyo mahitaji ni makubwa, basi rasilimali zile nyingine za miundombinu zinavyotekelezwa, kwa mfano, miundombinu ya vyuo, viwanda na miundombinu ya mbalimbali, tupate na sisi tulio pembeni na tulioko juu ya bonde la ufa hasa maeneo magumu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, zaidi nalilia barabara ya Mbuyuni - Magara – Mbulu. Mheshimiwa Waziri wa Uchukuzi na Wizara yake waje Mbulu waone jinsi tunavyoteseka na barabara hiyo ambayo ina jiografia ngumu na wananchi wanapoteza maisha mara nyingi, lakini barabara hiyo na udogo wake, haishughulikiwi. Tunaomba katika hii miaka mitano ufumbuzi wa barabara ile ya Karatu - Mbulu - Haydom na hii ya Mbuyuni – Magara – Mbulu na ile ya Dongobesh - Manyara kule Manyara – Dongobesh - Babati ipate basi namna ya kufanyiwa utatuzi ili wananchi wakae kwa amani.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ukuaji wa eneo hili unahitaji wadau wakubwa wa maendeleo, tusiisahau sekta kubwa binafsi ambayo ndiyo mhimili unaochochea maendeleo kwa nchi yetu hasa katika viwanda na katika ulipaji wa kodi na jinsi ambavyo Serikali inahitaji mapato ili iweze kutatua changamoto na matatizo ya Watanzania.
Mheshimiwa Mwenyekiti, niweze kuzungumza eneo hili kwa kufanya maandalizi ya Wataalam, miundombinu na fedha kwa ujumla katika ushauri wa jumla, lakini tusisahau kutoa nafasi kubwa katika uwekezaji kwa wazawa wa nchi yetu. Eneo hili linahitaji sana Watanzania ambao wataendesha shughuli nzima ya uzalishajii katika Sekta ya Viwanda na sekta mbalimbali ili tuweze kupata manufaa makubwa na Watanzania waweze kumiliki uchumi wa nchi kwa manufaa yao.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ukuaji wa sekta hii binafsi, unahitaji zaidi uchocheaji na uwekezaji katika wale wazawa ambao wanahitaji kufanya hivyo na kufanikiwa katika hali sahihi. Katika eneo hili la kukejeli kutumbua majipu; kutumbua majipu tuendelee kutumbua majipu kwa sababu ndio waliotufikisha katika hii hali ambayo tunakuwa tegemezi sana. Ili tuepukane na utegemezi ni lazima tusimame imara katika kuhakikisha eneo hili tunafanikiwa kwa jinsi ambavyo tunaweza tukaenda mbele katika ile hali ya kudhibiti ubadhirifu, ufisadi, hujuma za nchi na mambo mbalimbali. Kwa ujumla Mheshimiwa Rais ana azma nzima, Wabunge tuwe na azma nzima na Mawaziri mpate nafasi pekee ya kumpa ushirikiano Mheshimiwa Rais wetu ili tuweze kufanikiwa.
Kwa hivyo basi, katika harakati za pamoja, ushirikiano wa jumla unahitajika. Wanaokejeli shughuli za utendaji wa Serikali kwa sasa katika muda huu mfupi ni kama wameanza vibaya. Hatuna sababu yoyote ya kukejeli Serikali, bado ni mapema sana. Safari hii tunayoanza ni ya miaka mitano; tuko ndani ya miezi mitatu, minne, mitano hadi sita, tukianza kukejeli, matokeo yake ni hatujajua chombo hiki kinaendaje na kwa jinsi gani tunahitaji mafanikio na siyo kukejeliana au kukatishana tamaa katika mwelekeo wa Serikali yetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naiomba Serikali kwa nafasi ya pekee katika Mpango mwingine utakaowasilishwa hapo baadaye, tutazame upya hali ya Watanzania kwa jinsi ambavyo wanahitaji ushuru na kero mbalimbali ya tozo uondolewe kwa Watanzania wadogo. Wafanyabishara wadogo wana wakati mgumu! Tunapohitaji kuwadai ushuru na tozo mbalimbali, wao wanahitaji zaidi waweze kufanya mambo yao ya biashara ndogondogo ili wakue waje kwenye hatua ya wafanyabishara wa kati. Kwa hiyo basi, eneo hili litazamwe, lakini katika ile hali ya kulisaidia kundi hili la walioko chini sana katika maisha ya Watanzania.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mchango mkubwa unaotolewa na Mawaziri, Mheshimiwa Waziri Mkuu, Waheshimiwa Mawaziri na Wabunge kwa ujumla, unaweza kuchochea mafanikio makubwa na Mungu akitujaalia katika miaka hii mitano, Tanzania itasonga mbele na itakuwa nchi ya pato la kati na Watanzania wengi watanufaikia mapato ya nchi yao na watafurahia mafanikio ya nchi yao.
Mheshimiwa Mwenyekiti, binafsi nachukua hatua za makusudi kabisa za kututaka sisi Wabunge wote bila kujali itikadi; tumetoka kwenye Vyama mbalimbali, Majimbo mbalimbali lakini sisi wote ni Watanzania, tumeletwa na Watanzania katika Ukumbi huu ili tuweze kuzungumzia matatizo ya Watanzania, haijalishi ni wa eneo gani, lakini lengo kubwa ni kwa namna gani tunafanikiwa kutatua matatizo ya Watanzania wetu?
Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa yote lakini niseme kwa ujumla naomba ushirikiano kwa Waheshimiwa Wabunge wote. Hata huyu anayekejeli Serikali ataihitaji Serikali hii imhudumie.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi na ahsanteni kwa kunisikiliza.