Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa kwa Kipindi cha Januari, 2016 hadi Januari, 2017

Hon. Mohamed Omary Mchengerwa

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Rufiji

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa kwa Kipindi cha Januari, 2016 hadi Januari, 2017

MHE. MOHAMED O. MCHENGERWA – MWENYEKITI WA KAMATI YA KATIBA YA SHERIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nitambue michango ya Waheshimiwa Wabunge wote wa Bunge lako hili Tukufu waliochangia kuhusu taarifa ya Kamati yetu ya Katiba na Sheria. Waheshimiwa Wabunge 21 walichangia kwa kuzungumza lakini pia Wabunge watatu walichangia kwa maandishi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nitambue michango ya Waheshimiwa Mawaziri waliosimama mbele ya Bunge lako hili hususani Mheshimiwa Jenista Mhagama pamoja na Mwanasheria Mkuu wa Serikali kwa kutoa ufafanuzi wa baadhi ya hoja. Nami nitajikita kwenye baadhi ya hoja ambazo ziliibuka na kuzitolea maelezo na pia kuliomba Bunge lako Tukufu sasa lipokee na kukubali taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria pamoja na maoni na mapendekezo yaliyomo kwenye taarifa hiyo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilivyosema natoa shukrani za kipekee kwa Waheshimiwa Wabunge waliochangia taarifa yetu hii ya mwaka ambao ni 21. Naanza na hoja ya Mheshimiwa Balozi Adadi Rajab, Kamati inakubaliana dhahiri kabisa na mapendekezo yake kwamba Bunge liazimie kuitaka Serikali kufanya jitihada za kutosha kupunguza misongamano magerezani, tatizo la ucheleweshwaji wa kesi Mahakamani zinazohusiana na makosa ya mauaji na madawa ya kulevya.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hoja kwamba Kamati ina uwezo wa kulazimisha mahakama na kubadilisha taratibu ili kesi zichukue muda mfupi, sina hakika sana na hoja hii. Niseme tu kwamba kwa kuwa nilipata fursa ya kutumikia mhimili wa Mahakama kwa muda mrefu kidogo nafahamu zipo taratibu za kimahakama ambazo zinafuatwa na Mahakama zetu ikiwa ni pamoja na Katiba na Sheria ya Utumishi wa Mahakama pamoja na Judicial Administration Act ambayo ilipitishwa na Bunge lako hili Tukufu mwaka 2014.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusiana na mchakato wa kunyongwa wafungwa waliohukumiwa kunyongwa na kama Serikali inashindwa basi kifungu husika kibadilishwe kama ambavyo imezungumzwa na Mheshimiwa Adadi nitalitolea ufafanuzi hapo mbele.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mchango wa Mheshimiwa Abdallah Mtolea kuhusu watu wenye ulemavu na kwamba Kamati iliombe Bunge liazimie kwamba bajeti ya Ofisi ya Waziri Mkuu iongezwe hasa kwa Fungu la 65 linalohusika na kazi na ajira ili kuwe na mazingira bora ya kutengeneza ajira kwa vijana. Kamati pia inapenda kuikumbusha Serikali kwamba kile kiasi cha asilimia 10 kilichotengwa kwa ajili ya vijana na wanawake basi kiasi hiki kisipunguzwe na ile asilimia 50 iliyotengwa kwa ajili ya maendeleo pamoja na OC asilimia 40. Kwa hiyo, Kamati inaitaka Serikali kwamba kile kiwango cha asilimia 10 kilichotengwa kwa ajili ya akinamama na vijana kiwe ni kiwango asilia isipungue hata shilingi moja ili sasa vijana wetu pamoja na akinamama waweze kufaidika na kiasi hiki cha asilimia 10. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia tunatambua kwamba, nchi yetu inaongozwa na Chama cha Mapinduzi. Kwa mujibu wa ukurasa wa 110 wa Ilani yetu ya Chama cha Mapinduzi ilitengwa kiasi cha Sh. 50,000,000 kwa ajili ya kila kijiji. Tunaiomba Serikali kuhakikisha kwamba kiasi hiki cha fedha sasa kimetolewa ili kwenda kusaidia vijiji vyetu katika maeneo yetu mbalimbali.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Kamati pia inakubaliana na mawazo ya Mheshimiwa Mtolea kwamba Serikali iweke msisitizo mkubwa katika kusimamia haki na maslahi ya watu wenye ulemavu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu adhabu ya kifo, katika taarifa yetu ya Kamati kuhusu Muswada Na.4 wa mwaka 2016 iliishauri Serikali kupunguza misongamano magerezani na kufuata sheria ili adhabu ya kifo ambayo inatambulika kwa mujibu wa Kanuni za Adhabu (Penal Code), Sura ya 16 iweze kutekelezwa. Adhabu hii ya kifo ipo katika kifungu cha 197 na kifungu cha 196 ambacho kina-establish kosa la kuua. Kamati iliishauri Serikali kwa kuwa kuna mrundikano mkubwa wa wafungwa waliohukumiwa kunyongwa adhabu hii iweze kutekelezwa mara moja kwa sababu jukumu hili ni la kikatiba na la kisheria. Pia kama Serikali inaona adhabu hii haitekelezeki basi ni vyema ikawasilisha maoni ili iweze kuondolewa kwa mujibu wa Katiba.
Mheshimiwa Mwenyekiti, bado tunaendelea kuishauri Serikali utekelezaji wa adhabu hii uendelee kama ambavyo umeainishwa katika kifungu cha 197 cha Kanuni za Adhabu, Sura 16. Tunafahamu ni mateso makubwa sana wanayapata wale waliohukumiwa kunyongwa wakisubiri adhabu ya kifo. Wao wenyewe wako tayari kupatiwa adhabu yao ya kifo iwapo itatekelezwa hata kama ni kesho.
Mheshimiwa Mwenyekiti, wachangiaji wengine ni Mheshimiwa Taska Mbogo ambaye yeye amezungumzia suala la NSSF ambalo sitalizungumzia zaidi hapa kwa sababu tayari Mheshimiwa Waziri ameshalidokezea kuhusiana na mchango mkubwa wa hifadhi za jamii katika Taifa letu. Pia kama ilivyoagizwa katika taarifa za Kamati, Kamati inaendelea kusisitiza kwamba maagizo ya Bunge yatekelezwe na taasisi zote kama yalivyoelekezwa kuhusiana na uwasilishwaji wa mikataba ya uwekezaji unaofanywa na taasisi hii ya NSSF.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu taasisi za usimamizi wa haki, katika taarifa yake Kamati imesisitiza Mahakama na Tume ya Haki za Binadamu ziongezewe bajeti katika mwaka wa fedha ujao wa 2017/2018 ili kuboresha utendaji kazi wa taasisi hizo. Bajeti hiyo itasaidia utolewaji wa semina ili wadau wawe na uelewa wa kutosha wa sheria zinazopendekezwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Lucia Michael alizungumzia kwamba jukumu la Polisi sasa limebadilika kutoka ulinzi wa amani na kuelekea kwenye ukusanyaji wa kodi. Kamati pia inaendelea kushauri Serikali kwamba siyo jukumu la Polisi kukusanya kodi kama ambavyo inafanyika leo hii Polisi wanakusanya kodi kwa makosa mbalimbali ya barabarani ambapo wanawakamata washtakiwa na wanakusanya kodi kama wao ni TRA. Kamati inaitaka Serikali jukumu la ukusanyaji kodi liendelee kubaki TRA na kulitaka Jeshi la Polisi kuacha mara moja kufanya kazi hizi ambazo hawawajibiki kwa mujibu wa taratibu na sheria. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Chikota alizungumzia kuhusiana na fedha kutolewa chini ya kiwango kilichopitishwa. Msimamo wa Kamati ni kwamba fedha ziongezwe.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu ucheleweshwaji wa kesi mahakamani ombi la Mheshimiwa Adadi, kama nilivyosema hapo awali jibu katika taarifa ya Kamati kuhusu utekelezaji wa Wizara ya Katiba na Sheria, tarehe 3 Mei, 2016, Kamati iliagiza Wizara na taasisi zake kuhakikisha kwamba Mahakama inapunguza wingi wa kesi yaani backload of cases mahakamani na kwamba haki itolewe kwa haraka na kwa mujibu wa sheria kwani justice delayed is justice denied.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa namna ya kipekee nimpongeze Mheshimiwa Jaji Mkuu Msatafu Mohamed Chande Othman kwa jitihada zake kubwa alizofanya katika kupunguza mrundikano wa kesi mahakamani ambapo naamini Kaimu Jaji Mkuu wa sasa hivi anaweza kuendeleza ile njia nzuri ambayo alianzisha Mheshimiwa Jaji Mkuu Mstaafu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu taarifa ya Kamati kwa ujumla, Mheshimiwa Mtolea alisema kwamba taarifa imebeba maudhui mengi ya kikatiba na kisheria. Labda niseme tu kwamba Kamati ya Katiba na Sheria mpaka sasa imeshawasilisha Bungeni taarifa tisa, tatu za kibajeti na sita za Miswada ya Sheria. Kamati pia ilitoa maoni na mapendekezo ya jumla kuhusu Wizara na taasisi inazozisimamia, masuala ya kazi, ajira na watu wenye ulemavu yapo katika taarifa rasmi ya Kamati yaliyosomwa hapa Bungeni tarehe 19 Aprili, 2016.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Ngombale alizungumzia kuhusu Mabaraza ya Ardhi pamoja na uboreshwaji wa Kamati. Kamati pia inaishauri Serikali hususani Wizara ya Katiba na Sheria na tutaona uwezekano wa kukaa na Wizara hii ili kuweza kuzungumza na Mheshimiwa Waziri kuona uwezekano wa kesi za ardhi kurudishwa katika Mahakama ya Tanzania; kwa sababu tunafahamu kwamba kwa mujibu wa Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Ibara ya 107 inaitaja Mahakama kama ndiyo mhimili wa utoaji haki.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunafahamu kwamba upo mkinzano unaotokana na Mabaraza kuwa chini ya mihimili tofauti. Mfano, Mabaraza ya Ardhi ya Kata na Vijiji yapo chini ya TAMISEMI, Mabaraza ya Ardhi ya Wilaya yapo chini ya Wizara ya Ardhi lakini pia ipo Mahakama Kuu ambayo inawajibika chini ya Mahakama. Hivyo, Kamati inaona kuna mwingiliano mkubwa wa haki katika Mahakama na Serikali na ipo sababu kubwa hapo baadaye kuwepo na kesi nyingi za kikatiba kupinga hukumu zilizotolewa katika Mabaraza ya Ardhi kwa kuwa jukumu la mwisho la utoaji haki lipo chini ya Mahakama ya Tanzania kwa mujibu wa Ibara ya 107A ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 1977.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Omary Mgumba amechangia kuhusiana na mgogoro wa wakulima na wafugaji. Jambo hili sina hakika kabisa kama limeelekezwa kwenye Kamati yangu au ile Kamati ya Utawala lakini nataka niseme tu kwamba ni kweli kabisa mgogoro wa ardhi ni mkubwa sana katika nchi yetu na tunaona kabisa kwamba ile misingi imara aliyotuachia Mwalimu Nyerere ya Watanzania kupendana inakwenda kuvunjika iwapo migogoro hii ya wakulima na wafugaji haitatatuliwa mara moja. Hivyo, tunaona kabisa kwamba Wizara ya Kilimo na Mifugo imeshindwa kutatua mgogoro huu na tunaiomba Ofisi ya Waziri Mkuu sasa kuingilia kati ili kuweza kuondoa matatizo haya yaliyopo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lazima itambulike kwamba hakuna mgogoro wa ardhi, mgogoro uliopo ni mwingiliano wa kijinai yaani criminal trespass kati ya wakulima na wafugaji. Kwa hiyo, hatuna migogoro ya ardhi na naamini kabisa kwamba nchi yetu ina ardhi kubwa, mgogoro huu iwapo utatatuliwa kwa mujibu wa taratibu zilizowekwa utaweza kwisha mara moja.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Frank Mwakajoka alizungumzia kuhusiana na watu kukata tamaa kupiga kura. Kamati yetu kwa kuwa inasimamia Tume ya Uchaguzi tunaiagiza Serikali kuongeza fungu kwa ajili ya Tume ya Uchaguzi ili kuendelea kutoa elimu ya mpiga kura.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu wananchi kukamatwa kwa kutoa taarifa za njaa, tunaishauri pia Ofisi ya Waziri Mkuu, Wizara ya Kazi na Ajira kuendelea kutoa taarifa kuhusiana na majanga na maafa ili iweze kuondoa kero kubwa ambayo inajitokeza hivi sasa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Cecilia Paresso alizungumzia kuhusiana na ucheleweshwaji wa kesi kwamba viongozi wa CHADEMA wamekuwa wakikamatwa na kesi zao hazichukui muda mrefu. Ni jukumu la utendaji haki kama ilivyo katika Katiba kwamba ni lazima haki iendelee kuonekana imetendeka. Naamini kabisa kwamba siyo jambo la busara kwa kiongozi kuendelea kubaki mahakamani kwa muda mrefu. Kwa hiyo, tunaishauri Mahakama kuendelea kusikiliza kesi haraka hususani zinazowahusu viongozi wa vyama vya kisiasa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia itambulike kwamba zipo taratibu za rufaa ambazo zimeainishwa katika Katiba yetu ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Tunawaomba wale wote ambao wana malalamiko kuhusiana na kesi basi wafuate taratibu za rufaa ambazo zimeainishwa katika Katiba, lakini pia katika sheria mbalimbali za nchi yetu ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusiana na suala la akinamama magerezani, Mheshimiwa Mbaruk alizungumzia suala hili. Kamati inakubalina na mawazo ya Mheshimiwa Mbunge kwamba maslahi ya watoto yazingatiwe yaani best interest of the child pale ambapo wafungwa wanajifungulia magerezani. Kamati inasisitiza kwamba watoto wanaozaliwa katika mazingira haya watazamwe kwa umakini kwa ajili ya haki zao kama watoto kwa mujibu wa Sheria ya Watoto ya mwaka 2009 lakini pia na Mkataba wa Haki za Watoto wa mwaka 1989. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Paresso pia aliendelea kusisitiza kuhusiana na mrundikano wa wafungwa gerezani na utawala wa sheria. Suala hili Kamati inalitambua na inaungana na maoni ya Mbunge kwamba Serikali na Mahakama zifanye jitihada za kutosha kupunguza mrundikano wa kesi na wafungwa magerezani.
Mheshimiwa Mwenyekiti, michango iliyotolewa kwa ujumla ni kuhusu mrundikano wa wafungwa magerezani, wingi wa kesi mahakamani na kasi ndogo ya kumaliza kesi, haki za watu wenye ulemavu, suala la ajira na vijana, uongezaji wa bajeti katika Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora, ukaguzi wa miradi ya maendeleo, muda wa kikanuni uongezwe na jengo la Mwanasheria Mkuu wa Serikali lipewe kipaumbele. Kamati inakubalina na mapendekezo ya Waheshimiwa Wabunge na inaomba yawe sehemu ya mapendekezo ya Kamati na Bunge hili iyakubali kama maazimio ya Bunge yalivyotolewa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho kabisa naomba Bunge lako sasa lipokee na kuikubali taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria pamoja na maoni na mapendekezo yaliyomo kwenye taarifa hiyo pamoja na yale mengine ambayo nimeyasoma katika Bunge lako hili Tukufu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kutoa hoja.