Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria kwa Kipindi cha Januari, 2016 hadi Januari, 2017

Hon. Omary Tebweta Mgumba

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Morogoro Kusini Mashariki

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria kwa Kipindi cha Januari, 2016 hadi Januari, 2017

MHE. OMARY T. MGUMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa kunipa nafasi ili nitoe mchango huu katika mada iliyopo mbele yangu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nijielekeze moja kwa moja kwenye asilimia kumi ya vijana na akinamama. Niungane na wajumbe wenzangu waliotangulia, wengi wameshachangia mada hii hasa kutilia msisitizo kwenye hii asilimia tano ya vijana na asilimia tano kwa akinamama. Pamoja na kuchelewa kwa fedha za OC kwenda Halmashauri kwa sababu jambo hili ni la kisheria na jambo hili ambalo kwa sisi ni Ilani ya Chama cha Mapinduzi, tuliahidi kwa wananchi.
Naishauri Serikali ni vizuri ikafunguliwa akaunti maalum katika Halmashauri zetu kutenga fedha ili kila mwezi kwenye mapato bila kujali OC imekuja au haikuja.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mara nyingi kwenye bajeti zetu kule kwenye Halmashauri kama tulivyoona asilimia kumi inakwenda kwa vijana na akina mama, asilimia hamsini kwenye miradi ya maendeleo na asilimia arobaini kwenye matumizi ya ndani. Sasa mara nyingi wakati mwingine bajeti zinawekwa kubwa kwa ajili ya kupata hiyo asilimia 40 ya OC na matokeo yake kila hela inayokusanywa kwa kisingizio kwamba OC haijaja hela yote inatumika katika matumizi ya kawaida na matokeo yake hakuna mradi wowote wa maendeleo unakuwa umetekelezwa kwa kutumia fedha za ndani wala kwenda kwenye hii asilimia kumi kwa vijana na kila kitu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ni vizuri kwamba kila mwezi kila fungu ambalo tulilolipangia kwenye mipango yetu katika Halmashauri likawekwa kwenye akaunti yake ili kama OC haijaja basi athari iwe kwenye OC, katika ile miradi ya maendeleo iendelee ili tukifika mwisho tunajua OC tumekwama wapi ili wajibane wapi na ile miradi yetu ya maendeleo asilimia ile hamsini iliyotengwa hata kama tusipoimaliza yote lakini angalau kwamba kwingine tutakuwa tunaipunguza, la sivyo itakuwa kila kitu inaishia kwenye OC. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili kwenye suala la semina kwa viongozi. Ndugu zangu kama tulivyoona asilimia arobaini ya bajeti ya Serikali inakwenda kwenye miradi ya maendeleo. Hiyo miradi ya maendeleo inakwenda kule chini na watekelezaji na wasimamizi wakubwa ni Madiwani, lakini mpaka tunavyosema hivi hao wasimamizi wa miradi mikubwa na kutazama value of money kule chini hawana semina yoyote. Maana yake ni nini? Hawajui wanachoweza kukisimamia, kipi ni kipi. Ni vizuri pamoja na kujibana tukawapa mafunzo hawa Madiwani ili wawe na uelewa mpana wa kusimamia kile wanachopaswa kusimamia. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, pili; pia hata wale Viongozi wetu kule wa Serikali za Vijiji, kwa sababu kule hela zote hizi zinakwenda kwa Mwenyekiti wa Kijiji na Afisa Mtendaji. Afisa Mtendaji ni mwajiriwa wa Serikali ana mshahara, lakini huyu signatory ambaye ni Mwenyekiti wa Kijiji hana posho wala mshahara na ukizingatia ile asilimia ishirini haiendi huko. Kwa hiyo, anasimamia kitu ambacho yeye hafaidiki na chochote, sasa matokeo yake hata kudanganywa na Watendaji ili miradi hii isitekelezwe kwa kiwango kilichokubaliwa inakuwa ni rahisi sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naishauri Serikali yangu tukaangalia ni namna gani tunaweza kuwalipa chochote hawa Wenyeviti wa Serikali za Vijiji na Mitaa au posho ili waweze kusimamia miradi yetu kwa weledi mkubwa sana. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, niende kwenye utawala bora; suala hili la utawala bora hasa katika ngazi za Mikoa na Wilaya. Kwanza nimpongeze Mheshimiwa Rais kwa uteuzi mzuri alioufanya kwa Wakuu wa Mikoa na Wilaya, lakini pamoja na uteuzi huo bado hawa watu wanahitaji semina elekezi. Nasema hivyo kwa sababu kuna mambo mengi yanatokea hasa kwenye mgongano wa kimadaraka kule katika Halmashauri zetu.
Nitoe mfano tu kwenye Halmashauri yetu, unakuta Baraza la Madiwani wakati mwingine limeamua kwa mujibu wa kanuni na sheria lakini anaweza kuja Mkuu wa Wilaya au Mkuu wa Mkoa akasitisha yale maamuzi ya Baraza la Madiwani yasifanyike na matokeo yake Mkurugenzi anakuwa katika wakati mgumu amsikilize nani, alisikilize Baraza la Madiwani au amsilikize Mkuu wa Mkoa au Mkuu wa Wilaya. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, hii tuna ushahidi dhahiri upo umetokea kwenye Halmashauri zangu na matokeo yake Mkurugenzi huko analaumiwa na huku analaumiwa. Wakati mwingine tunawalaumu Wakurugenzi siyo maamuzi yao lakini kwenye kutumikia mabwana wawili na wakati mwingine majukumu yao hawayajui na mipaka ya kazi zao hawaijui, wanakuwa wanayumba yumba.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nitoe mfano mmoja tu ambao ulifanyika ndani ya Baraza la Madiwani; tumefanya maamuzi sahihi ya kuhamisha Halmashauri yetu kutoka Morogoro Mjini kwenye vijijini kwamba kikwazo kilikuwa pesa, tumepata pesa baada ya kushauriana na Wizara ya TAMISEMI yenyewe kwa msaada mkubwa ambao ametupa Mheshimiwa Waziri Simbachawene na timu yake, yule mdaiwa sugu matokeo yake akatulipa…
Mheshimiwa Mwenyekiti, jali muda wangu maana muda wenyewe mchache, siku yenyewe moja tunaijadili hii.
MHE. OMARY T. MGUMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana. Kwa hiyo, kwanza nampongeza Mheshimiwa Simbachawene kwa ushirikiano mkubwa sana alioipa Halmashauri ya Morogoro mpaka huyu mdaiwa sugu akatulipa hela zetu, tukapanga muda ndani ya mwezi mmoja tuhamie Makao Makuu kwenda Mvuha, kutoka Mjini kwenda Vijijini, lakini kabla ya maamuzi yale hayajafanyika, anajiandaa Mkurugenzi na timu yake anakuja Mkuu wa Wilaya, Mkuu wa Mkoa kupitia RAS anawabeba Wakuu wa Idara kawapeleka Mvuha kawabwaga pale anasema anayetaka kazi ndiyo hapa nimemfikisha, asiyetaka hamna.
Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lile halina choo, halina ofisi wala kitu chochote, lakini kwa kukubali kwamba ni mkubwa amesema hawa watu wakakaa kule, matokeo yake nini? Huo ni mfano mmoja mdogo sana. Sasa ni vizuri hawa watu wakapewa semina elekezi ili kila mmoja ajue madaraka yake na kila mtu ajue mipaka yake. Kwa sababu hawa wananchi Baraza la Madiwani ndiyo tunatakiwa tutetee maslahi yao. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kuhusu watumishi kutokujiamini katika kutoa maamuzi, huu ni mfano hai upo ndani ya Halmashauri ya Morogoro, tuna tatizo kubwa sana kule la wakulima na wafugaji, lakini ni kosa kwa kiongozi wa kuchaguliwa, uwe Mbunge au Diwani kusema kuna tatizo la wakulima na wafugaji. Umetokea mfano Diwani mmoja wa Kolelo amewekwa ndani mara mbili na vyombo vyenye mamlaka kwa kusema kwenye Kata yake kuna tatizo la wakulima na wafugaji, anaonekana ni mchochezi, sisi Wabunge ndiyo tulienda kumtoa zaidi ya mara mbili. Tunasema haya ni nini? Lakini Mungu siyo Athuman baadae yakaja kutokea mapigano makubwa sehemu ile ile viongozi waliyokuwa wanakataa kwamba hakuna mapigano ya wakulima na wafugaji; hakuna tatizo la wafugaji kuvamia kwenye mashamba ya wakulima. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nasema hivi ni kwa nini? Kwa sababu hawa viongozi wetu walishapewa miongozo kwamba sehemu yoyote kwenye tatizo la wakulima na wafugaji likitokea basi Mkuu wa Wilaya au Mkuu wa Mkoa hana kazi. Sasa wakati mwingine wanatumia kuficha maovu kwa kuogopa wao kuja kuchukuliwa hatua. Niombe sana tuwape moyo hawa viongozi, ni bora waseme ukweli ili tutatue tatizo kuliko kuficha baadaye mambo yanakuja kuharibika zaidi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu TASAF; kwanza niipongeze sana Serikali kwa mradi huu wa TASAF umesaidia sana kaya maskini, lakini naomba sana elimu iongezwe hasa kule vijijini hakuna elimu, wananchi hawajapata elimu sawasawa, kwa sababu wanaamini hasa wazee kwamba huu ni mradi wa kusaidia wazee, hawajui kwamba ni mradi wa kusaidia kaya maskini. Sasa ni lazima iongezwe ijulikane kuna tofauti ya kusaidia wazee na kusaidia kaya maskini. Mara nyingine unaona kuna mgogoro wanakwambia kijana ana nguvu zake lakini yupo kwenye mradi wa TASAF, kumbe ni kijana lakini hana uwezo kiuchumi. Kwa hiyo, ni vizuri elimu ikaongezeka kule chini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho, niongelee sasa kwenye Kamati ya Katiba na Sheria kuhusu suala la NSSF. Niungane na maoni ya Kamati kwa sababu ya utawala bora na kwa sababu tuna mihimili mitatu, Bunge, Mahakama na Serikali na Serikali imeshaanza kuchukua hatua katika wale watuhumiwa ipo kwenye vyombo vya uchunguzi, ni vizuri sana tukaipa nafasi Serikali ikamaliza uchunguzi wake, lakini naomba kuishauri baada ya uchunguzi huo walete taarifa hapa Bungeni ili ukweli ubainike.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.