Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa kwa Kipindi cha Januari, 2016 hadi Januari, 2017

Hon. Taska Restituta Mbogo

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa kwa Kipindi cha Januari, 2016 hadi Januari, 2017

MHE. TASKA R. MBOGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi hii. Nami naomba niongelee suala la ripoti yetu ya Kamati ya Katiba na Sheria, na-declare interest mimi ni Mjumbe wa Kamati ya Katiba na Sheria.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nizungumzie ufinyu wa bajeti. Kamati yetu ya Katiba na Sheria tulishindwa kukagua miradi ambayo iko nje ya Dar-es-Salaam kwa sababu ya ufinyu wa bajeti. Kamati imepewa milioni 20, milioni 10 kwa safari za ndani, milioni 10 kwa safari za nje. Kamati ina Wajumbe 25 sasa kama ni safari ya nje watakata tiketi ni shilingi ngapi hiyo? Milioni 10 si itakuwa imekwisha? Kwa hiyo, matokeo yake Kamati hii ilishindwa kabisa kwenda kujifunza jinsi Kamati nyingine za Katiba na Sheria zinavyofanya kazi zake nchi za nje.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano, kwenye Kamati yetu tuliletewa Muswada wa Legal Aid ambao tumetoka kuupitisha ndani ya wiki hii. Ilipaswa sisi kama Kamati tusafiri twende nchi jirani, Kenya walishapitisha huo Muswada, South Africa walishapitisha huo Muswada au Uganda, tukajifundishe, je, tunahitaji kuboresha kitu gani kwenye ule Muswada?
Mheshimiwa Mwenyekiti, Kamati hii ya Katiba na Sheria haikupata hiyo nafasi ya kwenda kujifunza kwa nchi za wenzetu wa jirani ile Miswada inasemaje. Matokeo yake tukaletewa huo Muswada, tukajadili kwenye Kamati yetu, tukawa tuna-struggle sisi wenyewe mpaka tukaweza kufanikisha kuleta huo Muswada humu Bungeni. Hilo naona ni tatizo na naomba kwenye bajeti ijayo Serikali ijaribu kufikiria na ijaribu kutuongezea bajeti na kuziongezea bajeti Kamati nyingine ili zisiwe zinapitisha vitu bila kuangalia nchi nyingine wanafanyaje, kwa sababu siku zote mtu unaangalia je, nyumba ya jirani wanafanyaje ili uweze kufananisha na kile kitu ambacho ninyi mmeandaliwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiona kuna hitilafu siyo vibaya mtu uka-copy kutoka kwa jirani yako au ukajifundisha kutoka kwa jirani yako. Kwa hiyo, naomba suala la Bajeti za Kamati Serikali itakapokuja na bajeti ya mwezi wa Julai ijaribu kufikiria kuongeza bajeti ya hizi Kamati zetu, hasa Kamati yetu ya Katiba na Sheria.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mfano mwingine Kamati yetu ilishindwa kwenda kukagua maafa kule Kigoma wakati kile Kitengo cha Maafa kiko chini ya Kamati yetu ya Katiba na Sheria. Samahani siyo Kigoma ni Kagera! Kagera walivyopata maafa sisi Kamati ya Katiba na Sheria tulipaswa twende kule tukakague yale maafa yameathiri kiasi gani, lakini hatukuweza kwenda kwa sababu ya ufinyu wa bajeti wakati lile fungu la Kitengo cha Maafa, fungu lake liko kwenye Kamati yetu, lakini hatukuweza kwenda kule Kagera kukagua huo mradi kwa sababu ya ufinyu wa bajeti. Kwa hiyo, naomba suala hili kwa kweli Serikali mwezi wa Julai itufikirie.
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine naomba Kamati ya Katiba na Sheria tunapoagiza maagizo, kwa mfano, tuliwaagiza NSSF watuletee mkataba wao walioingia na wale waliojenga zile nyumba za Kigamboni, zinaitwa Dege Eco Village, tuliagiza kwenye Kamati kwamba, watuletee ule mkataba kwa sababu NSSF huwa sera zao zinapitia kwenye Kamati yetu, tuliwahi kwenda kukagua zile nyumba pamoja na lile daraja la Kigamboni ilitushirikisha, lakini tulipoagiza kwenye Kamati tuletewe ule mkataba walioingia kati ya NSSF na lile shirika lililojenga hizo nyumba za Dege Eco Village, huo mkataba hatujaletewa mpaka leo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunashangaa Kamati na mimi nikiwa mmoja wa Wajumbe kwenye ile Kamati, kama Kamati inaagiza Mkataba kwa nini hao NSSF wasilete huo mkataba wakati sisi tulihitaji na nafikiri ni jukumu letu kwa sababu tunasimamia sera zao tuuone ule mkataba, lakini ule mkataba haukuweza kuletwa kwenye Kamati yetu. Kwa hiyo, naomba nalo hilo lizingatiwe.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tulitoa maagizo, tulienda kukagua Ofisi ya Makamu wa Rais tukakuta lile jumba limejengwa kwa nusu ya kiwango. Tumeingia pale Ofisi ya Makamu wa Rais ina muda sijui wa mwezi mmoja, lakini tulikuta mipasuko, finishing ilikuwa chini ya grade, siyo standard! Tukaagiza kwamba tuletewe ripoti ya fedha zilizotumika kwenye hilo jengo na tukaagiza marekebisho yafanywe, lakini ripoti ile hatujaletewa mpaka leo! Ni mwaka mzima tangu tulivyopita kwenye Jengo la Makamu wa Rais. Tulishindwa kwenda kutembelea Jengo la Makamu wa Rais lililoko Zanzibar kwa ufinyu wa bajeti, lakini Jengo la Makamu wa Rais la hapa Dar-es-Salaam tulilitembelea na kuna makosa tuliyaona.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mfano mdogo tulikuta jengo halina mlango wa kutokea unapotokea moto. Jengo limejengwa chini ya kiwango! Tulikuwa tumetoa hizo tuhuma na tukawaambia kwamba, watuletee wamefikia wapi, lakini hawakuwahi kuleta mpaka leo ni mwaka mzima. Kwa hiyo, tulikuwa tunaomba tunapotoa maagizo kama Kamati yatekelezwe. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine nataka kuongea kuhusu mambo ya mamlaka ya Wakuu wa Mikoa na Wakuu wa Wilaya. Nafikiri kila professional watu waheshimiane, mtu mwingine aheshimu professional ya mwenzie, kama ni Daktari aheshimike kama ni Mwalimu aheshimike. Kama ni Mkuu wa Wilaya afanye kazi zake za Ukuu wa Wilaya, lakini asimuingilie kwa mfano Daktari! Daktari ni professional, yuko professional, Mwalimu yuko professional, Injinia wa Mkoa yuko professional au wa Wilaya yuko professional, kwa nini aingiliwe katika utendaji wake wa kazi? Kila mtu aheshimu profession ya mwenzie. Tukiheshimiana hivyo kila mtu atatimiza wajibu wake.
Mheshimiwa Mwenyekiti, haitawezekana kwamba, mtu anakuwa ni Mkuu wa Wilaya au Mkuu wa Mkoa anaenda kutoa maagizo ya mambo ya Engineering wakati yeye siyo Engineer, anajuaje standards za engineering? Mtu ni Mkuu wa Mkoa au Mkuu wa Wilaya anaenda kutoa maagizo ya Daktari, yeye hajasomea udaktari, hana profession ya udaktari! Anatoaje maagizo kama hayo? Mkuu wa Wilaya au Mkuu wa Mkoa anaenda kutoa maagizo ya Afisa Kilimo, yeye hajasomea kilimo! Anajuaje mambo ya kilimo? Mkuu wa Mkoa siyo Mwalimu. Kila profession iheshimiwe! Mkuu wa Wilaya afanye kazi zake, Mkuu wa Mkoa afanye kazi zake tuheshimiane katika profession zetu ili tuweze kujenga hii nchi kwa sababu, usitoe maagizo ambayo hujasomea. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba hilo liweze kufikiriwa na watu waweze kuwajibika kwenye nafasi zao ili wasiogope kwa sababu, hili litazua utendaji mbaya wa kazi maana mtu atashindwa kutimiza wajibu wake kwa sababu atasema kwamba, nikifanya hivi Mkuu wa Wilaya atanifokea! Nikifanya hivi Mkuu wa Mkoa atanifokea! Matokeo yake ni yule mwananchi wa chini ambaye anahitaji zile huduma za Engineer au huduma za Daktari ndiye anayeathirika, Mkuu wa Wilaya hawezi kuathirika. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine niongelee suala la Halmashauri. Kwa mfano mdogo tu kule kwetu, ile Halmashauri ya Mpanda haina gari la kuzolea taka na hizi Ofisi za Wizara hii ya TAMISEMI imeziachia majukumu hayo Manispaa. Manispaa nyingine ni maskini siyo tajiri na hazina uwezo wa kununua hayo magari ya kuzolea taka, matokeo yake taka zinarundikana barabarani na kusababisha kipindupindu unasikia hakiishi(Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, mfano mdogo tu kule Kalema kuna kipindupindu na pale Mpanda taka zinaweza zikakaa wiki moja hazijazolewa kwa sababu hawana gari la taka na hawana uwezo.