Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mpango wa Pili wa Maendeleo wa Taifa kwa kipindi cha Miaka Mitano kuanzia mwaka 2016/2017 – 2020/2021

Hon. Zuberi Mohamedi Kuchauka

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Liwale

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Mpango wa Pili wa Maendeleo wa Taifa kwa kipindi cha Miaka Mitano kuanzia mwaka 2016/2017 – 2020/2021

MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote nitoe shukurani kwako wewe kwa kunipa nafasi ili niwe mchangiaji mmojawapo asubuhi hii ya leo.
Mheshimiwa Naibu Spika, mchango wangu kwenye Mpango huu ni kama ifuatavyo; Serikali yetu hii ya Chama cha Mapinduzi imekuwa ni Serikali ya kupanga mipango mizuri sana. Hii ni mara ya pili nalisema hili ndani ya Bunge lako Tukufu, lakini tatizo letu kubwa liko kwenye utekelezaji wa ile mipango tunayoipanga. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, sijui hizi takwimu mnazokuja nazo, hizi za ku-copy na ku-paste zinaletwa kwa sababu ipi? Tunakuwa tumedhamiria nini tunapoleta takwimu ambazo hatuna uhakika nazo na wala hazitekelezeki. Hatuwezi kuwa na mipango na ikatekelezeka iwapo hatuna mikakati iliyowazi ya kuonyesha namna gani tutatekeleza mipango hiyo.
Mheshimiwa Naibu Spika, nitolee mfano takwimu ambayo imetolewa na Mwenyekiti wa Kamati, anasema sera ya nchi yetu ilikuwa kuunganisha mikoa yetu na imekamilika na akaitaja baadhi ya mikoa na akasema ni mikoa michache tu ambayo imebaki haijaunganishwa. Hata hivyo, nashangaa Mkoa wa Lindi - Morogoro haijatajwa katika mikoa ambayo haijaunganishwa. Kwa sababu Mkoa wa Morogoro unapakana na Mkoa wa Lindi kupitia Wilaya ya Liwale lakini hakuna barabara. Mkoa wa Lindi unapakana na Ruvuma katika Wilaya ya Liwale hakuna barabara lakini takwimu hapa zinaonyesha kwamba mikoa hiyo tumeshaunganishwa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile Sera ya Taifa inasema kila kata kuwe na kituo cha afya na kila kijiji kiwe na zahanati. Lengo hili halijafikiwa kama ambavyo Msemaji wa Kambi Rasmi ya Upinzani amesema, tunadiriki vipi kwenda na mpango wa pili wakati hii mipango yetu ya kwanza haijakamilika, tena imekamilika kwa asilimia 26 tu. Katika Jimbo langu tuna kata 20 lakini tuna kituo cha afya kimoja tu.
Mheshimiwa Naibu Spika, leo hii hapa tunajitapa kwamba tunao uwezo wa kutekeleza mipango hii kwa kutumia rasilimali zetu ambazo nina hakika kabisa hazisimamiwi kama inavyotakiwa.
Ubadhirifu wa rasilimali zetu umekuwa ni mkubwa sana. Tunavyo viwanda, hivyo ambavyo sasa tunasema tunataka kuvifufua, Mkoa wa Lindi kulikuwepo na viwanda vya korosho vikabinafsishwa na havifanyi kazi mpaka leo lakini leo hii tunapokuja kufufua viwanda napata wasiwasi.
Mheshimiwa Naibu Spika, Mkoa wa Lindi sasa hivi unazalisha ufuta na korosho lakini kama nilivyosema tuna matatizo ya barabara. Hivi ni mwekezaji gani atayekuja kuwekeza Lindi mahali ambapo hakuna barabara, mahali ambapo hatujajiandaa na miundombinu yoyote? Nitoe mfano halisi, sasa hivi barabara ya Jimboni kwangu imeshafungwa, huwa inapitika kiangazi tu lakini sisi Mkoa wa Lindi ndiyo tunaoongoza wa kuzalisha korosho na ufuta lakini hatuna kiwanda hata kimoja. Mimi siwezi kumvutia mwekezaji yeyote aje kuanzisha kiwanda Liwale wakati ambapo hatuna barabara, umeme wala miundombinu yoyote, huku ni kudanganyana. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, mimi sijajua Serikali inavyokuja na hizi takwimu au maelezo ya juu juu wanakuwa wamedhamiria nini kwamba tupitishe tu ili mradi siku ziende au kweli tuko committed na hayo tunayoyaongea au tunayoyadhamiria? Kwa mfano, hapa tumesema malengo yamekamilika kwa asilimia tano, hivi ni kweli? Yaani mpango wa kwanza umetekelezwa kwa asilimia tano au asilimia 26 tunaingia kweli kwa kifua mbele kwa mpango wa pili, mimi sijaelewa na wala sishawishiki kuona kama tuko serious na jambo hili. Hivi tunawezaje kwenda na Mpango wa Pili.
Mheshimiwa Naibu Spika, nafikiri kikao kilichopita nilisema hapa kwamba hatuko serious. Mpango ule wa kwanza wa kujenga reli tulitekeleza kwa asilimia 5 tu na nikawaambia hapa kwamba hii haifanywi kwa bahati mbaya ila kwa makusudi kwani kuna watu wanataka wafanye biashara za malori, nikasema hapa wakaanza kulalamika. Mipango hii tunayokwenda nayo haiwezi kwenda kama hatuko serious. Mimi naomba Serikali ya Chama cha Mapinduzi kama hamko serious na nchi hii mtuachie na watu wako tayari kutuachia lakini ninyi hamtaki kutoka. Kwa mipango hii hatuwezi kwenda. Tumekuwa wepesi sana wa kuainisha vipaumbele lakini si watekelezaji wa vipaumbele. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nakuja upande wa kilimo, tangu Uhuru tumekuja na sera nyingi za Kilimo Kwanza, Kilimo Uti wa Mgongo lakini hivi kweli hiki kilimo kinaweza kikaimarishwa kwa njia hii na hakuna mkakati wowote wa kuimarisha masoko. Leo hii Waziri anakuja hapa anasema kwamba anataka kushusha bei mazao ya kilimo ina maana wakulima waendelee kuteseka, hiyo ndiyo mipango ya Serikali ya Chama cha Mapinduzi. Mtuachie nchi hii kwa sababu mimi ninavyofahamu huwezi kuimarisha kilimo kama haujaimarisha masoko. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, sisi kwetu tunapata shida, nitolee mfano wa Jimboni kwangu, tunalima korosho na ufuta lakini wananchi wangu wanahangaika kila mwaka. Mwaka huu wakivuna korosho, ufuta unapanda bei, mwakani wanavuna ufuta, korosho zinapanda bei hawajui kinachoendelea.
Leo hii tunakuja hapa na Mpango kwamba tunaanzisha viwanda hatujui hivyo viwanda vilivyokuwepo awali vilienda wapi, wale walioharibu viwanda hivi wamechukuliwa hatua gani hatujui, tunakuja tunavurugana vurugana hapa tu ndani kwamba tuna mipango endelevu.
Naomba Mheshimiwa Waziri atakapokuja atueleze, utekelezaji wa Mpango huu hizo hela anazipata wapi? Kwa sababu mipango iliyopita, Serikali ni hii hii, watu ni wale wale imetekelezwa kwa asilimia tano, leo hii mnakuja kutuambia kwamba mnaweza kutekeleza angalau asilimia 50, huo uwezo mnaupata wapi? Au ndiyo kama nilivyosema jana hapa tupo tu kwa ajili ya kuonekana kama sisi tupo Bungeni tunajadili mustakabali wa nchi yetu ili mradi siku ziishe lakini seriousness mimi sijaiona. Seriousness ya Chama cha Mapinduzi kuwahudumia watu wake sijaiona. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nawaambieni Jimboni kwangu tungekuwa tumepakana na nchi mojawapo ningeshawishi lile Jimbo tuliondoe Tanzania. Hata hivyo, kwa sababu tuko katikati hatujapakana na nchi yoyote tutaendelea kubaki kisiwani. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nasema hivi nikiwa na maana halisi. Mimi kwangu hakuna barabara, Kituo cha Polisi, hospitali, maji na nikisema hakuna maji namaanisha. Liwale tumerithi Kituo cha Polisi tulichukua jengo la benki.
MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza naomba ulinde muda wangu.
NAIBU SPIKA: Muda wako unalindwa, naona kuna taarifa nyingine.
MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Naibu Spika, pili naikataa taarifa kama ifuatavyo. Nimesema Wilaya ya Liwale haina barabara, mimi kila tarehe 15 Septemba na tarehe 15 Julai wananchi wa Liwale wanatoka kwenda Mahenge kwa miguu wanasindikizwa na askari wa wanyamapori na wanatembea muda wa siku tatu mpaka siku nne. Nimesema Liwale hakuna barabara, nimesema Liwale kama ingekuwa vita ile ya mwaka… (Makofi)
NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Kuchauka, naomba ukae kuna taarifa nyingine.
MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Kwa hiyo, nakataa Taarifa yake kama ifuatavyo; nimesema na naendelea kusema Liwale sisi hatuna hospitali inayoitwa Hospitali ya Wilaya, nashukuru aliyenipa taarifa ni Naibu Waziri wa Afya atalichukua akitaka kuthibitisha. Sasa hivi katika Wilaya nzima ya Liwale tuna Clinical Officers watatu tu, siyo Madakatari Bingwa ni Clinical Officers watatu tu mahitaji ni Clinical Officers 40, nasema kwa takwimu. (Makofi)
WABUNGE FULANI: Aibu.
MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Naibu Spika, labda uniambie unapotaka kuunganisha mikoa ina maana kwamba tutoke Lindi - Dar es Salaam - Dodoma - Iringa, twende Songea, labda kuunganisha kwa namna hiyo. Nikisema nina hali hiyo ya kusema, nawasemea wana Liwale. (Makofi)
Kwa hiyo, narudi kwenye Mpango. Kama nilivyotangulia kusema kwamba sisi shida yetu ni uhakika wa masoko. Serikali haionyeshi mahali ambapo wananchi hawa watasaidiwa vipi kwa upande wa masoko.
Mheshimiwa Naibu Spika, nikirudi kwa upande wa maliasili, sisi Liwale tuko kwenye Mbuga ya Selous lakini Liwale haina hoteli ya kitalii, barabara wala kiwanja cha ndege, hatunufaiki kwa chochote sisi kupakana na mbuga za wanyama zaidi ya kuendelea kupigwa na kunyanyaswa. Nimeshamletea Mheshimiwa Naibu Waziri wa Maliasili taarifa ya mgogoro uliopo Wilaya ya Liwale na Mbuga ya Selous. Sasa anapokuja Naibu Waziri akaniambia kwamba sina haki ya kuiondoa Liwale Tanzania sijamuelewa.
Mheshimiwa Naibu Spika, tunanufaikaje na maliasili? Sisi tunapakana na mbuga za wanyama lakini vilevile tulikuwa na uwanja wa ndege enzi zile za Mzee Kawawa, Mwenyezi Mungu amrehemu, tangu Mzee Kawawa amekufa na Liwale imekufa, ule uwanja wa ndege haupo tena pale. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, hivi leo hii Serikali hii kwenye Mpango wake huu, labda Waziri atakapokuja kuniambia kama ana mpango wowote, kama kuna mpango wa kuufufua uwanja wa ndege Liwale, kama kuna utaratibu wowote ule wa maliasili, kama wanajenga hoteli au kama wanatutengenezea barabara.
Mheshimiwa Naibu Spika, mimi nimetembea vijiji vyote vya Jimbo langu sijakuta hata choo kilichochangiwa na Selous, sijakiona! Sasa unategemea wananchi wa Liwale na Lindi wa-support mpango huu kwa kipaumbele gani ambacho wamepewa au kwa sehemu gani ambayo wamekumbukwa? Labda Waziri atakapokuja kwenye kujumuisha atakuja kunieleza kwamba Liwale au Mkoa wa Lindi kwa ujumla ameuweka katika mpango huu katika maeneo gani. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, leo hii Liwale bado watumishi hawataki kukaa kule, mawasiliano hakuna siyo ya barabara wala simu. Ndiyo maana nikasema hapa nahitaji Clinical Officers 40, siyo kwamba hawapangwi, wanapangwa lakini hawakai kwa sababu mazingira ya Liwale siyo rafiki. Jamani Chama cha Mapinduzi mtuachie hii nchi. Tuachieni hata miaka mitano tu muone nchi inaendeshwaje. (Makofi/Kicheko)
Mheshimiwa Naibu Spika, nilikuwa na hayo tu ya kusema. Ahsante sana.