Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali Pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018

Hon. Daimu Iddi Mpakate

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tunduru Kusini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali Pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018

MHE. DAIMU I. MPAKATE: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kabisa naunga mkono hoja ya mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa 2017/2018. Pili, napenda kutoa mapendekezo au ushauri wangu kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, suala la kilimo liangaliwe kwa upana zaidi ili kumsaidia mkulima kupitia vyama vya ushirika waweze kusaidiwa kwa urahisi zaidi kwani takribani asilimia 80 ya Watanzania ni wakulima. Hivyo, ili kuwahudumia vizuri inapaswa kuangalia chombo chao kinachowaunganisha kupitia vyama vyao vya ushirika vya mazao ili aweze kupata huduma kwa urahisi zaidi wakiwa pamoja kama elimu ya kilimo biashara, matumizi bora ya mbegu za mazao yao, kupata mikopo kupitia mabenki kwa kutumia vyama vya ushirika na mashamba yao kama dhamana ya Serikali.
Mheshimiwa Naibu Spika, pia pembejeo za kilimo zipatikane kwa urahisi na kwa wakati ili wakulima waweze kuendana na msimu wa kilimo ulivyo katika maeneo mbalimbali. Vilevile aina ya pembejeo kwa kila eneo izingatiwe zaidi kulingana na udongo wa maeneo husika.
Mheshimiwa Naibu Spika, suala la ujenzi wa maghala bora ya kuhifadhia mazao ni muhimu katika maeneo ya vijijini na Hifadhi ya Taifa ya Chakula kwa kuwa baada ya kuvuna vyakula hivyo ni vyema vikahifadhiwa vizuri kwa matumizi ya kipindi kijacho ambapo uzalishaji hamna. Ni vyema basi Mpango wa Maendeleo ya Taifa 2017/2018 ukazingatia ujenzi wa maghala haya kwani kwa mfano maghala ya Hifadhi ya Taifa ya Songea mahindi mengi yapo nje ambapo yana hatari ya kuharibika katika kipindi cha mvua, asilimia 50 ya mahindi yamehifadhiwa nje maghala yamejaa.
Mheshimiwa Naibu Spika, ili kuimarisha ushirika na mazao ni vyema basi Mpango wa Maendeleo wa Taifa ukatilia mkazo wa kuimarisha Tume ya Maendeleo ya Ushirika kwa kuiwezesha kifedha. Ni vyema Tume hii ikaimarishwa kiutaalam katika ngazi ya Taifa, Mkoa na Halmashauri za Wilaya kwa kuongeza watumishi wenye uwezo wa kusimamia ushirika na kurudisha imani ya wakulima kuamini vyama vyao vya ushirika. Ni vyema Makamishna wa Tume ya Ushirika wakateuliwa ili kuipa nguvu Tume hii kufanya kazi kama ilivyokusudiwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na kuimarisha Tume ya Maendeleo ya Ushirika, ni vyema kuimarisha Kitengo cha Ukaguzi wa Vyama vya Ushirika (COASCO) kwa kukiongezea uwezo kifedha na watumishi ili wapate muda wa kukagua vyama vya ushirika kila mwaka kwa maendeleo ya ushirika na wakulima wetu. Karibu wakulima wote wa Tanzania kwa njia moja au nyingine wanahudumiwa na ushirika wa mazao.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu soko la mazao yetu, ni vyema Serikali ikasisitiza kuuza mazao kwa mfumo wa stakabadhi ghalani kama inavyofanyika katika mikoa inayolima korosho ambapo mafanikio makubwa yanaonekana kwa wakulima wa Mkoa wa Lindi na Mtwara na imehakikishia Halmashauri zetu kuwa na uhakika wa kupata ushuru wa mazao kupitia mfumo huu. Mkulima anakuwa na uhakika wa kupata malipo yake ya mazao kupitia mfumo rasmi wa kiuchumi. Naiomba Serikali kuangalia uwezekano wa mazao yote ya biashara na chakula kuingia katika mfumo huu kwani unaruhusu wanunuzi kushindana katika bei.
Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho naunga mkono hoja ya mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa 2017/2018.