Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali katika Mwaka wa Fedha 2016/2017

Hon. Jenista Joackim Mhagama

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Peramiho

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali katika Mwaka wa Fedha 2016/2017

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU (SERA, BUNGE, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WALEMAVU): Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa, nitoe shukrani na pongezi za dhati sana kwa Waziri mwenye dhamana ya Fedha na Mipango. Tunamshukuru sana na tunampongeza kwa kweli kwa Mpango mzuri, Mpango utakaotuvusha nchi yetu katika kutupeleka kwenye Taifa na hali ile tunayoitaka, Taifa la kipato cha kati. Mheshimiwa Waziri wa Mipango tunakushukuru na tunakupongeza sana. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue nafasi hii kusema mambo machache sana. Nafurahi kuona kwamba Mheshimiwa Waziri mwenye dhamana ya Fedha na Mipango sasa ametuletea dira inayotupeleka kujibu hoja kubwa sana ya ajira kwa vijana wa Tanzania Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mambo yote Mheshimiwa Rais wetu wakati akiwa kwenye kampeni za uchaguzi, hoja iliyotawala kwa vijana wa Tanzania ni namna gani wanaweza kutengenezewa mazingira ya kupata ajira kwa utaratibu wa aina tofauti na kwa misingi ya ajira za aina tofauti.
Kwa hiyo, Mpango huu ukiutazama na hasa mtazamo huu wa kulifanya Taifa letu sasa liende kuwa Taifa la viwanda na viwanda vile vikiwa katika level mbalimbali, naomba niwahakikishie vijana wa Tanzania tatizo la ajira sasa litakwenda kutatuliwa kwa kiasi cha kutosha sana. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, vijana wanahitaji sasa watambuliwe. Mchango wao kwenye maendeleo ya Taifa hili ueleweke wazi, lakini wanahitaji kuwezeshwa, kutengenezewa miundombinu ambayo itawasaidia kushiriki katika uchumi wao wa Taifa. Mpango huu unatuelekeza huko na Mpango huu unatuambia kama tunakwenda kufungua viwanda kazi yetu sisi sasa, kama Wizara ya Kazi, ni kuhakikisha tunaanza kuwa na programu maalum, moja; ya kuwafanya vijana waweze kupata mitaji na mifumo itakayowafanya waweze kupata fedha za kujiingiza katika Mpango huo wa Maendeleo.
La pili, ni lazima sasa kupitia Wizara hii tujipange kuona vijana hawa sasa wanapata ujuzi, zile skills zinazohitajika ili waweze kujiajiri na kuajirika katika kujenga uchumi huu na kukamata uchumi wa nchi yao. Nawaomba Waheshimiwa Wabunge muunge mkono mapendekezo haya ya Mpango ili tatizo la ajira katika nchi yetu ya Tanzania tuweze kulitatua kwa kiasi cha kutosha. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niseme; Mpango huu pia, unakwenda kujibu hoja nyingi sana za muda mrefu za kundi maalum kabisa la wenye ulemavu katika nchi yetu ya Tanzania. Mpango huu sasa pia, utakwenda kutafsiri sheria na mikakati mbalimbali ambayo itakwenda kuwaruhusu watu wenye makundi ya ulemavu katika hatua mbalimbali na wao washirikishwe katika mipango ya maendeleo. Waweze kushiriki katika uchumi, waweze kushiriki katika uzalishaji, waweze kushiriki katika shughuli zote ambazo zitajitokeza kwa kuzingatia Mpango tulionao.
Kwa hiyo, naomba niwaambie Watanzania, Mpango ulioletwa na Serikali unakwenda kujibu matatizo mengi katika nchi yetu ya Tanzania na kama tulivyoona tutakapokuja kuunganisha Mpango huu sasa na bajeti, utajibu mambo mengi sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, vijana ambao wamesoma, vijana ambao wako kwenye elimu za kati, vijana ambao wako vijijini, unaona kabisa Mpango huu sasa tutakwenda kujipanganao na hayo matatizo yote ya makundi hayo yatakwenda kupatiwa majibu. Niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge, tutaendelea kuyashughulikia yale mnayotuambia ili tuweze kupata majibu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, yamezungumzwa hapa mambo mbalimbali, kero za dawa za kulevya; naomba niwaombe Watanzania wote tushirikiane kwa pamoja. Kama tunazungumzia maendeleo ya uchumi, tusipopambana na dawa za kulevya vijana hawa tutashindwa kuwashirikisha katika kujenga uchumi wa nchi yetu ya Tanzania. Sheria na mikakati yote itakayoletwa na Serikali tuiunge mkono, ili …
(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU (SERA, BUNGE, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WALEMAVU): Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja hii na naomba Serikali iende mbele.