Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali Pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018

Hon. Zuberi Mohamedi Kuchauka

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Liwale

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali Pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018

MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nianze na mchango wangu kwa kuangalia vipaumbele vya mpango wenyewe kuelekea Tanzania ya Viwanda. Nilitegemea kuona kilimo kikipewa kipaumbele katika mpango huu, lakini imekuwa kinyume chake sijaona mahali popote pakitajwa kama kipaumbele kwa kilimo cha mazao kama korosho, pamba, katani, ufuta na kadhalika ilikuwa malighafi katika viwanda hivyo. Hata hivyo, sijaona zao la ngano likitajwa popote wakati sasa ulaji wa watu nchini sasa umebadilika kwani sasa ngano huliwa zaidi kuliko mchele, mahindi na mazao mengine ya chakula.
Mheshimiwa Naibu Spika, nitoe mfano katika hili kama ifuatavyo:-
Kampuni ya Bakhresa peke yake kwa siku wanasindika tani 2700 za ngano ambazo zote zinatoka nje ya nchi. Katika miradi iliyotekelezwa hakuna mradi wa kilimo zaidi ya kuona mradi wa kuendeleza Kijiji cha Kilimo Mkoani Morogoro.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu viwanda sijaona kiwanda chochote kilichotajwa katika viwanda vinavyotarajiwa kukuza uchumi zaidi ya General Tyre na makaa ya mawe ya Mchuchuma na Liganga. Katika fungamanisha maendeleo ya kiuchumi na maendeleo ya watu hakuna uhalisia kwani hatujawaandaa vijana nchini kushiriki katika uchumi wa kilimo wala viwanda. Wakulima wetu wanashindwa kuondokana na jembe la mkono kwa kuwa hawakopesheki katika taasisi za fedha. Kwani gharama za kupata hati ya kumiliki mashamba bado ziko juu sana kwani hilo nalo sharti kuu kwa taasisi zinazokopesha vifaa ya kilimo kama tractor, hivyo kuwafanya wakulima kushindwa kulima kilimo chenye tija.
Mheshimiwa Naibu Spika, Wilaya ya Kilwa sasa imeanza kutoa madini ya gypsum ambayo sasa yanatumiwa na viwanda vyote vya cement nchini. Hata kusafirishwa kwenye nchi za Zambia, Malawi na Afrika Kusini, lakini sijaona mahali ilipotajwa katika mpango huu.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika taarifa ya Waziri wa Fedha kwa robo ya kwanza, sekta yenye ukuaji mdogo ni sekta ya usambazaji wa maji safi na udhibiti wa maji taka, pamoja na chakula na malazi, hivyo basi kutarajia kupata maendeleo toka kwa jamii yenye huduma hafifu kiafya ni sawa na kukamua ng‟ombe bila malisho.
Mheshimiwa Naibu Spika, elimu yetu bado ni ya kutegemea ajira kutoka Serikalini au sekta binafsi kwani wahitimu wetu wameshindwa kupata stadi za maisha kulingana na elimu wanayoipata. Vilevile kama hatutakuwa tayari kuboresha maisha ya Walimu na badala yake kuendelea kuwadhalilisha Walimu kwa kuwapa adhabu mbalimbali kama vile kuwapiga viboko mbele ya wanafunzi hakuinui ari ya Walimu hawa ya kufundisha.
Mheshimiwa Naibu Spika, viwanda; mlundikano wa viwanda katika Mji wa Dar es Salaam hasa kwa viwanda vinavyotegemea malighafi toka nje ungeweza kupunguzwa na kusambaza viwanda hivyo mikoa mingine ya nchi yetu. Ikiwa wawekezaji wangeondolewa kodi kwa wale watakaowekeza nje ya Dar es Salaam ili gharama zilingane na yule aliyewekeza Dar es Salaam. Kwa kiwanda kinachofanana kwani kwa kufanya hivyo kutasaidia kupanua ajira kwa vijana wa mikoa mingine kwa upatikanaji wa ajira.
Mheshimiwa Naibu Spika, sensa ya watu ni muhimu sana kwa sasa kwani takwimu tunazoletewa leo hazina uhalisia ukilinganisha na idadi ya watu. Hayo maendeleo ya kukua kwa uchumi tunayapima kwa kigezo gani wakati hatuna takwimu halisi ya idadi ya watu wetu. Ndio maana matamko mengi ya Serikali kuhusu huduma za jamii yanakosa uhalisia kwa wananchi wa hali ya kawaida. Haingii akilini mtu kuambiwa uchumi unakua wakati kipato cha mtu mmoja mmoja kinashuka.
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kumshauri Waziri mwenye dhamana ni bora akazingatia ushauri wa Wabunge ukizingatia ndiyo wawakilishi wa wananchi. Tunashauri kwa niaba yao kulingana na hali halisi ya maisha ya Mtanzania wa hali ya chini wa kawaida.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuwasilisha.