Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Hesabu za Serikali (PAC) pamoja na Maoni na Mapendekezo yaliyomo katika Taarifa hiyo; na Taarifa ya Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa (LAAC) pamoja na Maoni na Mapendekezo yaliyomo katika Taarifa hiyo

Hon. George Boniface Simbachawene

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kibakwe

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Hesabu za Serikali (PAC) pamoja na Maoni na Mapendekezo yaliyomo katika Taarifa hiyo; na Taarifa ya Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa (LAAC) pamoja na Maoni na Mapendekezo yaliyomo katika Taarifa hiyo

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kabisa nichukue nafasi hii kuwashukuru sana Wenyeviti wa Kamati zote mbili PAC na LAAC na Makamu Wenyeviti wao pamoja na Wajumbe wa Kamati hizi kwa kazi kubwa na nzuri wanazozifanya na kwa namna tunavyoshirikiana katika kufanya kazi ya maendeleo ya Watanzania.(Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, zimezungumzwa hoja nyingi sana, lakini kwa sababu ya muda pengine sio rahisi sana kuweza kuzijibu zote vizuri na nyingine ni mambo yanayoanza upya. Hata hivyo, nataka niseme jambo moja tu ili Bunge na sisi wote kwa faida ya maslahi ya Watanzania tuweze kuwa makini nalo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, tunapojadili Taarifa za Kamati ni lazima mambo tuliyoyachukulia hatua na kuyamaliza kwenye Kamati kule hayapaswi tena kuja huku na yanapokuja huku yanataka mjadala mpana sana ambao haupo. Kwa hiyo, tunapata shida kwa sababu baadhi mambo hapa tulikuwa tumekwishayazungumza na pengine ilipaswa kuwekwa vizuri ili yasirudi nyuma tulikotoka.
Mheshimiwa Naibu Spika, nichukulie mfano tu suala la UDA. Suala la UDA ni la muda mrefu, lakini nizungumze kifupi tu sitaki kwenda kwenye historia, ikuwaje na ikawaje. Nina muda mrefu lakini nikumbushe tu kwamba tarehe 13 hadi 15 Januari, 2015 Kamati ya LAAC ilitembelea Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam na kupokea taarifa kuhusu uuzaji na wakati huo Jiji la Dar es Salaam lilikuwa na msimamo wa kutokuahirisha uuzaji wa hisa zile. Maoni haya yalitolewa na Kamati ya PAC iliyopita ilikuwa chini ya akina Zitto Kabwe, lakini Kamati ya LAAC ikaagiza kwamba Jiji liondoe shauri lililofunguliwa Mahakama Kuu kitengo cha biashara ili Simon Group Limited aweze kulipa hisa hizo.
La pili, Simon Group Limited iruhusiwe kulipia hisa hizo haraka na ya tatu Jiji litoe account ya Benki kwa Simon Group Limited ili Simon Group Limited alipie hisa hizo kupitia account hiyo. Hapa yanasemwa mambo kama vile mjadala huu unaanza leo na wakati Jiji lenyewe limekwisharidhia. Tarehe 21 na 22 Januari, 2015, Kamati ya Fedha ya Uongozi ya Jiji la Dar es Salaam iliridhia kutekelezwa kwa maagizo haya ya LAAC. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa najiuliza hapa, Serikali hii ni mpya, Waziri mimi ni mpya, mambo haya yalikwishapita, kinachosemwa hapa maana yake ni kwamba maamuzi yaliyofanywa na Baraza lililopita la Madiwani wa Jiji la Dar es Salaam yanataka kuvunjwa na Baraza hili lililokuja leo. Sina hakika kisheria inakaaje lakini naanza kuona tatizo na mgogoro kama Bunge hili linaweza likaanza kufuta maamuzi ya Bunge lililopita, kama Serikali inaweza ikafuta maamuzi ya Serikali iliyopita, naanza kuona tatizo.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo nasema lakini tumekwenda vizuri na Kamati yako, tumekwenda hatua kwa hatua na mpaka sasa tuna maagizo ya Kamati ya LAAC juu ya jambo hilo na kuna taarifa wanazozihitaji zaidi ili tuweze kufahamu tunalimalizaje jambo hili. Kwa hiyo, Kamati hii tunafanya nayo kazi vizuri, Waheshimiwa Wabunge wasubiri tutakapomaliza na Kamati hii italeta mambo haya hapa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, limezungumzwa suala la Madaraka ya Rais kuteua. Ukisoma Katiba yetu ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Ibara ya 35(1), (2), (3) na (4) Rais anaweza ku-establish madaraka yoyote na anaweza kuteua mtu yoyote kushika nafasi yoyote kwa namna atakavyoona inafaa, hawezi kuhojiwa. Sisi wengine wote kama Mawaziri tunafanya kwa niaba yake kwa sababu ndio Mkuu wa Utumishi wa Umma. Kwa hiyo, haya mambo tunapoyazungumza tujue kwamba yana Misingi ya Kikatiba na Ikulu haiwezi ikakosea kwa sababu iko equipped. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini nikubaliane na Waheshimiwa Wabunge vizuri sana kwa asilimia mia moja kwamba wateule hawa ni vizuri wakafundishwa, wakapewa semina kama mlivyoshauri, ingawa tumefanya hivyo kwa kiasi kwa kanda, tumetoa semina kwa Wakurugenzi, Wakuu wa Wilaya, Ma-DAS, lakini tutaongeza jitihada ya kutoa semina zaidi ili wajue mamlaka yao na mipaka yao. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwamba Serikali inataka kuzivunja Mamlaka ya Serikali za Mitaa, hapana! Serikali nia yake ni kuziimarisha Mamlaka za Serikali za Mitaa kwa sababu zipo Kikatiba. Sura ya Nane, Ibara ya 145 na 146 zinatamka uwepo wa Mamlaka hizi, kama zilivyo Serikali nyingine. Kwa hiyo Mamlaka hizi zinapaswa kuendelea kuwepo.
Mheshimiwa Naibu Spika, hata hivyo, sisi katika Ilani yetu ya Uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi katika Ibara ya 147, tumesema waziwazi kabisa kwamba tutajitahidi sana kuziboresha na kuzipa uwezo Mamlaka hizi. Tumesema hapa kuendelea kuzifanyia mapitio Sheria zote zinazohusiana na Serikali za Mitaa na Mamlaka za Tawala za Mikoa ili kuharakisha mchakato wa Kugatua madaraka na lengo la kuziwezesha kutoa huduma bora zaidi kutoka ngazi za Vitongoji, Vijiji hadi kwenye Kata.
Pia tumesema (b) kuendelea kuzijengea uwezo Serikali za Vijiji kwa kuzipatia rasilimali watu na fedha ili ziweze kupanga na kusimamia kwa ukamilifu miradi yao. Lakini pia tumesema kuendelea kuongeza kiwango cha ruzuku katika Mamlaka ya Serikali za Mitaa, pia tunasema kuimarisha ubora wa upatikanaji wa huduma za jamii katika Mamlaka ya Serikali za Mitaa. Pia tumesema kuendelea kuchukua hatua kali za kinidhamu, za kisheria kwa watendaji wabovu na wanaofanya ubadhirifu katika Mamlaka ya Serikali za Mitaa. Hii tumeisema katika Ilani yetu ya Uchaguzi na hatuwezi kwenda kinyume na Ilani hii.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hivyo, niseme tu, kwamba ingekuwa sasa unataka kuchukua hatua hizi tunazozichukua sasa kwa falsafa ya kutumbuana kwa maana ya kuchukua hatua za haraka kunapotokea ubadhirifu au matumzi mabaya ya madaraka, ukalinganisha kinachofanyika leo na kinachosemwa na Wabunge, ukafanya flashback, ukaangalia Bunge lililopita na kilichokuwa kinasemwa juu ya Serikali kutokuchukua hatua, unaiona contradiction. Kwa hiyo, utawala wa nchi yetu hii unaweza ukawa mgumu sana kuutengenezea ideology kwa sababu kila mtu anataka kutengeneza ideology yake.
Mheshimiwa Naibu Spika, lazima tufike hatua tuamue, na watu wote waliopiga kura kwenye uchaguzi uliopita walipigia kura mabadiliko, nataka niwahakikishie Watanzania wanayataka mabadiliko kwa sababu walipigia kura mabadiliko, whether wao walipigia CHADEMA, whether walipigia CUF, whether walipigia CCM lakini wote wengine walifanya hivi, wengine walifanya hivi, lakini walikuwa wana lugha ya mabadiliko. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, hii ina maana gani? Ina maana kwamba Watanzania wamechoka kuishi vile ilivyokuwa, wanataka kitu kipya na ndicho hiki ambacho Rais Magufuli anakileta, si kama tulivyozoea. Hapa hatuna uwezo wa kukubaliana na kila jambo, tunaweza tukakubaliana kwamba yanahitajika mabadiliko wote tunakubaliana. Yafanyikeje haliwezi likawa jambo la kukubaliana, kwa sababu yanaweza yakawa kwa namna moja hayo yanayotaka kufanyika yanakugusa, kwa hiyo, hatuwezi kukubaliana, tuache walioshinda na anayeiongoza nchi atupeleke kwa mwendo unaotakiwa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, yamesemwa mengi lakini kama nilivyosema kwamba sisi tutaendelea kushirikiana na Kamati hizi lakini lilizungumzwa suala lingine la suala la Oysterbay Villa. Oysterbay Villa ulikuwa ni mradi wa kujenga nyumba kwa ajili ya kupangisha, mradi huu kusema ukweli ulikuwa ni mbovu, haufai na Mwanasheria Mkuu wa Serikali ameshawasilisha Mahakama ya Rufani maombi namba 299 ya mwaka 2016 kupinga uamuzi wa Jaji wa Mahakama ya Kitengo cha Biashara na Sheria uliofanyika ili ufanyiwe mapitio. Kwa hiyo, maana yake sisi Serikali haturidhiki na kinachofanyika pale katika lile, kwa sababu ya muda siwezi kwenda into details.
Mheshimiwa Naibu Spika, East Africa Meat Company zilitengwa fedha kiasi kikubwa tu, Dar es Salaam ilitoa Dola milioni moja, Ilala ikatoa Dola laki nne na themanini, Temeke Dola laki mbili na thelathini na mbili, Kinondoni Dola laki moja na themanini kampuni ya NICO ikatoa Dola laki moja na kumi na moja. Pia kulikuwepo na mwekezaji mwingine anaitwa Rheinhold and Mahla wa Malaysia ambaye alitakiwa kutoa mitambo yenye thamani kubwa tu kama sehemu yake ya umiliki.
Mheshimiwa Naibu Spika, ile bodi ya East African Meat Company ilipoanzishwa, ilipopata ile fedha ikaanza kuzitumia fedha zile kwenda kutafuta mitaji badala ya kutumia fedha zile kufanya uwekezaji. Serikali hii haifumbii macho ufisadi. Haturidhiki na hili tunaendelea kuchukua hatua na tumeshaanza kuchukua hatua, lakini tumewaomba wanahisa hawa wakutane waone wanaweza kufanya nini? Wakishindwa kukubaliana na wanahisa, basi waseme na ikibidi wa wind up ili wagawane kilichopo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, Jiji wasikae peke yao lazima wajue kwamba kuna Mamlaka hizi zinatakiwa na zenyewe kushiriki kuona kama wanakwenda mbele au wanakwenda wapi, wakishindwa Serikali itachukua hatua juu ya hao waliofanya hayo.
Mheshimiwa Naibu Spika, vile vile imezungumzwa asilimia 10 ya mikopo ya akinamama na vijana na hapo hapo ikazungumzwa asilimia 20 kwa ajili ya fedha kupelekwa kwenye mitaa na vijiji kama fidia ya vyanzo vilivyofutwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, own source inayozungumzwa hapa na kwa maana ya asilimia 10 iko huko huko Halmashauri ambako ninyi Wabunge mpo na ni Madiwani. Wakurugenzi ambao wanashindwa kupeleka fedha hizo mko nao huko na mnashiriki vikao. Mamlaka ya kuwawajibisha mnayo, kuwafukuza hata kuwasimamisha kazi Wakuu wa Idara mnayo, lakini hawapeleki pesa mnawangalia.
wa Kinondoni nafikiri, alichangia, rafiki yangu pale, amesema wao wamepeleka mpaka bilioni mbili, lakini pia kuna Mbunge wa Nyamagana amesema na wao wanapeleka kwa sababu wamemsimamia. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, Waheshimiwa Wabunge hayo mnatakiwa mkawasimamie nyie kuhakikisha kwamba fedha hizi zinakwenda kwa wapiga kura wetu. Ingawa kuna mgongano mkubwa sasa katika fedha hii ya gawio hili, hasa unapozungumza kuna maagizo ya Kamati hapa ambayo hayakupitishwa kama parliamentary resolution, yakaagizwa kwa Serikali kwamba 60 percent ya own source ifanyiwe development.
Mheshimiwa Naibu Spika, hapo hapo inasemwa 20 percent ipelekwe kwenye vijiji, 10 percent igawiwe kwa vijana na akinamama mikopo, 20 percent ibakie utawala, 10 percent ipelekwe kwa ajili ya kukatia bima ya wazee. Yaani there is a contradiction. Nadhani kwa sababu Serikali ndiyo inayotengeneza sera na hili jambo ni jambo la kisera, acha tukakae tutashirikishana tuone namna gani mgawanyo huu unaweza. Kwa sababu formula hii ya 60 percent development ilifanywa wakati Mheshimiwa Dkt. Kigwangalla akiwa Mwenyekiti wa TAMISEMI.
Mheshimiwa Naibu Spika, hata hivyo, si Halmashauri zote zenye uwezo wa kuwa na fedha ya kutoa 60 percent na zikabaki zinaweza kufanya shughuli zake. Itabidi tuzifanyie cluster ili tuone zipi zinaweza zikatoa hiyo pesa kwa development na zikaweza kujiendesha na zipi ziko maskini ambazo zina hela kidogo, hizo hazitaweza.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini hili la fedha limezungumzwa na Waziri wa Fedha. Tatizo la Wakuu wa Idara kukaimu, tumefanya upembuzi, Wakuu wa Idara 802 wanakaimu, kati ya hao 583 hawana sifa. Hata hivyo, nani anayepandisha mtu kuwa Mkuu wa Idara? Ni Mkurugenzi, ambaye mnaye pale, moja ya majukumu ya Mkurugenzi ni kuwaambia, wewe kama unaona wanafaa mbona huwapandishi tuwathibitishe? Kazi yenyewe ni nyepesi tu, kuwaleta kwetu na tuwapeleke for vetting, wakirudi wanathibitishwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, Wakurugenzi hawafanyi hivyo muwahoji huko kwenye vikao na muwachukulie hatua endapo hawataki kuwathibitisha wenzao. Tusaidiane ingawa tunatafakari kwa sababu upungufu ni mkubwa tufanye mass promotion. Tufanye vetting kwa pamoja, tuwatafute watu wenye uwezo wenye sifa, halafu tufanye mass promotion tunadhani pengine inaweza ikasaidia kwa sababu hawa kila siku wanatoka na kuingia.
Mheshimiwa Naibu Spika, maagizo ya RC na DED yanayoharibu Mipango ya Halmashuri na kuvuruga bajeti, lakini mengine yanaingilia Mamlaka ya Halmashauri zenyewe. Nataka niungane na Waheshimiwa Wabunge, kwamba hii haikubaliki na kwa sababu jambo lenyewe limekaa kitaaluma unajua masuala ya utawala hayana principle yaani yana namna fulani hivi, masuala ya utawala huwezi kuyatengenezea kanuni kama hesabu.
Mheshimiwa Naibu Spika, nadhani bado kupitia semina hizi tunahitaji kutoa elimu kwa wenzetu ambao wako huko, kuanzia Wakuu wa Mikoa, Wakuu wa Wilaya, Ma-DED, lakini pia na Ma-DAS. Nimeambiwa na najua kuna Wakuu wa Wilaya wengine hana raha mpaka aitishe Kamati ya Ulinzi na Usalama kila asubuhi.
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa Kamati ya Ulinzi na Usalama ikiitishwa kila siku asubuhi watu watafanya kazi saa ngapi? Polisi, OCD anakuwepo pale, mwisho nchi itakuja kuvamiwa pale hawana hata habari wako kwenye Kamati ya Ulinzi na Usalama. Kwa hiyo hili halikubaliki na nachukua nafasi hii kusema waziwazi kawmba waache, Kamati za Ulinzi na Usalama ni vikao muhimu na vinatakiwa kufanyika kwa jambo mahususi au maalum. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini yako maamuzi mengine yanafanya interference. Kinachoruhusiwa na hawa Viongozi wa Serikali Kuu ni kufanya intervention pale ambapo mambo hayaendi sawa, kwa mfano sheria inavunjwa, kuna mipango na mikakati ya kupiga hela, hapo ndipo wanapoweza kufanya intervention, lakini haiwezi kuwa Mamlaka ya Serikali za Mitaa imetoa maamuzi kwa kufuata sheria, utaratibu wote, halafu wewe unasema hii sikubaliani, hapana! (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, hiyo inaitwa interference, kwa hiyo haikubaliki, tutaendelea kuelezana, lakini wanajitahidi wanafanya kazi vizuri, tunahitaji kueleweshana, tunahitaji kuelimishana na hao walioteuliwa ndugu zangu ni Watanzania wenzetu. Tusiwe na sense ya kuwabagua, wana elimu, wana sifa, wamesoma hata sisi tulipokuwa Wabunge hapa hatukuja na uzoefu huu. Kwa hiyo, tukubaliane kwamba ni wenzetu, ni ndugu zetu, wanatakiwa kupata fursa na wao kujifunza. Ukisoma, Mheshimiwa Zitto alikuwa ameni-consult hapa nikamwambia viko vifungu ambavyo vinawapa Mamlaka lakini kwa sababu ya muda acha niliache. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nizungumzie vikao vya Mabaraza ya Madiwani na Kamati za Uongozi vinapoitishwa wakati Bunge linaendelea. Tumetoa maelekezo kwamba wasiitishe vikao hivyo wakati Bunge linaendelea. Tumetoa na kuelekeza ma-RAS, nadhani ujumbe labda haujakwenda, pengine tupeleke nguvu zaidi ya kuwaeleza wao wenyewe kwamba, lazima wahakikishe wanaitisha vikao hivyo wakati Bunge halipo kwenye session ili Wabunge wapate fursa ya kuhudhuria.
T A A R I F A...
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Naibu Spika, naikubali lakini itabidi tu-harmonize haya mawazo na yale mawazo mengine, tupate utaratibu fulani mzuri unaoweza ku-accommodate situations zote.
Mheshimiwa Naibu Spika, nimalizie. Kinachokosekana kwenye mamlaka zetu zilizoundwa na Serikali ya Awamu ya Tano ni ari na kasi ya watu kutaka kutekeleza majukumu yao. Niwasihi sana Waheshimiwa Wabunge, ninyi ni Viongozi wale walio kule ma-DC, Wakurugenzi ni Viongozi wenzetu. Tukiwa na tabia ya ku-interact, unafika pale usisikilize Madiwani tu wamekwambia kitu, basi unabeba, huyu hafai, amefanya hivi, sikiliza na upande wa pili.
Mheshimiwa Naibu Spika, tufahamu kwamba Wakuu wa Mikoa na Wakuu wa Wilaya ni Wenyeviti wa Kamati za Ulinzi na Usalama; na hivyo vyombo vya Ulinzi na Usalama viko chini yao wana taarifa ambazo wakati mwingine sisi hatuna. Kunaweza kukawa kuna mpango wa kufanya hujuma fulani na yeye anayo taarifa halisi, ya kweli, wewe huna.
Mheshimiwa Naibu Spika, Madiwani wanafika pale wanakukamata wanakwambia huyu hivi hivi na hivi na wewe unaamini. Unakwenda kuanza kusema, hapana, huyu anaingilia anafanya nini; tuwe na tabia ya ku-interact na hawa viongozi wenzetu itatusaidia. Itatusaidia sana kuyajua yaliyo ndani, kujua taarifa za siri, nani anafanya nini na wakati mwingine ningetamani kama ninavyoyajua mimi na nyie mngeyajua kwenye maeneo yenu yangesaidia kuondoa hii migongano. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa nafasi hii.