Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Hesabu za Serikali (PAC) pamoja na Maoni na Mapendekezo yaliyomo katika Taarifa hiyo; na Taarifa ya Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa (LAAC) pamoja na Maoni na Mapendekezo yaliyomo katika Taarifa hiyo

Hon. William Tate Olenasha

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ngorongoro

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Hesabu za Serikali (PAC) pamoja na Maoni na Mapendekezo yaliyomo katika Taarifa hiyo; na Taarifa ya Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa (LAAC) pamoja na Maoni na Mapendekezo yaliyomo katika Taarifa hiyo

NAIBU WAZIRI WA KILIMO, MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Naibu Spika, nami napenda kuchukua fursa hii kuzipongeza sana Kamati za PAC na LAAC kwa kazi waliyofanya kwa sababu kimsingi kupitia kwao Bunge limeendelea kufanya kazi yake ya Kikatiba ya kuisimamia na kuishauri Serikali.
Mheshimiwa Naibu Spika, Kamati ya PAC ilijadili na kutoa ushauri kuhusu upotevu wa fedha katika Wakala wa Taifa wa Hifadhi ya Chakula NFRA kutokana na mahindi yaliyoharibika. Kimsingi walishauri kwamba, namna mojawapo ya kuhakikisha kwamba hilo tatizo halijirudiii tena ni kutoa fursa kwa wakulima kuuza mahindi nje.
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali na Wizara imelichukua pendekezo hili na kimsingi kwa sasa hatuzuii wafanyabiashara kupeleka mahindi nje, lakini napenda kulieleza Bunge lako Tukufu kwamba, tunaruhusu chakula kipelekwe nje kulingana na ziada au hali halisi ya chakula ndani ya nchi. Kwa hiyo kuna wakati tunalazimika kupunguza kiwango kinachoenda nje si kwa sababu hatutaki wakulima wetu wanufaike na biashara ya chakula, lakini ni kwa sababu tunatanguliza maslahi mapana ya nchi ya kuhakikisha kwamba tunakuwa na usalama wa chakula.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika miezi ya hivi karibuni mnafahamu kwamba, tumekuwa tukichukua hatua kadhaa ili kuhakikisha kwamba, kunakuwa na usalama wa chakula kwa sababu majirani zetu hali yao si nzuri.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, naomba Waheshimiwa Wabunge pale unapoona kwamba, kuna kidogo kupunguza kasi ya kupeleka nje, mfahamu si kwa sababu hatutaki wakulima wetu wauze chakula nje.
Mheshimiwa Naibu Spika, pendekezo na ushauri mwingine ambao Serikali imeupokea ni kwamba, Wakala (NFRA) wajenge maghala kwa ajili ya kuongeza uwezo wa kuhifadhi chakula. Napenda kulitaarifu Bunge lako Tukufu kwamba, katika bajeti ambayo tunaitekeleza Wakala una mpango wa kuongeza uwezo wa kuhifadhi chakula kutoka tani 246,000 hadi kufikia tani 496,000 kwa sababu tuna mpango wa kujenga vihenge vyenye uwezo wa tani 190,000, lakini vilevile maghala yenye uwezo wa tani 60, 000. Vihenge na maghala hayo yatajengwa Babati, Dodoma, Shinyanga, Makambako, Mbozi, Songea, Sumbawanga na Mpanda.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika kuchangia hoja ya Kamati ya PAC, Waheshimiwa Wabunge walipata fursa vilevile ya kuzungumza baadhi ya masuala ambayo ningependa kuyatolea ufafanuzi. Mheshimiwa Omary Mgumba pamoja na Mheshimiwa Aeshi Hilaly walizungumzia sana kuhusu wafanyakazi wa NFRA waliosimamishwa kazi.
Mheshimiwa Naibu Spika, ningependa kutumia fursa hii kulieleza Bunge lako Tukufu kwamba, ni kweli kuna wafanyakazi wanne wa ngazi ya juu wa NFRA ambao wamesimamishwa kazi. Nisingependa kuzungumzia kwa undani kuhusu suala hilo kwa sababu tayari Wizara imeunda tume ili kuchunguza tuhuma ambazo zinawakabili na kimsingi itakuwa prejudicial, hatutawatendea haki tukianza kulijadili Bungeni na hata wale wanaofanya uchunguzi nao vilevile, si vizuri wakaingiliwa wakati bado wanaendelea na kazi.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kwa maelezo kidogo tu ni kwamba, wafanyakazi waliosimamishwa, tuhuma yao si hiyo tu inayosemekana na Waheshimiwa Wabunge, kuhusu uharibifu wa mahindi. Uharibifu wa mahindi ni moja tu kati ya masuala mengi ambayo tume ya Wizara iliyoundwa inachunguza. Kuna masuala kuhusu uuzaji wa mahindi; kuna malalamiko ambayo yanachunguzwa katika mchakato mzima wa kuuza mahindi, lakini vilevile kuhusu fedha zinazotokana na uuzwaji wa mahindi yenyewe…
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo ninachosema tu ni kwamba, tuvute subira, taarifa ikiwa tayari Waheshimiwa Wabunge mtataarifiwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana.