Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Hesabu za Serikali (PAC) pamoja na Maoni na Mapendekezo yaliyomo katika Taarifa hiyo; na Taarifa ya Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa (LAAC) pamoja na Maoni na Mapendekezo yaliyomo katika Taarifa hiyo

Hon. Fakharia Shomar Khamis

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Hesabu za Serikali (PAC) pamoja na Maoni na Mapendekezo yaliyomo katika Taarifa hiyo; na Taarifa ya Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa (LAAC) pamoja na Maoni na Mapendekezo yaliyomo katika Taarifa hiyo

MHE. FAKHARIA SHOMAR KHAMIS: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Kwanza nashukuru kwa kupata nafasi hii adhimu katika Bunge lako Tukufu ya kuweza kuchangia hoja ya PAC na LAAC kama hivi nitakavyoelezea.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza Kamati na CAG wote fedha za kufanyia kazi zilikuwa ndogo, lakini tumshukuru Mwenyezi Mungu kila mmoja ilibidi atekeleze wajibu wake ili suala hili liweze kufanikiwa. Ukweli ni kwamba kulikuwa na uhaba wa fedha za kufanyia kazi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nitaanza na Shirika la Taifa la Hifadhi ya Jamii (NSSF). Kulikuwa na hoja hapa ilizungumzwa kuhusu ujenzi wa Kigamboni ambapo NSSF waliingia mkataba na Azimio Housing Estate. Azimio House Estate ilikuwa watoe ekari 20,000 za ujenzi huo kulingana na makubaliano ya mkataba. Kiukweli ekari walizotoa ni 300. Makubaliano yao ilikuwa kama wangetoa ekari 20,000 ilikuwa na sawasawa na 20% ya hisa na 35% ya hisa ilikuwa ni kuchangia fedha, lakini hayo hayakuweza kutendeka na ndiyo maana ujenzi wa Kigamboni ukasuasua na kusimama kabisa.
Mheshimiwa Naibu Spika, maelezo ya Kamati aliyoeleza Mwenyekiti nakubaliana nayo kwamba kuundwe Kamati Ndogo iweze kusimamia na kufuatilia nini kilichokwamisha, nini ilikuwa tatizo hata makubaliano hayo hayakufikiwa na mradi huo ukawa haukuendelea. Taarifa hiyo baadaye iletwe Serikalini kuangaliwa na kujadiliwa hadi suala hilo liweze kukamilika.
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa napenda kuongelea Mfuko wa Pensheni ya Watumishi wa Umma. Mfuko wa Pensheni wa Watumishi wa Umma una matatizo, baadhi ya wastaafu wetu wanahangaika, hawalipwi na kutokana na upungufu uliojitokeza katika tathmini ya kitaalam kwa muda mrefu mfuko huo umekuwa unasuasua haufanyi kazi.
Mheshimiwa Naibu Spika, mimi naona mfuko huu unakwamishwa na Serikali, inatakiwa Serikali ikikopa kwenye mifuko hii iweze kulipa. Serikali imechukua fedha za mfuko huu na tumefanya kazi zetu, lakini hatulipi tutegemee hawa wastaafu wetu watapata fedha wapi na wanategemea walipwe na mfuko? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, ingawa tathmini iliyofanyika inaonesha kuanzia mwaka 1999 hadi leo wazee wetu wanahangaika. Wengine hawana watoto, wengine hawajiwezi, tunategemea hawa watapata wapi matumizi yao? Ingawa wamezungumzia kwamba wanategemea Februari watamaliza tathmini yao na waweze kuwalipa, hivi kweli mtu ataweza kukaa bila kutumia, bila kula mpaka ifike Februari? Naiomba na Serikali iweze kulipa madeni ya mashirika yake. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nizungumzie suala lingine la Bandari. Udhibiti wa mapato ya bandari kidogo uko hafifu, na kwanini nasema hivyo? Kuna meli nne zilikuja bandarini lakini hakuna mapato yaliyokusanywa kutokana na meli hizo kuwepo pale. Meli ziliondoka na baada ya kuondoka, baada ya muda wa miezi 18; CAG katika kuangalia taarifa kwenye vitabu vya hesabu za bandari ile anakuta kwamba meli nne zimeingia na zimetoka, makusanyo hayakupatikana kiusahihi na meli zimeshaondoka.
Mheshimiwa Naibu Spika, tuangalie ni meli ngapi zimeingia. Hizi nne CAG ameziona, je, hizo za nyuma ambapo siku nyingine hata kwenye vitabu hazikuingizwa? Inamaana wao wenyewe Bandari wanajikosesha mapato yao kutokana na kutokuwa udhibiti katika makusanyo yake.
Mimi ninampongeza Mheshimiwa Rais kwa kufanya ziara bandarini, kaujua udhaifu wa bandari yetu na ndiyo maana Mheshimiwa Rais ikabidi aende akaangalie hali halisi na sote tulisikia kwenye vyombo vya habari nini Mheshimiwa Rais alichogundua na matokeo yake yalikuwa nini. Ushauri wangu, naiomba bandari iweze kudhibiti mapato yao maana tunaitegemea kimapato. Wakiweza kudhibiti mapato yao ndipo Serikali yetu itakapoweza kufanyakazi na wananchi tutafaidika. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, ningeomba kuzungumzia Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA). Taarifa ya CAG inayoishia Juni 30, 2015 ilionesha kwamba misamaha ya kodi imepungua kufikia jumla ya bilioni 1.6, sawa na asilimia 15.1 kwenye makusanyo ya TRA. Ingawa tunasema misamaha ya kodi imepungua lakini Serikali bado inapoteza mapato yake kutokana na misamaha hiyo.
Mheshimiwa Naibu Spika, ninao mfano naweza kutoa. Kuna misamaha ya kodi iliyotolewa kwenye mafuta yenye thamani ya shilingi bilioni 22.3 ya Kampuni ya Uchimbaji Madini ya Geita na Resolute. Mafuta hayo badala ya kutumiwa na Kampuni ya Uchimbaji Madini ya Geita na Resolute wao wakawapelekea wakandarasi wengine kuyatumia. Sasa msamaha umepewa wewe kisha wewe unampelekea mwenzio, hilo si tatizo? Tena tatizo sugu.
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa ningeiomba Serikali, masuala kama haya CAG akishayaona lazima tuwe tunayafuatilia. Lakini wakati mwingine ufuatiliaji unashindikana kwa sababu fedha ambayo ndiyo nyenzo hakuna.
Kamati imetaka kufuatilia ili ipate uhakika, inashindwa kwenda kutokana na nyenzo ziko hafifu. Sasa nafikiri kwa haya machache niliyoyazungumza na yote ambayo yanakwamishwa na nyenzo za kifedha naomba kuunga mkono hoja.