Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa mwaka wa Fedha 2017/2018

Hon. Stella Ikupa Alex

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa mwaka wa Fedha 2017/2018

MHE. STELLA I. ALEX: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipatia nafasi hii na mimi niweze kuchangia mapendekezo haya ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa 2017/2018.
Awali ya yote napenda nimshukuru sana Mwenyezi Mungu kwa ajili ya ulinzi na mambo mengi ambayo anatujali sisi Waheshimiwa hapa ndani, na hasa mpaka tukafika kipindi hiki kuweza kuchangia mpango huu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia napenda niipongeze sana Serikali kwa sababu mimi ni Mbunge ambaye nipo katika kundi la vijana, katika mpango huu Serikali imeonesha ni jinsi gani ambavyo vijana wanaweza wakapunguziwa ugumu ama ukali wa maisha. Ukiangalia katika ukurasa wa 55 limeongelewa suala zima la ajira pamoja na mambo ya biashara, lakini pia yameongelewa na mambo ya kilimo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kwa sababu mimi ni mlemavu ninaomba niongelee masuala ambayo yanahusiana na watu wenye ulemavu katika mpango huu. Mpango huu ni mzuri na jukumu letu sisi Wabunge ni kuangalia ni mambo gani ambayo yanakosekana ili tuweze kuyaboresha ama tuweze kuyaongezea.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mpango huu mtu mwenye ulemavu ninamuona sehemu moja katika ukurasa wa 55, naomba ni nukuu, kuna hiki kipengele kimeandikwa kazi, vijana, ajira na wenye ulemavu. Kifungu (d) kinasema kwamba; “Kutenga maeneo maalum ya biashara ili kuwezesha vijana na wenye ulemavu kujiajiri.” Ni hapa tu ambapo ninamwona mtu mwenye ulemavu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba niishauri ama niiombe serikali yangu ya Chama cha Mapinduzi kwamba masuala ya ulemavu ni mtambuka, kwa hiyo ninapendekeza yafuatayo, nitaenda page wise nikianzia na huu ukurasa wa 55 hapa ambapo inaelezea kwamba; “kuendelea kutekeleza programu ya kukuza ajira kwa vijana.”
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba isomeke kwamba; kuendelea kutekeleza programu ya kukuza ajira kwa vijana na watu wenye ulemavu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia kuna suala la kuimarisha Mfuko wa Maendeleo wa Vijana. Sheria Namba 9 ya mwaka 2010 inaelezea jinsi ya kuanzisha Mfuko wa Taifa wa Watu Wenye Ulemavu. Mfuko huu ulianzishwa kisheria. Ukiangalia katika hii sheria kifungu namba 57 (1) kinaelezea unazishwaji wake na kifungu kidogo cha (2) kinaelezea vyanzo vya mapato. Katika hivi vyanzo vya mapato fedha inayoidhinishwa na bunge hili ni fedha ambayo ni mojawapo ya chanzo kikubwa cha mapato, kwa hiyo mimi niiombe Serikali kuutengea mfuko huu fedha
Mheshimiwa Mwenyekiti, kifungu cha tatu kinaelezea kazi za mfuko huu. Mfuko huu unakazi nyingi, na iwapo Serikali itautengea fedha kama ambavyo imefanya kwa Mfuko wa Vijana, mfuko huu utasaidia mambo mengi sana ya watu wenye ulemavu zikiwemo tafiti mbalimbali, mambo ya elimu lakini pia uwezeshwaji wa vyama vya watu wenye ulemavu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaona sasa hivi ni zaidi ya miaka mitatu ama miaka minne hivi vyama vya walemavu havipatiwi hata ruzuku, hivyo uwepo wa mfuko huu utasaidia mambo mengi sana kwa ajili ya watu wenye ulemavu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nakimbia kwaajili ya muda ninaomba niende ukurasa wa 56, niongelee suala la kilimo. Hapa naomba ninukuu, inasema; “kuongeza ushirika wa vijana katika kilimo.”
Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi naomba iseme kwamba; kuongeza ushiriki wa vijana na watu wenyeulemavu katika kilimo. Kwa nini ninasema hivi? Ninasema hivi kwa sababu katika maeneo mengi ambayo nimefanya ziara ama nimetembelea watu wenye ulemavu nikakuta ni wakulima, wanalima, kwa hiyo ni vizuri wakajumuishwa katika hili kundi. Watu wenye ulemavu wanalima si kwa kutumia matrekta, wanalima kwa nguvu zao. utakuta ni mtu mwenye ulemavu amekaa chini kabisa lakini analima pale pale chini alipo kaa, mimi nimeshuhudia kwa macho yangu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwahiyo niombe watu wenye ulemavu wajumuishwe katika hiki kipengele ili waweze kupewa elimu ya kilimo pamoja na biashara ili kuweza kuwaondolea ugumu wa maisha, lakini pia kuendelea kupunguza wimbi la omba omba la wenye ulemavu na tegemezi Tanzania.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba pia niongelee suala la afya. Kwenye suala zima la afya mtu mwenye ulemavu pia anaingia…
MHE. STELLA I. ALEX: Mheshimiwa Mwenyekiti, hili suala la afya pia ni muhimu sana kwa hili kundi la watu wenye ulemavu kwa sababu hata wakati naendelea na hizi ziara zangu afya ni moja ya vitu ambavyo watu wenye ulemavu waliviongelea na waliiomba sana Serikali iwasaidie kwenye suala la afya. Na pia niliulizwa maswali mengi ikiwemo bima ya afya, kuna watu wenye ulemavu ambao hawajiwezi kabisa.
Kwa hiyo, niiombe Serikali katika mpango huu iingize ama itenge fungu maalumu ambalo litawawezesha watu wenye ulemavu kupatiwa bima ya afya.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba niunge mkono hoja, naomba kuwasilisha.