Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa mwaka wa Fedha 2017/2018

Hon. Innocent Sebba Bilakwate

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kyerwa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa mwaka wa Fedha 2017/2018

MHE. INNOCENT S. BILAKWATE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi kuchangia.
Kwanza nichukue nafasi hii kuishukuru Serikali yangu ya Chama cha Mapinduzi kwa jinsi ambavyo imeendelea kushughulikia tatizo la tetemeko katika Mkoa wa Kagera, tunaipongeza sana Serikali yetu kwa jitihada zake.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia niipongeze Serikali kwa jinsi ambavyo imeshughulikia suala la ukame ambalo limeupata Mkoa wetu, tayari Serikali ya Chama cha Mapinduzi, Serikali sikivu imeshaleta chakula kuonyesha jinsi gani inavyowajali wana Kagera na wana Kyerwa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naishukuru Serikali lakini ombi langu niendelee kuiomba Serikali sisi Mkoa wa Kagera hatujawahi kupata njaa kiasi hiki, Serikali iendelee kuliangalia na ione ni namna gani ya kusaidia. Chakula kilicholetwa Kyerwa kilisaidia asilimia ifike hata asilimia kumi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, niombe Serikali bado tunahitaji chakula cha gharama nafuu. Lakini kuhusiana na suala la tetemeko niombe Serikali kuna wananchi ambao wanauwezo wa kuweza kujenga nyumba zao, lakini wananchi wengi hawana uwezo na ukilinganisha hali halisi ambayo tumeipata ya ukame.
Mimi niiombe Serikali bado tunahitaji wananchi wasaidiwe wale ambao hawana uwezo Serikali ione namna gani ambavyo inaweza kuwasaidia hasa hasa wale ambao hawajiwezi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusiana na mpango niipongeze Serikali, mpango huu ni mzuri, una mambo ambayo ni mazuri. Lakini kuna mambo ambayo nataka nishauri, tunaposema tunataka kuingia Tanzania iwe ni ya viwanda kuna mambo ambayo tunabidi tuyaangalie; kwa mfano, suala la wakulima, sijaona kama limepewa nafasi kubwa nchi hii asilimia kubwa tunategemea kilimo, lakini hiki kilimo bado hatujawa na kilimo ambacho ni cha kisasa. Asilimia kubwa ya Watanzania wanategemea kilimo cha kutumia jembe ya mkono, lakini mazingira yenyewe haya ya kilimo wananchi bado sio mazuri, mwananchi anapolima bado hana soko la uhakika. Niiombe Serikali katika mpango wake iweke mazingira ambayo ni mazuri, mwananchi anapolima apate mahala pakuuza mazao yake. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine sasa hivi nchi yetu wametangaza maeneo mengi tutakumbwa na ukame. Tanzania tuna vyanzo vingi vya maji hata ukija kwetu kule Kagera, niombe Serikali iwekeze nguvu kubwa kwenye kilimo cha umwagiliaji, tutapata chakula kingi lakini tutaweza kupata chakula hata cha kuuza. Ninaamini tukiwekeza kwenye kilimo tutapata pesa nyingi ambayo itainua uchumi wetu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine kwenye upande wa ardhi niombe Serikali kama ambavyo imekuwa ikiendelea kushughulikia matatizo ya migogoro ya ardhi, Serikali ili iweze kufanikiwa katika mpango wake lazima tupambane na hizi kero ambazo ziko kwa wananchi wetu, tuainishe yale maeneo ambayo tayari yalishatengwa na Serikali kwa ajili ya wakulima yajulikane na yale ambayo yalishatengwa kwa ajili ya wafugaji yajulikane. Kwa mfano kama kule kwetu Kyerwa kuna mgogoro mkubwa wa ardhi, kuna ardhi ambayo ilishatengwa kwa ajili ya wafugaji. Ardhi hii imeporwa na wezi, wameingia humo tayari Serikali ilishatangaza kuwa hili eneo ni la wafugaji, lakini wameingia watu wamejiwekea fensi humo, wananchi hawana maeneo ya kufugia. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naamini haya maeneo yatakapotengwa wafugaji wakapata maeneo ya kufugia tutapata maziwa, tutaweza kuanzisha viwanda. Niiombe sana Serikali tunaposema tunaingia kwenye Serikali ya viwanda tuhakikishe hii migogoro inaondoka.
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ili tuweze kufanikiwa lazima wananchi wetu wawe na afya nzuri. Kwa upande wa afya bado tuseme ukweli tatizo bado lipo, wananchi hawana dawa, lakini wananchi hao hao ambao hakuna dawa za kutosha kwenye zahanati, hatuna maji ya uhakika. Hawa wananchi hawana maji safi na salama, hawana dawa za kutosha hospitalini wanapoumwa watapelekwa wapi? Niiombe Serikali tuwekeze nguvu kubwa kwenye zahanati zetu, kwenye maji ili maisha ya wananchi yaweze kuwa mazuri. Tunaposema tunaingia kwenye... (Makofi)
MHE. INNOCENT S. BILAKWATE: ...vizuri wananchi wetu wakawa na afya bora, tuboreshe…
MWENYEKITI: Ahsante.