Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa mwaka wa Fedha 2017/2018

Hon. Katani Ahmadi Katani

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tandahimba

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa mwaka wa Fedha 2017/2018

MHE. KATANI A. KATANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru pia kwa kunipa fursa hii. Nitaanza na suala la utawala bora ambalo lipo kwenye mapendekezo ya mpango huu tunaozungumza. Wakati tunazungumza suala la utawala bora sisi Watanganyika ambao tumejipa mamlaka ya kuwa Tanganyika sasa kuwa Gereza la Guantanamo Bay kwa kuwachukua Wazanzibari na kuwaleta Tanganyika bado watu mkazungumza suala la utawala bora, hatuwezi kuiendesha nchi na tukawa na mipango mizuri kama kuna watu wanadhulumiwa, kuna watu wanaonewa, bado mkaendelea kuzungumza mipango hii. Na kaka yangu Mheshimiwa Mwigulu, hili nalo lazima uliangalie sana kwa sababu linakugusa pia, ulione kwamba ni jambo la msingi tunapozungumza suala la mipango, suala la utawala bora na wa sheria ni lazima lizingatiwe kwa namna yoyote ile, ndiyo tutakwenda mbele. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini wakati nasoma ukurasa wa 62, mmezungumzia suala la Benki ya Maendeleo ya Kilimo, niliona miaka ya nyuma Benki ya Maendeleo ya Kilimo ikiwa Dar es Salaam, wakulima wenyewe wanapatikana Tandahimba, sasa ni mambo ya ajabu na vichekesho kwa Taifa hili, mnazungumza benki ambayo iko Dar es Salaam, wakulima wa Rujewa kule Mbarali, wakulima wa korosho wa Tandahimba hakuna wanachonufaika na benki hiyo ambayo inayokaa Dar es Salaam, ni jambo la ajabu sana. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, hili nina ushahidi wakati hata mmeleta trekta, watu wangu wa Tandahimba mpaka leo, wajanja wachache wameshachukua matrekta, wenyewe wakulima wa Tandahimba hawajachukua. Sasa wakati mnazungumza suala hili la Benki ya Maendeleo ya Kilimo basi mhakikishe na watu wa Tandahimba, watu wa Rujewa kule vijijini wananufaika na jambo hili la Benki ya Kilimo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati mnazungumza mambo haya mmezungumza suala la barabara ambalo nimeliona, suala la barabara ile ya Masasi – Mtwara – Newala – Tandahimba, ukaizungumzia ile ya Masasi – Songea – Tunduru, bahati nzuri hii ya Masasi – Songea – Tunduru inakwenda vizuri sana. Lakini hii ya kwetu ya kutoka Mtwara – Tandahimba – Newala, pamoja na kwamba umepitisha bajeti na wananchi wakakubali kubomoa mabanda yao yaliyo barabarani, mpaka leo hakuna kinachoeleweka na tunaandaa sasa mpango wa mwaka unaofuata. Hili ni jambo la ajabu na linaweza likawaangusha Serikali ya CCM, sasa kama mnataka mipango iende, tutekeleze kwanza tuliyokubaliana halafu ndiyo mlete mipango ambayo inaweza ikawasaidia Watanzania hawa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, mmezungumza suala la viwanda. Suala la viwanda, Mheshimiwa Waziri wa Fedha nikwambie tu kwamba Kusini, kwa maana ya Mtwara na Lindi tulikuwa na viwanda vya korosho vya kutosha, viwanda ambavyo mmeuza kwa bei chee, tena kwa njia za panya, zaidi ya viwanda vinane tulikuwa navyo, sasa kama mna dhamira ya dhati muone namna gani mnakwenda kuvichukua vile viwanda. Na hili linawezekana kwa Serikali yenu, kwa sababu ni Serikali tu ikiamua jambo inafanya, sasa tuone viwanda vile vya korosho kule mnavichukua ili watu wa Mtwara na Lindi waweze kunufaika na viwanda vile. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, wenzangu wamezungumza hapa, suala la single customer territory, napata shida kwenye jambo hili, kama makusanyo ya ndani yametushinda, tunakuja kujibebesha mzigo wa kukusanya na pesa za watu wa Kongo, Zambia, hii ni akili ya wapi? Una mzigo wa magunia wa kilo 200 umeshindwa kuubeba mwenyewe unasema niongezee kilo 400, hili ni Taifa la ajabu sana. Nikuombe sana, mlikwenda kwenye jambo hili mkiwa mmeshirikiana na watu wa Kenya kwenye suala la VAT kwenye suala la utalii, Wakenya wakatukimbia, leo tumeingia mkenge kwenye jambo hili tayari bandari yetu inadorora ambayo inaleta zaidi ya asilimia 60 ya Pato la Taifa hili.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nikuombe sana Mheshimiwa Dkt. Mpango, wewe ni msomi mzuri na mara zote tukiwaambia muwe mnapokea ushauri, sio kila kinachozungumzwa na upinzani ni maneno ambayo tunaiudhi Serikali, sisi tunajua nchi hii ni ya Watanzania wote na tunazungumza kwa maslahi ya Taifa la Tanzania hatuzungumzi kwa maslahi ya Chama cha Mapinduzi, hatuzungumzi kwa maslahi ya Chadema, hatuzungumzi kwa maslahi ya CUF. Tunapotoa hoja za msingi za Kitanzania pokeeni hoja na mzifanyie kazi badala ya kukaa hapa mnatuletea ngonjera, mnazungumza majungu, mnazungumza mipasho, tuzungumze kauli za Kitanzania, tuwakomboe Watanzania wachache ambao wanapata shida huko vijijini. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana.