Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa mwaka wa Fedha 2017/2018

Hon. Leah Jeremiah Komanya

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Meatu

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa mwaka wa Fedha 2017/2018

MHE. LEAH J. KOMANYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kukushukuru kwa kunipatia nafasi hii na mimi niweze kuchangia mpango wa bajeti kwa mwaka 2017/2018. Kwanza, napenda kumpongeza Mheshimiwa Waziri kwa mpango mzuri aliotuletea. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kabla ya kuchangia, naomba niunge mkono mpango huu ila naomba nishauri katika maeneo yafuatayo na Mheshimiwa Waziri aweze kuzingatia ushauri wangu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nitaanza kuchangia kuhusu madeni ya ndani na nitajikita zaidi katika madeni ya Halmashauri. Halmashauri zetu zinakabiliwa na madeni makubwa ambayo yanaleta ugumu katika utendaji wa kazi. Napenda ku-declare interest nilikuwa mtumishi katika Serikali za Mitaa pia ni Mjumbe wa Kamati ya Hesabu za Serikali za Mitaa. Madeni haya yamegawanyika katika sehemu mbalimbali naomba niyataje, madeni ya wazabuni, ya watumishi na ya mradi kwa mradi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Halmashauri zinapata ugumu katika ulipaji wa madeni haya kutokana na baadhi ya Halmashauri vyanzo vyao vya mapato ni vidogo. Kwa hiyo, kutegemea Halmashauri ziweze kulipa madeni haya mambo mengi yatakwama kwa sababu wazabuni wamekopa mikopo, watumishi wanahitaji malipo yao na miradi kwa miradi inadaiana. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, madeni haya nayazungumzia kwa sababu nina hoja za msingi, yamesababishwa na upelekaji kidogo wa fedha ambapo Serikali ilikuwa inatekeleza majukumu mengine muhimu ya kitaifa. Sababu nyingine ni Halmashauri zilitekeleza maagizo mbalimbali mengine ya Serikali ambayo ni muhimu na tumeona matokeo yake ikiwepo ujenzi wa maabara. Kwa hiyo, Halmashauri zimeachwa na madeni makubwa. Mheshimiwa Waziri naomba katika mpango wako uweke mpango pia wa kuzisaidia Halmashauri kulipa madeni. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, hoja yangu ya pili naunga mkono uamuzi wa Serikali wa kuhamisha ukusanyaji wa kodi ya majengo kukusanywa na TRA. Ninazo sababu za msingi. Kwanza, baadhi ya Halmashauri zilikuwa hazina takwimu za majengo yanayopaswa kukusanywa kodi ya majengo, hazikuwa na makadirio yanayoeleweka ya kukusanya mapato hayo zilikuwa zikikadiria mapato kidogo. Hata yale mapato kidogo yaliyokuwa yakikadiriwa ukusanyaji wake ulikuwa ni hafifu sana. Hivyo tu niishauri Serikali mfumo wa Taifa wa kukusanya mapato ya Serikali za Mitaa uzifikie Halmashauri kwa wakati na fedha hizo zikipatikana basi zirejeshwe haraka Halmashauri ili waweze kutekeleza shughuli zao.
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kuipongeza Serikali kwa namna inavyokusanya mapato kikamilifu na imekuwa ikivuka malengo. Hata hivyo, ukusanyaji huu wa mapato kikamilifu hauwezi kupunguza umaskini walionao wananchi wetu. Serikali inapaswa iwekeze kikamilifu katika sekta zinazogusa maisha ya wananchi moja kwa moja zikiwemo kilimo, mifugo na uvuvi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda niongelee upande wa kilimo cha pamba. Sekta ya pamba bado inakabiliwa na changamoto nyingi ambazo zinapelekea wakulima kuanza kujiondoa kuzalisha zao hilo. Baadhi ya changamoto ni ukosekanaji na uhafifu wa pembejeo wanazopewa wakulima. Wakulima wamekuwa wakipewa pembejeo hafifu kwa mfano mwaka jana dawa za kuua wadudu hazikufanikiwa, ziliwafanya wale wadudu wasinzie. Kwa mwaka huu dawa ziko kidogo, ziko kama kopo 500.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba Serikali iweke mpango wa kuhakikisha pembejeo zinapatikana kwa wingi kwa sababu wananchi wamepata pia mwamko wa kulima kutokana na bei ya pamba iliyotolewa mwaka jana ambayo Mheshimiwa Rais aliisimamia na wakulima wakapata angalau bei iliyoweza kuwanufaisha kidogo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, changamoto nyingine ni kukabiliwa na tatizo la mbegu. Ipo mbegu ya UK91 ambayo imeingia sokoni kwa muda mrefu na kupoteza ubora wake. Mbegu hii imekuwa ikipandwa na wakulima wakati mwingine imekuwa haioti na kusababisha umaskini kwa wakulima wetu. Nashauri Serikali iweke mpango kwa mwaka 2017/2018 wa kuidhinisha mbegu mpya ya pamba ili iweze kuinua uchumi wa wananchi hasa Kanda ya Magharibi, zao la pamba linategemewa katika uchumi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimalizie kwa kuongelea afya. Wakati tukichangia bajeti ya mwaka 2016/2017, yalitoka matamko ya Serikali kwamba Serikali inajipanga kufanya tathmini ya ujenzi wa zahanati na vituo vya afya. Kwa hiyo, natumaini safari hii mpango mzuri utakuwepo na bajeti ya kutosha itawekwa ili kuweza kukamilisha ujenzi wa zahanati na vituo vya afya. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kuna ufadhili ambao unatolewa kwa kitengo cha afya kwa ajili ya utekelezaji wa shughuli ambazo siyo za construction. Tumeona wafadhili wakitoa fedha za result based financing. Naomba vigezo vinavyotumika vipitiwe upya kwa sababu ili hospitali ya wilaya au kituo cha afya kiweze kufuzu kupata fedha hizi inatakiwa zifikie nyota tano. Vituo hivi vya afya au zahanati zinawezaje kufuzu kupata hizo nyota tano ili ziweze kupata fedha hizo kwa sababu ukiangalia changamoto nyingi zinasababishwa na Serikali. Kwa hiyo, inakuwa viko nje ya uwezo wa Halmashauri. Naomba yafanyike upya mapitio ya vigezo hivi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hayo, machache naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja.