Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa mwaka wa Fedha 2017/2018

Hon. Mashimba Mashauri Ndaki

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Maswa Magharibi

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa mwaka wa Fedha 2017/2018

MHE. MASHIMBA M. NDAKI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ili nami pia niweze kuchangia mapendekezo haya ya Mpango wa Maendeleo wa mwaka 2017/2018.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kama ambavyo Mheshimiwa Mapunda amesema. Nilidhani kwamba tungekuwa na rejea ambayo inatuelekeza ni kwa namna gani angalau tumejaribu kufanya kwa mwaka huu ambao unaelekea mwishoni, ingekuwa nzuri sana; lakini sasa tumekosa hiyo. Wakati nasoma haya mapendekezo nikawa najiuliza, hivi inakuwaje mtu anafikiria kuoa mke wa pili wakati huyu wa kwanza hata hajamwoa? (Kicheko/Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa unamwita mke wa pili au mke wa kwanza? Sasa kwa kweli hiyo tu ndiyo imeleta shida kwenye mapendekezo haya.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nadhani ni vizuri kama ndiyo taratibu zetu, kanuni zetu au sheria zetu, basi ni vizuri kuzibadilisha ili tupate angalau matokeo ya miezi sita ya mpango ule uliopo kwenye mwaka, halafu tuweze kuangalia sasa tunapendekeza nini. Vinginevyo inakuwa ngumu kweli kweli kuchangia. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme kitu cha pili kabla sijatoa mchango wangu. Cha pili ni kwamba, mwaka 2015 tulipokuwa kwenye uchaguzi kila mtu alikuwa anaimba mabadiliko. Mabadiliko ni rahisi kuyaimba lakini yana tabia moja ambayo siyo nzuri wakati mwingine. Mabadiliko yana tabia ya kumtoa mtu kwenye comfort zone yake. Sasa inaelekea Serikali hii ya Awamu ya Tano, kwa sababu imevaa njuga za mabadiliko, watu wengi hatufurahii.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni ukweli kwamba kama tunataka mabadiliko, ni lazima tutoke kwenye comfort zone tuliyokuwa tumezoea. Haiwezekani ukataka kwenda Peponi au Mbinguni bila kufanya ibada. Ibada nyingine ni mara tano kwa siku, nyingine inabidi uache kula na kunywa, lengo tu ufike Peponi au Mbinguni.
Sasa kuna vitu ambavyo sisi kama wananchi na Serikali yetu kama kweli tunataka mabadiliko yaliyo ya maana, vitu vingine inabidi tuvisahau na vitu vingine inabidi tuviache kwa sababu tunataka mabadiliko. Hatuwezi kufikia mafanikio ikiwa tutataka tukae kwenye raha ile tuliyokuwa nayo miaka 50 iliyopita. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Waheshimiwa Wabunge ni lazima tulielewe hilo hata tunapojadili hali ngumu za maisha zinazowakabili watu wetu, tujue kuwa hiyo ndiyo hali halisi ya kutaka mabadiliko.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kitu cha pili ni kwamba humu Bungeni kuna kitu ambacho mimi sijakipenda sana kinatugawa Wabunge. Kuna kitu kinasemwa na Wabunge wengi wewe huwajui wapiga kura, wewe hukupigiwa kura, kuna mtu hakupigiwa kura humu ndani?
MBUNGE FULANI: Ndio.
MHE. MASHIMBA M. NDAKI: Hapana. Mimi naamini kila Mbunge amepigiwa kura hapa, kura zetu zinatofatiana idadi tu, Mheshimiwa Mpango amepigiwa kura moja akawa Mbunge. Mimi nimepigiwa kura makumi elfu nikawa Mbunge, wenzetu wa Viti Maalum wamepigiwa kura kadhaa ni Wabunge, sasa tunapofika humu na kuanza kugawanyana wewe hujapigiwa kura, wewe huwajui wapiga kura, kila mtu anajua mpiga kura wake.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninachotaka kutahadharisha tu ni kwamba Mheshimiwa Mpango kura yako wewe ni moja ukapata Ubunge, lakini nyuma ya kura moja kuna kura mamilioni ya Watanzania yaliyompa kura aliyekupa wewe kura. Kwa hiyo, aliyekupa kura anatarajia mamilioni ya kura za Watanzania waliompigia waguswe kupitia wewe. Wewe ni Mbunge kabisa halali wa kupigiwa kura, ni Mbunge halali na Uwaziri wako ni halali, lakini kumbuka kuna kura nyingi huko nyuma ya kura yako zinataka kuguswa na wewe. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa niende kwenye kuchangia mapendekezo. Kitu cha kwanza mapendekezo yanasema kufungamanisha maendeleo ya uchumi na maendeleo ya watu, ninakubaliana nayo, lakini ili maendeleo ya watu yaonekane yamefungamanishwa na maendeleo ya uchumi lazima ionekane kwamba katika huduma zile za kijamii ambazo zinagusa watu wengi, wananchi wetu wanazipata kwa urahisi kwa gharama nafuu, wanazipata wanapozihitaji. Hali ilivyo, wakati huu kwa kweli haiko namna hiyo, kwa sababu mpango ambao tuko nao sasa hivi haujawahi kutekelezwa kikamilifu kiasi cha kugusa maeneo yanayogusa wananchi wengi, kwa mfano afya, elimu na mambo mengine. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa tunapotaka kukuza uchumi wetu ili ufungamane na maendeleo ya watu lazima tufanye juu chini katika mapendekezo haya tufanye juhudi zile zinazogusa wananchi wetu hasa wanyonge. Tusipofanya hivyo hatutafungamanisha maendeleo ya uchumi wetu unakua ndio, lakini watu wetu watabaki kwenye hali zile zile, kwa hiyo ni ushauri wangu wa kwanza huo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine tunatakiwa tuwe na miradi ya kielelezo ndiyo, lakini miradi ya kielelezo kutoka mwaka juzi, kutoka miaka ya nyuma sana mpaka tunaendelea na kuendelea nayo nadhani pia hii sio mpango mzuri, sio utaratibu mzuri. Nimejaribu kuangalia mapendekezo ya mpango huu, mimi nikawa nafikiri ningekuta kuna mradi angalau mmoja wa kielelezo wa umwagiliaji lakini hakuna. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa napendekeza ni vizuri na ni muhimu sana tukaangalia kwa sababu tumekwishakupewa taarifa, hali ya hewa ya mwaka tunaoundea sio nzuri. Watu wa hali ya hewa wametuambia, lakini pia mabadiliko ya tabia nchi yanatueleza hivyo, hali sio nzuri ya mvua zitakazonyesha baadae, lakini tuna eneo na maeneo makubwa ambayo yangeweza kumwagiliwa yakatupa chakula na mazao ya biashara.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye mapendekezo haya unaona vitu vingine tu lakini jambo la umwagiliaji ambalo lingetupa maji ya uhakika halijawekewa msimamo, ambalo lingetupa mazao kila wakati, halijawekewa mpango, sasa tunafanyaje? Nahisi habari hii ya kuwa na umwagiliaji mkubwa ni ya muhimu sana kuwekwa kwenye mpango kwa sababu tuna vyanzo vya maji vingi, maziwa matatu makubwa na mito mikubwa tunayo hapa nchini kwetu, hilo ni la kwanza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili ni uvuvi wa bahari kuu, hatujaona humu kama kwenye mpango kunapendekezwa kitu chochote. Mheshimiwa Rais ameimba wakati wa kampeni anasema anashangaa kwa nini ukanda wetu wa Pwani hakuna hata kiwanda kimoja cha samaki, hakuna. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia tunashangaa hatuna meli ya kuvua hata moja ambayo ingeweza kununuliwa na Serikali kwa bei ambayo iko chini ya bei ya Bombardier, inawezekana kabisa tukinunua meli moja tunaweza tukawa na uvuvi mkubwa kwenye bahari kuu. Lakini kwenye mapendekezo haya unaona tu uvuvi umetajwatajwa tu kifupi kifupi tu lakini hakuna seriousness yoyote ambayo unaiangalia na kuiona iko humo ndani. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kitu cha tatu ambacho nimekikosa ni mazao yetu makuu ya biashara kwenye mpango, kwenye mapendekezo hayapo, lakini ukijaribu kuangalia takwimu mazao yetu makuu ya biashara korosho, tumbaku, kahawa, pamba mazao haya uzalishaji wake unapungua kila mwaka, uko chini lakini kwenye mapendekezo hakuna kitu chochote kinachotajwa angalau mkakati kuonyesha ya kwamba tuna mkakati wa maana kupandisha uzalishaji wa mazao haya ili tuweze kupata hela nyingi za kigeni, lakini pia watu wetu waweze kujipatia kipato kwa sababu ndio wengi wanaolima mazao haya.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nilitaka nipendekeze pia kwamba mapendekezo haya ya mpango yajaribu kuangalia mazao makuu ya biashara tunafanyaje juu ya haya ili kwamba kuweza kupandisha kipato cha wananchi wetu. Mengi ya mazao haya tunauza yakiwa ghafi, kwenye mapendekezo ya mpango hakuna dalili zozote ya kuyageuza ili angalau tuyauze yakiwa na value added, hakuna, sasa tunafanyaje?
Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nilitaka kusema hayo machache tu nashukuru sana kwa kunipa nafasi.